Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Waliwapa Mbwa Wangu Biskuti

Waliwapa Mbwa Wangu Biskuti

NICK anayeishi Oregon, Marekani, anaandika hivi: “Mwanzoni wa mwaka wa of 2014, nilianza kuwatembeza mbwa wangu wadogo katika sehemu fulani ya mji wetu. Mashahidi walikuwa wanasimama kwa ukawaida katikati ya jiji, karibu na vigari vyao vya machapisho. Walikuwa wamevalia vizuri, na walimsalimu kila mtu kwa tabasamu changamfu.

“Mashahidi hao hawakuwatendea tu kwa fadhili watu, bali pia mbwa wangu. Siku moja, Elaine, aliyekuwa amesimama kando ya kigari cha machapisho, aliwapatia mbwa wangu wawili biskuti. Baada ya hapo, kila mara tulipokaribia kigari cha machapisho, mbwa walikuwa wakivuta kamba kuelekea sehemu ambayo walipewa biskuti.

“Miezi mingi ilipita. Mbwa walifurahia kula biskuti, nami nilifurahia mazungumzo mafupi pamoja na Mashahidi. Lakini sikutaka kuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja nao. Nilikuwa na umri wa zaidi ya miaka 70 na sikuwa na uhakika na mambo ambayo Mashahidi waliamini. Nilikuwa nimekatishwa tamaa na makanisa ya Kiprotestanti, hivyo niliamua kujifunza Biblia peke yangu.

“Wakati huo, niliwaona Mashahidi wengine katika sehemu tofauti za jiji, wakiwa wamesimama kando ya vigari vyao vya machapisho. Wao pia walikuwa wenye urafiki. Sikuzote walijibu maswali yangu kwa kutegemea Biblia, na matokeo yake nilianza kuwaamini zaidi.

“Siku moja, Elaine aliniuliza hivi: ‘Je, unaamini kwamba wanyama ni zawadi kutoka kwa Mungu?’ Nikajibu, ‘Ndiyo, ninaamini hivyo! ’ Kisha Elaine akanisomea Isaya 11:6-9. Kuanzia hapo, nilitaka kujifunza mengi zaidi kuhusu Biblia, lakini bado nilisita kuchukua machapisho.

“Katika siku zilizofuata, nilifurahia mazungumzo mafupi lakini yenye kuvutia na Elaine pamoja na Brent, mume wake. Walipendekeza kwamba nisome kitabu cha Mathayo hadi Matendo ili kuelewa mambo yanayohusika ili kumwiga Kristo. Nami nikafanya hivyo. Baada ya muda mfupi, nilikubali kujifunza Biblia pamoja na Brent na Elaine. Ilikuwa katikati ya mwaka wa 2016.

“Nilitazamia kwa hamu kujifunza Biblia kila juma na kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Nilihisi nimebarikiwa na mwenye furaha kwa kujifunza mambo ambayo kwa kweli Biblia inasema. Baada ya mwaka mmoja hivi, nilibatizwa na kuwa Shahidi. Sasa nikiwa na umri wa miaka 79, ninajua kwamba niko katika njia sahihi. Yehova amenibariki kwa kunikaribisha katika familia yake ya watumishi waliojiweka wakfu.”