Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 18

Jinsi ya Kujiwekea na Kufikia Malengo ya Kiroho

Jinsi ya Kujiwekea na Kufikia Malengo ya Kiroho

“Tafakari mambo haya; zama katika hayo, ili maendeleo yako yaonekane wazi kwa watu wote.”​—1 TIM. 4:15.

WIMBO 84 Tumejitoa Kutumikia

MUHTASARI *

1. Tunaweza kujiwekea malengo gani ya kiroho?

 TUKIWA Wakristo wa kweli, tunampenda sana Yehova. Tunataka utumishi wetu kwake uwe wa kiwango bora kabisa. Hata hivyo, ili tufaulu kutumia uwezo wetu wote, tunahitaji kujiwekea malengo ya kiroho, kama vile kusitawisha sifa za Kikristo, kujifunza ustadi muhimu, na kutafuta njia za kuwatumikia wengine. *

2. Kwa nini tunapaswa kujiwekea malengo ya kiroho na kujitahidi kuyafikia?

2 Kwa nini tupendezwe na kufanya maendeleo ya kiroho? Jambo muhimu ni kwamba tunataka kumfurahisha Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo. Yehova anafurahi anapoona tukitumia kikamili vipawa na uwezo wetu katika utumishi wake. Pia, tunataka kufanya maendeleo ya kiroho ili tuweze kuwasaidia zaidi ndugu na dada zetu. (1 The. 4:9, 10) Haidhuru tumekuwa kwenye kweli kwa muda mrefu kadiri gani, sote tunaweza kufanya maendeleo ya kiroho. Acheni tuone jinsi tunavyoweza kufanya hivyo.

3. Kama inavyoonyeshwa kwenye 1 Timotheo 4:12-16, mtume Paulo alimtia moyo Timotheo afanye nini?

3 Mtume Paulo alipomwandikia Timotheo barua yake ya kwanza, tayari mwanamume huyo kijana alikuwa mzee mwenye uzoefu. Hata hivyo, bado Paulo alimtia moyo azidi kufanya maendeleo ya kiroho. (Soma 1 Timotheo 4:12-16.) Unapofikiria maneno ya Paulo, utatambua kwamba alitaka Timotheo afanye maendeleo katika njia mbili: kwa kusitawisha sifa za Kikristo kama vile upendo, imani, usafi wa kiadili na kwa kuboresha ustadi mbalimbali kama vile kusoma mbele ya watu, kuhimiza, na kufundisha. Tukiwa na mfano wa Timotheo akilini, acheni tuone jinsi kujiwekea malengo yanayofaa kunavyoweza kutusaidia kufanya maendeleo ya kiroho. Pia, tutachunguza baadhi ya njia tunazoweza kupanua huduma yetu.

SITAWISHA SIFA ZA KIKRISTO

4. Kulingana na Wafilipi 2:19-22, ni nini kilichomfanya Timotheo awe mtumishi mwenye thamani wa Yehova?

4 Ni nini kilichomfanya Timotheo awe mtumishi mwenye thamani wa Yehova? Ni sifa zake za Kikristo zenye kutokeza. (Soma Wafilipi 2:19-22.) Kutokana na jinsi Paulo alivyomzungumzia Timotheo, tunaweza kuona kwamba alikuwa mnyenyekevu, mshikamanifu, mwenye bidii, na aliyetegemeka. Aliwapenda na kuwajali sana akina ndugu. Matokeo ni kwamba Paulo alimpenda Timotheo, naye hakusita kumkabidhi migawo migumu. (1 Kor. 4:17) Vivyo hivyo, Yehova atatupenda na tutakuwa na thamani zaidi kutanikoni, ikiwa tutasitawisha sifa anazozipenda.​—Zab. 25:9; 138:6.

Chagua sifa ya Kikristo ambayo ungependa kuiboresha zaidi (Tazama fungu la 5 na 6)

5. (a) Unaweza kuchukua hatua gani unapojiwekea lengo la kusitawisha sifa fulani ya Kikristo? (b) Kama inavyoonyeshwa kwenye picha, dada huyo anafanya nini ili kutimiza lengo lake la kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi?

5 Chagua lengo hususa. Sali na uchunguze ni sehemu gani ya utu wako unayohitaji kuboresha. Chagua sifa moja hususa ambayo ungependa kukazia fikira. Kwa mfano, unaweza kusitawisha zaidi sifa ya hisia-mwenzi au kuimarisha zaidi tamaa yako ya kuwasaidia waabudu wenzako. Je, unahitaji kuwa mwenye kufanya amani zaidi na mwenye kusamehe? Unaweza kupata msaada kwa kumwomba rafiki unayemtumaini, akupe mapendekezo kuhusu mambo unayoweza kuboresha.​—Met. 27:6.

6. Unaweza kufanya nini ili kutimiza lengo la kusitawisha sifa fulani?

6 Jitahidi kufikia lengo lako. Unawezaje kufanya hivyo? Njia moja ni kwa kuchunguza kwa makini sifa unayotaka kuboresha. Tuseme unataka kuboresha sifa ya kuwasamehe wengine. Unaweza kuanza kwa kusoma na kutafakari mifano ya Biblia ya wale waliowasamehe wengine kwa hiari, na wale ambao hawakufanya hivyo. Fikiria mfano wa Yesu. Aliwasamehe wengine kwa hiari. (Luka 7:47, 48) Pia, hakukazia fikira makosa yao ya wakati uliopita, badala yake, alikazia fikira sifa zao nzuri. Kinyume chake, Mafarisayo katika siku za Yesu ‘waliwadharau watu wengine.’ (Luka 18:9) Baada ya kutafakari mifano hiyo, jiulize hivi: ‘Ninaona nini ninapowatazama wengine? Kati ya sifa walizo nazo, ninachagua kukazia fikira sifa gani? Ikiwa unapambana ili kumsamehe mtu fulani, jitahidi kuandika orodha ya sifa nzuri za mtu huyo. Kisha, ujiulize hivi: ‘Yesu anamwonaje mtu huyu? Je, angemsamehe?’ Mradi kama huo wa kujifunza unaweza kutusaidia kubadili maoni yetu. Mwanzoni, huenda tukalazimika kujitahidi sana ili kumsamehe mtu fulani aliyetukosea. Lakini ikiwa tutaendelea kuboresha utu wetu, baada ya muda tutakuwa tayari zaidi kuwasamehe wengine.

JIFUNZE USTADI WENYE MANUFAA

Jitolee kujifunza kazi ya udumishaji katika Jumba lenu la Ufalme (Tazama fungu la 7) *

7. Kulingana na Methali 22:29, ni katika njia gani Yehova anawatumia wafanyakazi wenye ustadi leo?

7 Lengo lingine unaloweza kujiwekea ni kujifunza ustadi wenye manufaa. Fikiria idadi kubwa ya wafanyakazi wanaohitajika ili kujenga majengo ya Betheli, Majumba ya Makusanyiko, na Majumba ya Ufalme. Wengi kati ya wafanyakazi hao wanapata ustadi wao kwa kufanya kazi pamoja na akina ndugu ambao ni mafundi wenye uzoefu. Kama inavyoonyeshwa kwenye picha, ndugu na pia akina dada wanajifunza ustadi ambao unahitajika ili kusaidia kudumisha Majumba ya Makusanyiko na Majumba ya Ufalme. Kwa njia hiyo, na njia nyinginezo, Yehova Mungu, “Mfalme wa umilele,” na Yesu Kristo, “mfalme wa . . . wafalme,” wanatimiza mambo yenye kustaajabisha kupitia wafanyakazi wenye ustadi. (1 Tim. 1:17; 6:15; soma Methali 22:29.) Tunataka kufanya kazi kwa bidii na kutumia ustadi wetu ili kumtukuza Yehova na si kujitukuza sisi wenyewe.​—Yoh. 8:54.

8. Unaweza kufanya nini unapojiwekea lengo la kujifunza ustadi fulani?

8 Chagua lengo hususa. Unaweza kukazia fikira ustadi gani? Waulize wazee wa kutaniko lenu au labda mwangalizi wenu wa mzunguko ustadi ambao wanafikiri unaweza kusitawisha. Kwa mfano, ikiwa wanapendekeza kwamba unahitaji kuboresha ustadi wako wa kusema na kufundisha, waombe wakusaidie kutambua sifa hususa ya usemi ambayo unahitaji kuifanyia kazi. Kisha, uchukue hatua hususa za kuboresha sifa hiyo. Unaweza kutimizaje hilo?

9. Unaweza kufanya nini ili kutimiza lengo lako la kujifunza ustadi fulani?

9 Jitahidi kufikia lengo lako. Tuseme unataka kuboresha uwezo wako wa kufundisha. Unaweza kujifunza kwa makini broshua Boresha Uwezo Wako wa Kusoma na Kufundisha. Unapopewa mgawo kwenye mkutano wa katikati ya juma, unaweza kumwomba ndugu anayestahili asikilize mgawo wako kabla ya kuutoa, na akupe mapendekezo ya kuuboresha. Mbali na kupata ustadi, jitahidi kuwa mwenye bidii na anayetegemeka.​—Met. 21:5; 2 Kor. 8:22.

10. Toa mfano wa jinsi ya kuboresha ustadi fulani.

10 Namna gani ikiwa ustadi unaotaka kusitawisha unahusisha jambo fulani ambalo kiasili si rahisi kwako kulifanya? Usife moyo! Ndugu anayeitwa Garry, alipambana na tatizo la kushindwa kusoma vizuri. Anakumbuka jinsi alivyoaibika, alipojaribu kusoma kwa sauti kwenye mikutano ya kutaniko. Lakini aliendelea kujitahidi. Sasa anasema kwamba kwa sababu ya mazoezi aliyopata, anaweza kutoa hotuba kwenye Jumba la Ufalme, kwenye makusanyiko ya mzunguko, na makusanyiko ya eneo!

11. Kama Timotheo ni nini kitakachotusaidia kutimiza majukumu zaidi?

11 Je, Timotheo alikuja kuwa msemaji maarufu au mwalimu mwenye ustadi? Biblia haisemi. Lakini bila shaka, Timotheo aliendelea kutimiza vizuri zaidi mgawo wake alipofuata ushauri wa Paulo. (2 Tim. 3:10) Vivyo hivyo, ikiwa tutasitawisha ustadi wetu, tutaweza kutimiza majukumu zaidi katika utumishi wetu kwa Yehova.

TAFUTA NJIA ZA KUWATUMIKIA WENGINE

12. Umenufaikaje kutokana na utumishi wa wengine?

12 Sisi sote tunanufaika kutokana na utumishi wa wengine. Tunapokuwa hospitalini, tunathamini kutembelewa na wazee wanaotumikia katika Halmashauri za Uhusiano na Hospitali au Vikundi vya Kutembelea Wagonjwa. Tunapopitia hali ngumu maishani, tunathamini mzee mwenye kujali anapotumia muda wake kutusikiliza na kutufariji. Tunapohitaji msaada wa jinsi ya kuongoza funzo la Biblia, tunafurahi painia mwenye uzoefu anapokubali kuandamana nasi kwenye funzo hilo na kutupatia mapendekezo. Ndugu na dada hao wote wanafurahi kutusaidia. Tunaweza kupata shangwe hiyo pia ikiwa tutakuwa tayari kuwatumikia ndugu zetu. Yesu alisema, “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Mdo. 20:35) Ikiwa unataka kupanua utumishi wako katika njia hizo au njia nyingine kama hizo, ni nini kitakachokusaidia kufikia malengo yako?

13. Tunapojiwekea lengo fulani la kibinafsi tunapaswa kukumbuka nini?

13 Epuka kujiwekea lengo ambalo si hususa. Kwa mfano, huenda ukafikiri hivi, ‘Ningependa kufanya mengi zaidi kutanikoni.’ Lakini huenda ikawa vigumu kujua jinsi ya kutimiza lengo hilo na huenda ukashindwa kutambua ikiwa umelitimiza. Hivyo, chagua lengo hususa na lililo wazi. Unaweza hata kuandika lengo hilo na jinsi unavyopanga kulitimiza.

14. Tunapojiwekea malengo, kwa nini tunapaswa kuwa tayari kufanya mabadiliko?

14 Pia, tunapojiwekea malengo tunahitaji kuwa tayari kufanya mabadiliko inapohitajika. Kwa nini? Kwa sababu hatuwezi kudhibiti kikamili hali zetu. Kwa mfano, mtume Paulo alikuwa amesaidia kuanzisha kutaniko jipya katika jiji la Thesalonike. Na bila shaka, alikuwa na lengo la kukaa huko na kuwasaidia Wakristo hao wapya. Lakini wapinzani walimlazimisha Paulo kuondoka katika jiji hilo. (Mdo. 17:1-5, 10) Ikiwa Paulo angeendelea kukaa huko angewahatarisha ndugu zake. Lakini Paulo hakufa moyo. Badala yake, alifanya mabadiliko kulingana na hali zilizotokea. Baadaye, alimtuma Timotheo ili awaimarishe kiroho waamini hao wapya huko Thesalonike. (1 The. 3:1-3) Ni lazima Wathesalonike hao walifurahi sana kwamba Timotheo alikuwa tayari kutumikia mahali popote alipohitajika!

15. Malengo yetu yanaweza kuathiriwaje na hali zinazopita uwezo wetu? Toa mfano.

15 Tunaweza kujifunza kutokana na kisa cha Paulo huko Thesalonike. Huenda tunatamani kufikia pendeleo fulani la utumishi, lakini hali zetu zinaweza kubadilika na hivyo kutuzuia kufikia pendeleo hilo la utumishi. (Mhu. 9:11) Ikiwa unapitia hali hiyo, uwe tayari kujiwekea lengo tofauti ambalo unaweza kulifikia. Hivyo ndivyo wenzi wa ndoa Ted na Hiedi walivyofanya. Kwa sababu ya tatizo la kiafya walihitaji kutoka Betheli. Lakini kwa sababu ya upendo wao kwa Yehova, walichochewa kutafuta njia nyingine ya kupanua utumishi wao. Kwanza, walianza utumishi wa upainia wa kawaida. Baada ya muda, waliwekwa rasmi kuwa mapainia wa pekee, na Ted alizoezwa kuwa mwangalizi wa mzunguko wa badala. Baadaye takwa la umri wa kuwa mwangalizi wa mzunguko lilibadilishwa. Ted na Heidi walitambua kwamba hawangeweza kustahili kwa ajili ya pendeleo hilo la utumishi. Ingawa walivunjika moyo, walitambua kwamba wangeweza kumtumikia Yehova katika njia nyingine. Ted anasema hivi: “Tumejifunza kutokazia fikira aina moja tu ya utumishi.”

16. Tunaweza kujifunza somo gani kutokana na Wagalatia 6:4?

16 Hatuwezi kudhibiti kila jambo linalotokea maishani mwetu. Kwa hiyo, ni muhimu tusipime thamani yetu kupitia mapendeleo yetu ya utumishi au kulinganisha mapendeleo yetu na ya wengine. Hiedi anaeleza hivi: “Utakosa amani ikiwa utalinganisha maisha yako na maisha ya wengine.” (Soma Wagalatia 6:4.) Ni muhimu kutafuta njia ambazo tunaweza kuwatumikia wengine na Yehova. *

17. Unaweza kufanya nini ili kustahili kupata mapendeleo ya utumishi?

17 Unaweza kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova, kwa kurahisisha maisha yako na kuepuka madeni yasiyo ya lazima. Jiwekee malengo ya muda mfupi yatakayokusaidia kufikia malengo ya muda mrefu. Kwa mfano, ikiwa una lengo la muda mrefu la kuwa painia wa kawaida, je, kwa sasa unaweza kutumikia ukiwa painia msaidizi kwa mfululizo? Ikiwa lengo lako ni kutumikia ukiwa mtumishi wa huduma, je, unaweza kutumia muda zaidi katika utumishi wa shambani na kuwatembelea wagonjwa na wenye umri mkubwa katika kutaniko lenu? Uzoefu unaopata sasa unaweza kufungua milango ya kupata mapendeleo zaidi ya utumishi wakati ujao. Azimia kufanya yote unayoweza katika mgawo wowote unaopewa.​—Rom. 12:11.

Chagua lengo hususa unaloweza kulifikia (Tazama fungu la 18) *

18. Kama inavyoonyeshwa kwenye picha, unajifunza nini kutokana na mfano wa dada Beverley?

18 Hata tuwe na umri gani tunaweza kujiwekea na kutimiza malengo ya kiroho. Fikiria mfano wa Beverley, dada mwenye umri wa miaka 75. Alikuwa na tatizo kubwa la afya hivi kwamba alishindwa kutembea vizuri. Lakini alitamani kushiriki kikamili katika kampeni ya Ukumbusho. Hivyo, akajiwekea malengo hususa. Beverley alipotimiza malengo yake kwa ajili ya kampeni hiyo alifurahi sana. Jitihada zake ziliwachochea wengine waongeze bidii katika huduma. Yehova anathamini jitihada za ndugu na dada zetu wenye umri mkubwa, hata ikiwa hali zao haziwaruhusu kufanya mengi.​—Zab. 71:17, 18.

19. Ni baadhi ya malengo gani ya kiroho tunayoweza kujiwekea?

19 Jiwekee malengo unayoweza kuyafikia. Sitawisha sifa zitakazomfurahisha Yehova. Jifunze ustadi utakaokufanya utumiwe zaidi na Mungu wetu na tengenezo lake. Tafuta njia za kuwatumikia ndugu na dada zako kikamili zaidi. * Kama Timotheo, kwa baraka za Yehova, ‘maendeleo yako yataonekana wazi kwa watu wote.’​—1 Tim. 4:15.

WIMBO 38 Atakupa Nguvu

^ Timotheo alikuwa mhudumu wa habari njema mwenye uzoefu mwingi. Hata hivyo, mtume Paulo alimtia moyo azidi kufanya maendeleo ya kiroho. Kwa kufuata shauri la Paulo, Timotheo angetumiwa zaidi na Yehova na angewasaidia zaidi ndugu na dada zake. Je, kama Timotheo, unatamani kumtumikia Yehova na waabudu wenzako kikamili zaidi? Bila shaka, ungependa kufanya hivyo. Ni malengo gani yatakayokusaidia kufanya hivyo? Na ni mambo gani yanayohusika katika kujiwekea na kutimiza malengo hayo?

^ UFAFANUZI WA MANENO: Malengo ya kiroho yanatia ndani jambo lolote tunalojitahidi kufanya ili tuweze kumtumikia Yehova kikamili zaidi na kumfurahisha.

^ Tazama sehemu “Kutumikia Maeneo Yenye Uhitaji Mkubwa” katika kitabu Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova, sura ya 10, fungu la 6-9.

^ Tazama somo la 60, “Endelea Kuimarisha Urafiki Wako na Yehova,” katika kitabu Furahia Maisha Milele!

^ MAELEZO YA PICHA: Ndugu akiwazoeza dada wawili kufanya kazi ya udumishaji, na dada hao wanatumia ustadi wao mpya vizuri.

^ MAELEZO YA PICHA: Dada ambaye hawezi kutoka nyumbani anafaulu kufanya utumishi kwa kutumia simu, anawaalika watu kwenye Ukumbusho.