Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAONI YA BIBLIA

Afya

Afya

Je, Mungu anajali jinsi tunavyoitendea miili yetu?

“Usiwe kati ya watu wanaokunywa divai mno, kati ya watu wanaokula nyama kwa ulafi.”—Methali 23:20.

KWA NINI SWALI HILO NI MUHIMU?

Biblia si kitabu cha kitiba; wala hakina maagizo ya jinsi mwanadamu anavyopaswa kujiendesha katika kila sehemu ya maisha yake. Hata hivyo, unaweza kufaidika kwa kujua maoni ya Mungu kuhusu afya kama yanavyoelezwa katika Biblia.

BIBLIA INASEMA NINI?

Mistari mingi ya Biblia inaonyesha maoni ya Mungu kuhusu jinsi tunavyoitendea miili yetu. Kwa mfano, Biblia inashutumu mazoea yenye kupita kiasi yanayodhuru, kama vile ulevi na ulafi. (Methali 23:20) Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli wa kale ilitia ndani hatua ambazo zingedhibiti au hata kuzuia magonjwa. Sheria hiyo pia ilitia ndani maagizo hususa ya usalama ili kuzuia majeraha. (Kumbukumbu la Torati 22:8) Ni wazi kwamba Biblia inatutia moyo tutunze miili yetu na kuchukua hatua zinazofaa ili kulinda afya yetu.

Kulingana na Biblia, kwa nini tunakuwa wagonjwa?

“Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi.”—Waroma 5:12.

 WATU HUSEMA NINI?

Watu wengi huamini kwamba magonjwa ni matokeo yasiyotazamiwa ya mageuzi ya wanadamu. Wengine wanadhani kwamba nguvu fulani zisizoonekana, kama vile roho waovu, ndizo husababisha matatizo yetu ya afya.

BIBLIA INASEMA NINI?

Kulingana na Biblia, sisi huwa wagonjwa kwa sababu wanadamu wa kwanza walimwasi Mungu. (Waroma 5:12) Kabla ya kuasi, wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, walikuwa na afya kamilifu. Walijua wangekufa ikiwa wangekataa utunzaji wenye upendo wa Mungu. (Mwanzo 2:16, 17) Lakini bado walivunja kimakusudi urafiki wao pamoja na Mungu na kupoteza hali yao ya ukamilifu. *

Tumerithi hali ya kutokamilika ya wazazi wetu wa kwanza walioasi. Hivyo, licha ya jitihada zetu za kuondoa magonjwa, bado sisi huwa wagonjwa.

UNAWEZA KUFANYA NINI?

Biblia inafundisha kwamba tukijipatanisha na Mungu kwa kutii kanuni zake zenye hekima, hatimaye tutafurahia afya kamilifu katika paradiso duniani. (Isaya 33:24) Mungu anaahidi kwamba ataondoa maumivu, magonjwa, na kifo.—Ufunuo 21:3, 4.

Je, Biblia inawakataza watu kutafuta matibabu hospitalini?

“Watu wenye afya hawahitaji tabibu, bali wenye kuugua ndio wanaomhitaji.”—Mathayo 9:12.

WATU HUSEMA NINI?

Watu fulani hupendekeza kuponywa kwa imani (au uponyaji wa kimuujiza) badala ya kutafuta matibabu hospitalini.

BIBLIA INASEMA NINI?

Mungu aliruhusu kuwe na matabibu kati ya watu wake nyakati za Biblia. (Mwanzo 38:28; Wakolosai 4:14) Hakuna andiko lolote katika Biblia linalosema kwamba Mungu alichukizwa na mbinu zao za matibabu kama vile kutumia mitishamba, dawa za kujipaka, kupendekeza vyakula fulani, na matibabu mengine. Kwa kweli, hata Yesu alisema kwamba “watu wenye afya hawahitaji tabibu, bali wenye kuugua ndio wanaomhitaji.”—Mathayo 9:12.

Hata hivyo, Biblia haipendekezi kwamba mtu atafute matibabu kwa njia yoyote ile. Kwa mfano, Biblia haiungi mkono zoea la kisasa la uponyaji wa kimuujiza. Na matibabu yanayohusisha kuwasiliana na roho hayakubaliwi na Mungu. (Wagalatia 5:19-21) Mbali na kuepuka mazoea ambayo Biblia inakataza, mtu anapokuwa mgonjwa, ni jambo la hekima kutafuta matibabu haraka iwezekanavyo, ikiwa yanapatikana.

^ fu. 10 Katika makala hii, tunatumia neno “kamilifu” na “ukamilifu” kurejelea hali ya afya ya wanadamu wa kwanza wakati Mungu alipowaumba, yaani, hawangeweza kuwa wagonjwa, na kufa.