Hamia kwenye habari

Je, Mkristo Anaweza Kukubali Matibabu?

Je, Mkristo Anaweza Kukubali Matibabu?

Jibu la Biblia

 Ndiyo. Yesu alionyesha kwamba wafuasi wake wanaweza kutafuta matibabu aliposema kuwa “watu wenye afya hawahitaji tabibu, bali wenye kuugua ndio wanaomhitaji.” (Mathayo 9:12) Ingawa Biblia si kitabu cha kimatibabu, ina kanuni za kuwaongoza wale wanaotaka kumpendeza Mungu.

Maswali unayopaswa kujiuliza

 1. Je, ninaelewa matibabu ninayopendekezewa? Biblia inatushauri tutafute habari zinazotegemeka badala ya ‘kuamini kila neno.’—Methali14:15.

 2. Je, nitafute ushauri wa madaktari wengine? Kutafuta ‘washauri wengi’ kunaweza kuwa jambo la maana, hasa ikiwa tatizo lako ni kubwa.—Methali 15:22.

 3. Je, matibabu hayo yanavunja amri ya Biblia ya ‘kujiepusha na damu?’—Matendo 15:20.

 4. Je, matibabu au mbinu za uchunguzi wa kimatibabu zinatia ndani mazoea ya kuwasiliana na pepo? Biblia inashutumu “mazoea ya kuwasiliana na pepo.” (Wagalatia 5:19-21) Ili ujue ikiwa matibabu fulani yanatia ndani mazoea ya kuwasiliana na pepo, fikiria maswali kama haya:

  •   Je, daktari anawasiliana na pepo?

  •   Je, matibabu yanategemea imani ya kwamba ugonjwa unasababishwa na miungu iliyokasirika au maadui wanaotumia uchawi?

  •   Je, dhabihu, nyimbo za kichawi, au desturi nyingine za kuwasiliana na pepo hutumiwa wakati wa kutengeneza au kutumia dawa?

 5. Je, ninahangaikia afya yangu kupita kiasi? Biblia inashauri hivi: “Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.” (Wafilipi 4:5) Kuwa na usawaziko kutakusaidia ukazie fikira “mambo yaliyo ya maana zaidi,” kama vile mambo ya kiroho.—Wafilipi 1:10; Mathayo 5:3.