Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAHOJIANO | CÉLINE GRANOLLERAS

Mtaalamu wa Figo Anaeleza kwa Nini Anamwamini Mungu

Mtaalamu wa Figo Anaeleza kwa Nini Anamwamini Mungu

Dakt. Céline Granolleras, ni daktari nchini Ufaransa anayeshughulikia hasa magonjwa ya figo. Zaidi ya miaka 20 baada ya kuwa daktari, alianza kuamini kwamba kuna Muumba anayetujali. Mwandishi wa Amkeni! alimhoji kuhusu kazi yake na imani yake.

Tueleze kuhusu malezi yako.

Nilipokuwa na umri wa miaka tisa, familia yetu ilihamia Ufaransa kutoka Hispania. Wazazi wangu walikuwa Wakatoliki, lakini niliacha kumwamini Mungu nilipokuwa na umri wa miaka 16. Kwa maoni yangu, dini haikuwa muhimu maishani. Mtu aliponiuliza uhai ulitokeaje ikiwa hakuna Mungu, nilimjibu, “Kwa sasa, wanasayansi hawawezi kujibu, lakini siku moja watafaulu.”

Ni nini kilichokufanya uamue kujifunza kuhusu magonjwa ya figo?

Nilisomea katika chuo kimoja cha kitiba katika jiji la Montpellier, Ufaransa. Profesa mmoja katika shule hiyo alinitia moyo nijifunze kuhusu magonjwa ya figo. Masomo hayo yalihusisha kufanya utafiti na wakati uleule kuwatibu wagonjwa. Na hilo ndilo nililotaka kufanya. Katika mwaka wa 1990, nilianza kushiriki katika utafiti wa jinsi ya kutumia homoni inayoitwa erythropoietin (EPO) kudhibiti kutokezwa kwa chembe nyekundu za damu katika mifupa yetu. Wakati huo, taaluma hiyo ya utafiti ilionekana kuwa mpya sana.

Ni nini kilichokufanya uanze kufikiri kuhusu Mungu?

Katika mwaka wa 1979, mume wangu, Floréal, alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Lakini mimi sikupendezwa. Tangu utotoni nilikuwa nimechoshwa na dini. Hata hivyo, mume wangu na watoto wangu wakawa Mashahidi, na punde si punde marafiki wetu wengi walikuwa Mashahidi. Mmoja wao, anayeitwa Patricia, akaniambia nijaribu  kusali. Aliniambia hivi: “Ikiwa hakuna mtu yeyote mbinguni, hutapoteza chochote. Lakini ikiwa kuna mtu, utaona kitakachotokea.” Miaka mingi baadaye, nilianza kujiuliza kuhusu kusudi la uhai, na nikakumbuka maneno ya Patricia. Nikaanza kusali ili nipate kuelewa.

Ni nini kilichokufanya uanze kujiuliza kuhusu kusudi la uhai?

Lile shambulio la kigaidi kwenye majengo ya World Trade Center huko New York lilinifanya nijiulize kwa nini kuna uovu mwingi sana. Nilijiambia: ‘Dini zenye imani kali zinahatarisha wakati wetu ujao. Lakini hapa kwangu nimezungukwa na Mashahidi wa Yehova ambao ni watu wenye amani. Hawana imani kali. Wanaitii Biblia. Labda ninapaswa kuchunguza kile ambacho Biblia inasema.’ Kwa hiyo, nikaanza kuisoma Biblia.

Kwa kuwa wewe ni daktari, je, ilikuwa vigumu kuamini kuna Muumba?

Hapana. Nilipendezwa sana na jinsi mwili wetu ulivyobuniwa kwa njia ya ajabu. Kwa mfano, nilistaajabishwa sana na jinsi figo zetu zinavyodhibiti kiwango cha chembe nyekundu katika damu yetu.

Unamaanisha nini?

Nilitambua kwamba ni Mungu tu ambaye angeweza kubuni mfumo wa hali ya juu kama huo

Kama unavyojua, chembe nyekundu za damu husafirisha oksijeni. Ukipoteza damu nyingi au ukienda maeneo yenye milima, mwili wako utakosa oksijeni. Figo zetu zina vipima oksijeni. Zinapotambua kwamba kuna upungufu wa oksijeni katika damu, zinachochea kutokezwa kwa homoni ya EPO, na kiwango cha EPO ndani ya damu kinaweza kupanda zaidi ya mara elfu moja. EPO huchochea uloto wa mfupa kutokeza chembe nyekundu kwa wingi, nazo chembe hizo husafirisha oksijeni zaidi. Inastaajabisha sana! Kwa kushangaza, nilijifunza utendaji huo kwa miaka kumi kabla ya kutambua kwamba ni Mungu tu ambaye angeweza kubuni mfumo wa hali ya juu kama huo.

Ulikuwa na maoni gani uliposoma Biblia?

Nilikuwa nimesoma vitabu vingi sana vya kihistoria na vitabu maarufu vya hadithi, lakini mara moja nilitambua kwamba Biblia ilikuwa tofauti. Mashauri yake yanafaa kabisa hivi kwamba lazima yawe yametoka kwenye chanzo cha juu zaidi kuliko mwanadamu. Utu wa Yesu ulinivutia sana. Niliona kwamba alikuwa mtu halisi. Alikuwa na hisia, na alikuwa na marafiki. Kwa kuwa sikutaka kusoma vitabu vya Mashahidi wa Yehova, nilipokuwa na swali nilifanya utafiti kwenye ensaiklopidia na vitabu vingine.

Ulifanya utafiti gani?

Nilifanya utafiti kwa kutumia vitabu vya kihistoria . . . Mwishowe, nilifikia mkataa kwamba unabii huo wa Biblia ulitimia kwa wakati

Nilipendezwa na jinsi Biblia ilivyotabiri mwaka ambao Yesu alibatizwa. Ilionyesha muda hususa ambao ungepita kati ya mwaka wa 20 wa utawala wa Artashasta, mtawala wa Uajemi na mwaka ambao Yesu angetokea akiwa Masihi. * Nimezoea kufanya utafiti—hiyo ni sehemu ya kazi yangu. Kwa hiyo, nilifanya utafiti kwa kutumia vitabu vya kihistoria ili kuthibitisha kipindi cha utawala wa Artashasta na kipindi cha huduma ya Yesu. Mwishowe, nilifikia mkataa kwamba unabii huo wa Biblia ulitimia kwa wakati na lazima uwe uliongozwa na roho ya Mungu.

^ fu. 19 Ona kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, ukurasa wa 197-199.