Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU

Chembe Zako—Maktaba Iliyo Hai!

Chembe Zako—Maktaba Iliyo Hai!

KATIKA mwaka wa 1953, wanabiolojia wa molekuli James Watson na Francis Crick walichapisha ugunduzi wao ulio muhimu sana katika uelewaji wetu wa kisayansi kuhusu uhai. Waligundua umbo la DNA linalofanana na kamba yenye matita mawili. * Mara nyingi kamba hizo zinazopatikana ndani ya kiini cha kila chembe huwa na programu, “maandishi” au habari zinazofanya chembe hizo kuwa kama maktaba zilizo hai. Ugunduzi huo wenye kustaajabisha ulikuwa wa muhimu sana katika elimu ya biolojia! “Maandishi” yaliyo kwenye chembe yana umuhimu gani? Yalitokeaje?

KWA NINI CHEMBE ZINAHITAJI HABARI?

Je, umewahi kujiuliza ni kwa nini mbegu inapopandwa hatimaye huwa mti au ni jinsi gani yai lililotungishwa mimba hatimaye huwa mwanadamu? Je, umewahi kufikiria jinsi ulivyorithi tabia? Majibu ya maswali hayo yanategemea habari zinazopatikana kwenye DNA.

Karibu chembe zote zina DNA ambayo ni molekuli tata zaidi inayofanana na ngazi iliyopindika. Katika genome ya mwanadamu au safu kamili ya DNA, ngazi hizo zinakadiriwa kuwa na “vipande” bilioni tatu vya kemikali. Wanasayansi huviita vipande hivyo jozi za msingi kwa sababu kila kipande kimeundwa kwa kemikali za aina mbili ambazo kwa pamoja ziko nne. Chembe hizo huandikwa kwa kifupi kwa kutumia herufi nne rahisi ambazo ni A, C, G, na T. * Katika mwaka wa 1957, Crick alieleza pia kwamba kuna mistari yenye mpangilio katika vipande vya kemikali ambayo hutokeza maagizo yaliyoandikwa. Jambo hilo lilianza kueleweka vizuri katika miaka ya 1960.

Habari yoyote iwe ni picha, sauti, au maandishi, inaweza kuhifadhiwa na kushughulikiwa kwa njia nyingi. Kwa mfano, kompyuta hufanya hivyo kielektroniki. Kwa kutumia DNA, chembe hai huhifadhi na kushughulikia habari kwa njia ya kikemikali. DNA hupitishwa wakati chembe zinapogawanyika na viumbe vinapozaliana—uwezo unaoaminika kwamba ndiyo unaofafanua maana ya uhai.

Chembe hutumia habari jinsi gani? Hebu wazia kwamba DNA ni kama kitabu cha mapishi chenye maelekezo na hatua mbalimbali, na kila hatua imeandikwa kwa umakini na utaratibu maalumu. Hata hivyo, badala ya maelekezo hayo kutokeza keki au biskuti yanatokeza kabichi au ng’ombe. Hata hivyo, hatua hizo hujiendesha zenyewe katika chembe hai na hivyo hufanya iwe vigumu kuzielewa.

Habari zilizo katika chembe ya bakteria zinaweza kujaza kurasa 1,000 za kitabu

Habari zilizo kwenye chembe ya urithi huhifadhiwa mpaka zitakapohitajiwa, labda ili kubadili chembe zilizochakaa au zilizo na ugonjwa kwa kutokeza chembe mpya au kupitisha tabia kwa mtoto. DNA ina habari nyingi kadiri gani? Fikiria bakteria, mmoja kati ya viumbe wadogo zaidi. Mwanasayansi Mjerumani Bernd-Olaf Küppers alisema hivi: “Tukilinganisha na lugha, ujumbe ulio katika molekuli unaofafanua muundo wa chembe ya bakteria unaweza kutoshea kitabu chenye kurasa elfu kadhaa.” Kwa sababu hiyo, profesa wa kemia David Deamer aliandika hivi: “Mtu anaweza kupendezwa na mambo tata kuhusu uhai hata ule unaonekana kuwa wa hali ya chini.” Genome ya mwanadamu inaweza kulinganishwa na nini? Küppers anasema hivi: “Habari zilizo katika [Genome] zinaweza kujaza maelfu ya vitabu katika maktaba.”

“ZIMEANDIKWA KWA NJIA AMBAYO TUNAWEZA KUELEWA”

Kufafanua habari zilizo katika DNA kama “lugha ya molekuli ya chembe za urithi hakutoshi,” anasema Küppers. Anaendelea kusema hivi: “Kama tu ilivyo katika lugha za wanadamu, lugha ya molekuli ya chembe za urithi ina utaratibu maalumu.” Kwa ufupi, DNA ina “sarufi,” au kanuni, zinazoongoza kikamili jinsi maagizo yanavyotolewa na kutekelezwa.

“Maneno” na “sentensi” katika DNA huunda “maagizo” mbalimbali ambayo huongoza kutokezwa kwa protini na viini vingine vinavyojenga chembe mbalimbali zinazounda mwili. Kwa mfano, “maagizo” hayo yanaweza kuongoza kufanyizwa kwa chembe za mifupa, misuli, neva, au chembe za ngozi. Mwanabiolojia wa mageuzi, Matt Ridley aliandika hivi: “Uzi wa DNA una habari au ujumbe ulioandikwa kikemikali, na kila herufi moja inawakilisha kemikali moja.” Akaongezea hivi: “Ni jambo la kushangaza kwamba alama hizo au utaratibu huo hubadilika na kuwa maandishi tunayoweza kuelewa.”

Mwandikaji wa Biblia Daudi alisali kwa Mungu hivi: “Macho yako yalikiona kiini-tete changu, na katika kitabu chako sehemu zake zote zilikuwa zimeandikwa.” (Zaburi 139:16) Daudi alitumia lugha ya kishairi. Hata hivyo, kulingana na kanuni, alikuwa sahihi kabisa akiwa mwandishi wa Biblia. Hakuna mwandishi yeyote wa Biblia aliyeathiriwa hata kidogo na hekaya au mapokeo ya watu wa kale.—2 Samweli 23:1, 2; 2 Timotheo 3:16.

Mtoto hurithi tabia za wazazi wake jinsi gani?

MAANDISHI HAYO HUANDIKWAJE?

Kama ilivyo katika visa vingi, wanasayansi wanapofafanua jambo moja maswali mengi hujitokeza yanayohitaji ufafanuzi mwingine. Hivyo ndivyo ilivyokuwa walipogundua DNA. Ilipojulikana kwamba DNA ina habari zilizoandikwa, watafiti waliuliza hivi: ‘Maandishi hayo huandikwaje?’ Bila shaka, hakuna mwanadamu aliyeona molekuli ya kwanza ya DNA ilipoumbwa. Hivyo, tunaweza kuwa na maoni mbalimbali. Hata hivyo, maoni hayo hayapaswi kukisiwa-kisiwa. Fikiria ulinganifu ufuatao.

  • Katika mwaka 1999, vipande vya vigae vya kale vilivyo na alama au michoro isiyo ya kawaida vilichimbuliwa nchini Pakistan. Alama hizo bado hazijaweza kufafanuliwa. Hata hivyo, inadhaniwa kwamba alama hizo ziliandikwa na binadamu.

  • Miaka michache baada ya Watson na Crick kugundua muundo wa DNA, wanafizikia wawili walianza kuchunguza mawimbi ya redio kutoka angani. Huo ukawa mwanzo wa uchunguzi unaoendelea wa ikiwa kuna viumbe hai katika sayari nyingine.

Jambo kuu ni nini? Watu huhusianisha habari na ujuzi iwe habari hiyo iko kwenye michoro ya kigae au ishara kutoka angani. Hawahitaji kuona jinsi habari hiyo ilivyojitokeza ili kufikia mkataa huo. Hata hivyo, wakati mfumo tata wenye habari ulipogunduliwa, yaani, kemikali yenye habari kuhusu uhai, wengi huona utendaji wa DNA kuwa jambo lisilo na maana yoyote. Je, ni jambo linalofaa kuwa na maoni hayo? Je, linapatana na akili? Je, hilo ni jambo la wanasayansi pekee? Wanasayansi wengi mashuhuri husema haipaswi kuwa hivyo. Baadhi ya wanasayansi hao ni Dakt. Gene Hwang na Profesa Yan-Der Hsuuw. * Fikiria yale waliyosema.

Dakt. Gene Hwang amefanya utafiti wa msingi wa mpangilio wa chembe za urithi. Wakati fulani aliamini mageuzi, lakini utafiti aliofanya ulibadili maoni yake. Aliliambia gazeti la Amkeni! hivi: “Kujifunza kuhusu chembe za urithi kunaongeza ujuzi kuhusu mfumo wa uhai, ujuzi unaonifanya niheshimu sana hekima ya Muumba.”

Profesa Yan-Der Hsuuw ni kiongozi wa utafiti wa viini-tete katika Chuo kikuu cha Taiwan cha National Pingtung University of Science and Technology. Yeye pia aliamini mageuzi mpaka baada ya kufanya utafiti uliomwongoza kufikia mkataa tofauti. Alisema hivi kuhusu mgawanyiko wa chembe na utendaji wake wa pekee: “Chembe zinazofaa lazima zitokezwe kwa utaratibu na sehemu zinazofaa. Kwanza chembe hizo huungana na kuwa tishu ambazo pia huungana na kuwa viungo. Ni injinia gani anayeweza kuandika maagizo yanayojiendesha yenyewe? Hata hivyo, maagizo ya ukuzi wa viini-tete yameandikwa kwa njia ya pekee katika DNA. Ninapofikiria utaratibu huo mzuri ninaamini kwamba uhai ulibuniwa na Mungu.”

Gene Hwang (kushoto) na Yan-Der Hsuuw

JE, JAMBO HILO NI MUHIMU?

Bila shaka! Ikiwa Mungu ndiye aliyeumba uhai, basi Mungu ndiye anayestahili kusifiwa wala si mageuzi. (Ufunuo 4:11) Pia, ikiwa sisi tumeumbwa na Muumba mwenye hekima, basi tupo hapa kwa kusudi fulani. Hali isingekuwa hivyo ikiwa uhai ulijitokeza wenyewe. *

Kwa kweli, watu wanaotafakari hutafuta majibu yenye kuridhisha. “Ni jambo la msingi kwa wanadamu kutafuta kusudi la uhai,” akasema Viktor Frankl, aliyekuwa profesa wa mfumo wa neva na magonjwa ya akili. Kwa upande mwingine, tuna njaa ya kiroho ambayo tunatamani kuitosheleza, yaani, njaa inayowapata wanadamu kwa sababu wao ni viumbe wa pekee. Hata hivyo, ikiwa tumeumbwa na Mungu, je, ametupatia njia ya kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho?

Yesu Kristo alijibu swali hilo aliposema kwamba: “Mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova [au Mungu].” (Mathayo 4:4) Maneno ya Yehova yaliyoandikwa kwenye Biblia, yametosheleza njaa ya kiroho ya mamilioni ya watu, na yamewapa kusudi la uhai na tumaini zuri la wakati ujao. (1 Wathesalonike 2:13) Biblia inaweza kukusaidia. Kwa kweli, itafaa pia ukisoma kitabu hicho cha pekee.

^ fu. 3 Watson na Crick walifanya utafiti wao wakitegemea uchunguzi uliofanywa awali kuhusu DNA, au deoksiribonyukilia asidi.—Ona sanduku “ Historia ya Ugunduzi wa DNA.”

^ fu. 6 Herufi hizo humaanisha kemikali ya adenine, cytosine, guanine, na thymine.

^ fu. 18 Mahojiano zaidi pamoja na wanasayansi mashuhuri yanaweza kupatikana kwenye tovuti yetu, jw.org/sw. Bonyeza kitufe cha Tafuta, kisha ingiza “mahojiano na wanasayansi.”

^ fu. 22 Maswali kuhusu uumbaji na mageuzi yamezungumziwa kwa kina katika broshua Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai na Uhai—Ulitokana na Muumba? zinazopatikana kwenye www.mt711.com/sw.