Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumtumikia Mungu Ndiyo Dawa Yake!

Kumtumikia Mungu Ndiyo Dawa Yake!

Mapainia wawili walipoalikwa katika nyumba fulani nchini Kenya, walishangaa kumwona mwanamume mdogo aliyelala kitandani. Alikuwa na mwili mdogo sana na mikono mifupi. Walipokuwa wakizungumza naye kuhusu ahadi ya Mungu kwamba “kilema atapanda juu kama vile paa anavyofanya,” mwanamume huyo alifurahi sana.Isa. 35:6.

Baadaye mapainia hao walijua kwamba Onesmus, ambaye sasa ana umri wa karibu miaka 40, alizaliwa akiwa na ugonjwa wa mifupa (osteogenesis imperfecta). Mifupa yake ni dhaifu sana hivi kwamba inaweza kuvunjika kwa urahisi sana. Kwa kuwa ugonjwa huo hauna dawa, Onesmus alijua kwamba sikuzote angeishi na maumivu na kutumia kiti cha magurudumu.

Onesmus alikubali kujifunza Biblia. Hata hivyo, mama yake alimkataza kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa sababu alisema kwamba Onesmus angepata maumivu zaidi. Kwa hiyo, ndugu walirekodi mikutano ili Onesmus asikilize akiwa nyumbani. Baada ya kujifunza kwa miezi mitano, Onesmus aliamua kuanza kuhudhuria mikutano licha ya hali yake.

Je, Onesmus alihisi maumivu zaidi baada ya kuhudhuria mikutano? Hapana. Onesmus anasema hivi: “Ni kana kwamba maumivu niliyokuwa nayo yalipungua wakati wa mikutano.” Alijihisi amepata nafuu kwa sababu ya tumaini alilopata. Mama ya Onesmus aliona jinsi mtazamo wa mwana wake ulivyobadilika na alifurahi sana hivi kwamba akakubali pia kujifunza Biblia. Alisema hivi: “Kumtumikia Mungu ndiyo dawa ya mwanangu.”

Baada ya muda mfupi, Onesmus akawa mhubiri ambaye hajabatizwa. Baadaye, alibatizwa na sasa anatumika akiwa mtumishi wa huduma. Ingawa hawezi kutumia miguu na mkono wake mmoja, Onesmus alitamani kufanya yote awezayo katika utumishi wa Yehova. Alitaka kuwa painia msaidizi lakini alisita kujaza ombi. Kwa nini? Kwa sababu alijua kwamba angehitaji mtu wa kusukuma kiti chake cha magurudumu. Alipowaeleza Wakristo wenzake hangaiko lake, waliahidi kumsaidia. Na walimsaidia Onesmus alipokuwa painia msaidizi.

Onesmus alitamani kuwa painia wa kawaida ingawa alikuwa pia na wasiwasi. Hata hivyo, pindi moja, andiko la siku lilimpa kitia-moyo alichohitaji. Lilikuwa andiko la Zaburi 34:8 linalosema: “Onjeni mwone ya kuwa Yehova ni mwema.” Baada ya kutafakari andiko hilo, Onesmus aliamua kuwa painia wa kawaida. Sasa anahubiri kwa siku nne kila juma na anajifunza Biblia na watu kadhaa wanaofanya maendeleo ya kiroho. Mwaka wa 2010, alihudhuria Shule ya Utumishi wa Painia. Onesmus alifurahi sana alipofundishwa katika shule hiyo na mmoja wa ndugu waliomhubiria kwa mara ya kwanza!

Wazazi wa Onesmus walikufa, na sasa ndugu na dada katika kutaniko lao humtunza kila siku. Anathamini sana baraka anazofurahia sasa, na anatazamia kwa hamu wakati ambapo “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”Isa. 33:24.