Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumkaribia Mungu Ni Kwema Kwangu

Kumkaribia Mungu Ni Kwema Kwangu

NILIPOFIKIA umri wa miaka tisa, sikuendelea kukua. Hilo lilitukia miaka 34 iliyopita nchini Côte d’Ivoire, na mpaka leo nina urefu wa mita moja tu. Wazazi wangu walipogundua hali yangu, walinitia moyo nifanye kazi kwa bidii ili nikazie fikira kazi badala ya kufikiria mwonekano wangu. Niliweka meza ya kuuzia matunda mbele ya nyumba yetu na nilidumisha usafi. Hilo liliwavutia wateja wengi.

Hata hivyo, kufanya kazi kwa bidii hakukubadili kila kitu. Bado nilikuwa mfupi sana, na ilikuwa vigumu kufanya mambo ya kawaida maishani, kama vile kufikia urefu wa meza za dukani. Kila kitu kilionekana kuwa kimetengenezwa kwa ajili ya watu warefu. Nilijihurumia sana, lakini mambo yalibadilika nilipokuwa na umri wa miaka 14.

Siku moja, wanawake wawili Mashahidi wa Yehova walinunua matunda, na kisha wakaanza kunifundisha Biblia. Mara moja nikaelewa kwamba kumjua Yehova na kusudi lake ni muhimu zaidi kuliko hali yangu ya kimwili. Hilo lilinisaidia sana. Ninalipenda sana andiko la Zaburi 73:28. Sehemu ya kwanza ya andiko hilo inasema hivi: “Kumkaribia Mungu ni kwema kwangu.”

Punde si punde, familia yetu ilihamia Burkina Faso, na maisha yangu yalibadilika kabisa. Nchini Côte d’Ivoire, watu walizoea kuniona kando ya meza ya matunda. Lakini katika makao yetu mapya, nilikuwa mgeni machoni pa wengi. Watu walinishangaa. Hilo lilinifanya nisitoke nje ya nyumba kwa majuma kadhaa. Kisha, nikakumbuka jinsi ilivyokuwa vyema kwangu kumkaribia Yehova. Niliiandikia barua ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova, na nikatembelewa na mmishonari anayeitwa Nani, aliyekuwa na pikipiki.

Barabara zetu zilikuwa zinateleza, na zilikuwa na matope wakati wa mvua. Dada Nani alianguka na pikipiki mara nyingi alipokuja kunifundisha Biblia, hata hivyo hakuchoka. Kisha, akajitolea kunipeleka mikutanoni. Nilijua kwamba ili kufanya hivyo nilihitaji kutoka nje ya nyumba na kuvumilia kukodolewa macho na watu. Zaidi ya hilo, kupanda pikipiki kungeongeza uzito na hilo lingefanya iwe vigumu hata zaidi kuiendesha. Licha ya hayo, nilikubali kwa sababu nilikumbuka sehemu ya pili ya andiko ninalolipenda inayosema hivi: “Nimeweka kimbilio langu katika Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”

Nyakati fulani mimi na Dada Nani tulianguka kwenye matope, lakini ilikuwa muhimu sana kuhudhuria mikutano. Watu niliokutana nao Jumba la Ufalme walikuwa na tabasamu changamfu tofauti na watu wengine. Miezi tisa baadaye nikabatizwa.

Sehemu ya tatu ya andiko ninalolipenda inasema hivi: “Kutangaza kazi zako zote.” Nilijua kwamba kuhubiri kungekuwa changamoto kubwa sana kwangu. Bado ninakumbuka mara ya kwanza nilipohubiri nyumba kwa nyumba. Watoto na watu wazima walinikodolea macho, walinifuata na kuigiza jinsi ninavyotembea. Jambo hilo liliniumiza sana, lakini nilikumbuka kwamba wao pia wanahitaji Paradiso kama mimi; hivyo nikaendelea kuvumilia.

Nilinunua baiskeli inayoendeshwa kwa mikono, na ilinisaidia sana. Nikiwa utumishi, mwandamani wangu angenisukuma mahali penye mwinuko na kisha angepanda kwenye baiskeli tulipokuwa mteremkoni. Ingawa mwanzoni haikuwa rahisi kushiriki katika huduma, kufanya hivyo kulinipa shangwe kubwa sana hivi kwamba mwaka wa 1998 nikawa painia wa kawaida.

Niliwafundisha watu wengi Biblia, na wanne kati yao wamebatizwa. Nilifurahi sana mdogo wangu pia alipokubali kweli! Ninafurahia sana kusikia wengine wakifanya maendeleo na hilo linaniimarisha. Siku moja nilipokuwa ninaugua malaria, nilipokea barua kutoka Côte d’Ivoire. Nilianza kumfundisha Biblia mwanafunzi mmoja wa chuo nchini Burkina Faso na kisha nikamkabidhi ndugu fulani aendelee kumfundisha. Baadaye, mwanafunzi huyo alihamia Côte d’Ivoire. Nilifurahi sana kujua kwamba amekuwa mhubiri ambaye hajabatizwa!

Ninafanya nini ili kupata riziki? Shirika moja linalosaidia watu wenye mahitaji maalum lilijitolea kunifundisha kushona. Mwalimu mmoja alipoona utendaji wangu wa kazi alisema hivi: “Tunapaswa kukufundisha kutengeneza sabuni.” Nao walinifundisha. Nikiwa nyumbani, ninatengeneza sabuni za kufulia na za kuogea. Watu wanazipenda sabuni zangu nao huzitangaza kwa wengine. Ninasambaza sabuni hizo kwa kutumia pikipiki yenye magurudumu matatu.

Kwa kusikitisha, mwaka 2004 maumivu ya uti wa mgongo yaliongezeka sana hivi kwamba nililazimika kuacha upainia. Hata hivyo, bado ninashiriki kwa ukawaida katika huduma.

Watu husema kwamba mimi ni mtu mwenye tabasamu. Nina kila sababu ya kufurahi kwa sababu kumkaribia Mungu ni kwema kwangu.—Limesimuliwa na Sarah Maiga.