Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siri ya Furaha ya Familia

Wajibika Sikuzote Katika Ndoa Yako

Wajibika Sikuzote Katika Ndoa Yako

Mke anasema: “Nilitambua kwamba kwa muda fulani mume wangu Michael alikuwa amepunguza upendo wake kwangu na kwa watoto wetu. * Tabia zake zilibadilika mara tu tulipoanza kutumia Intaneti, na nilishuku kwamba alikuwa akitazama ponografia (picha au habari za ngono) kwenye kompyuta. Usiku mmoja baada ya watoto kulala, nilimwuliza na kumshurutisha aniambie naye akakiri kwamba alikuwa akitazama tovuti za ponografia. Nilihuzunishwa sana. Sikuamini kwamba hilo lilikuwa likinipata. Niliacha kumwamini kabisa. Isitoshe, mfanyakazi mwenzangu alikuwa ameanza kupendezwa nami kimahaba.”

Mume anasema: “Wakati fulani uliopita mke wangu, Maria, alipata picha kwenye kompyuta yetu na kunikabili kuhusu jambo hilo. Nilipokiri kwamba nilikuwa nikitazama tovuti za ponografia alikasirika sana. Niliaibika sana na nikajihisi kuwa mwenye hatia. Nilifikiri ndoa yetu ingevunjika.”

UNAFIKIRI uhusiano wa Michael na Maria uliendelea namna gani? Huenda ukafikiri kwamba tatizo kuu la Michael lilikuwa kutazama ponografia. Lakini kama Michael alivyotambua baadaye, kutazama ponografia kulikuwa dalili ya tatizo kubwa zaidi, yaani, kutowajibika katika ndoa yao. * Michael na Maria walipooana walitazamia kuishi maisha yenye upendo na yenye kufurahisha. Lakini kama wenzi wengi, baada ya muda uwajibikaji wao kuelekea ndoa ulipungua, na uhusiano wao ukazorota.

Je, unahisi kwamba uhusiano kati yako na mwenzi wako umezorota kadiri ambavyo miaka imepita? Je, ungependa kubadili hali hiyo? Ikiwa ndivyo, unahitaji kujua majibu ya maswali matatu: Kuwajibika katika ndoa kunamaanisha nini? Ni mambo gani yanayoweza kudhoofisha uhusiano wenu? Na unaweza kufanya nini ili kuimarisha uwajibikaji wako kwa mwenzi wako?

Kuwajibika Kunamaanisha Nini?

Unaweza kusema kuwajibika katika ndoa ni nini? Wengi wanaweza kusema kunatokana na kutambua kwamba mtu ana majukumu ya kutimiza. Kwa mfano, huenda wenzi wa ndoa wakawajibika katika ndoa yao kwa sababu ya watoto wao au kwa sababu ya majukumu kuelekea Mungu ambaye ndiye Mwanzilishi wa ndoa. (Mwanzo 2:22-24) Kwa wazi, mambo hayo yanapendeza na yatasaidia ndoa kukabiliana na hali ngumu. Lakini ili wawe na furaha, wenzi wa ndoa wanahitaji kufanya mengi zaidi ya kutimiza majukumu yao.

Yehova Mungu alianzisha ndoa ili iwaletee wenzi shangwe na uradhi wenye kina. Alikusudia mwanamume ‘ashangilie pamoja na mke wake’ na mwanamke ampende mume wake na kuhisi kwamba mume wake anampenda kama mwili wake mwenyewe. (Methali 5:18; Waefeso 5:28) Ili wawe na uhusiano wa aina hiyo, wenzi wa ndoa lazima wajifunze kuaminiana. Jambo lingine muhimu ni kusitawisha urafiki wa kudumu. Mwanamume na mwanamke wanapoaminiana na kujitahidi kuwa marafiki wa karibu, watawajibika zaidi katika ndoa yao. Watakuwa na kifungo ambacho Biblia inafafanua kuwa cha karibu sana kana kwamba watu hao wawili ni “mwili mmoja.”—Mathayo 19:5.

Hivyo, uwajibikaji unaweza kufananishwa na saruji inayounganisha matofali ya nyumba iliyo imara. Saruji inatengenezwa kutokana na mchanganyiko fulani unaotia ndani mchanga, sementi, na maji. Vivyo hivyo, uwajibikaji unatokezwa na mchanganyiko wa mambo mbalimbali kama vile, majukumu, kuaminiana, na urafiki. Ni nini kinachoweza kudhoofisha kifungo hicho?

Kuna Vizuizi Gani?

Kuwajibika kunahitaji jitihada na kujidhabihu. Ni lazima uwe tayari kuacha mapendezi yako mwenyewe ili umpendeze mwenzi wako. Hata hivyo, mtazamo wa kukubali mapendezi ya wengine, yaani, kutoa bila kujiuliza, ‘Nitafaidika jinsi gani?’ haupendwi na wengi na hata unawachukiza wengine. Lakini jiulize hivi, ‘Ninajua watu wangapi wenye ubinafsi walio na ndoa zenye furaha?’ Ikiwa kuna wowote, huenda wakawa wachache sana. Kwa nini? Inaelekea kwamba mtu mwenye ubinafsi hatawajibika katika ndoa ikiwa anahitaji kujidhabihu, hasa ikiwa haoni jinsi jitihada zake zitakavyomfaidi. Bila kuwajibika, uhusiano utazorota hata ikiwa kulikuwa na hisia za kimahaba zenye nguvu kadiri gani wenzi hao walipoanza kupendana.

Biblia inaonyesha kwamba kudumisha ndoa ni kazi ngumu. Inasema kwamba “mwanamume aliyeoa huhangaikia mambo ya ulimwengu, jinsi anavyoweza kupata kibali cha mke wake,” na kwamba “mwanamke aliyeolewa huhangaikia mambo ya ulimwengu, jinsi anavyoweza kupata kibali cha mume wake.” (1 Wakorintho 7:33, 34) Kwa kusikitisha, nyakati nyingine hata wenzi ambao kwa kawaida hawana ubinafsi hawatambui mwenzi wao anapohangaika au hawathamini anapojidhabihu. Wenzi wanapokosa kuonyeshana uthamini, ndoa yao itawafanya wawe na ‘dhiki nyingi katika mwili wao’ kuliko kawaida.—1 Wakorintho 7:28.

Ili ndoa yako ikabiliane na hali ngumu na iimarike hali zinapokuwa nzuri, unahitaji kukumbuka kwamba hicho ni kifungo cha kudumu. Unaweza kusitawisha mtazamo huo jinsi gani, na unaweza kumtia moyo mwenzi wako awajibike kwako namna gani?

Jinsi ya Kuimarisha Uwajibikaji

Jambo kuu ni kuwa mnyenyekevu na kufuata mashauri ya Neno la Mungu, Biblia. Kwa kufanya hivyo ‘utajifaidi mwenyewe’ na mwenzi wako. (Isaya 48:17) Fikiria hatua mbili unazoweza kuchukua.

Tenga wakati kwa ajili ya mwenzi wako

1. Tanguliza ndoa yako.

“Mhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi,” akaandika mtume Paulo. (Wafilipi 1:10) Machoni pa Mungu, jinsi mume na mke wanavyotendeana ni muhimu sana. Mwanamume anayemheshimu mke wake ataheshimiwa na Mungu. Na mwanamke anayemheshimu mume wake ana “thamani kubwa machoni pa Mungu.”—1 Petro 3:1-4, 7.

Unathamini ndoa yako kadiri gani? Kwa kawaida, unapoona jambo fulani kuwa muhimu, unatumia wakati mwingi kulifanya. Jiulize: ‘Katika mwezi mmoja uliopita, nimetenga kiasi gani cha wakati ili kuwa na mwenzi wangu? Ni mambo gani hususa ambayo nimefanya ili kumhakikishia mwenzi wangu kwamba tungali marafiki wazuri?’ Ikiwa umetumia wakati mchache au hujatumia wakati wowote kuonyesha kwamba unamjali mwenzi wako, huenda asiamini kwamba unawajibika katika ndoa.

Je, mwenzi wako anafikiri kwamba umewajibika kwa ndoa yako? Utajua namna gani?

JARIBU KUFANYA HIVI: Andika kwenye karatasi mambo haya matano: pesa, kazi, ndoa, burudani, na marafiki. Sasa orodhesha kulingana na kile ambacho unadhani mwenzi wako anatanguliza. Mwambie mwenzi wako afanye hivyo kukuhusu. Mnapomaliza, badilishaneni orodha mlizoandika. Ikiwa mwenzi wako anafikiri kwamba hutumii wakati na jitihada za kutosha kuboresha ndoa yenu, zungumzieni mabadiliko ambayo huenda ukahitaji kufanya ili kuimarisha uwajibikaji wako. Pia, jiulize, ‘Ninaweza kufanya nini ili kupendezwa zaidi na mambo yaliyo muhimu kwa mwenzi wangu?’

Ukosefu wa uaminifu unaanzia moyoni

2. Epuka kukosa uaminifu katika njia yoyote.

Yesu Kristo alisema: “Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” (Mathayo 5:28) Mtu anapofanya ngono nje ya ndoa, yeye analeta pigo kubwa kwa muungano huo, na Biblia inasema kwamba kufanya hivyo ni msingi wa talaka. (Mathayo 5:32) Hata hivyo, maneno ya Yesu yaliyonukuliwa hapo juu yanaonyesha kwamba tamaa mbaya huwa katika moyo wa mtu hata kabla hajafanya uzinzi. Kwa kweli, kukuza tamaa hiyo mbaya ni kumsaliti mwenzi wako.

Ili kuwajibika sikuzote katika ndoa yako, azimia kabisa kutotazama ponografia. Tofauti na maoni ya watu wengi, ponografia ni sumu katika ndoa. Ona jinsi mke mmoja anavyoeleza hisia zake kuhusu mazoea ya mume wake ya kutazama ponografia: “Mume wangu anasema kwamba kutazama ponografia kunachochea hisia zetu za kimahaba. Lakini hilo linanifanya nijihisi sifai na simtoshelezi. Mimi ninalala nikilia anapotazama ponografia.” Je, ungesema kwamba mwanamume huyo anawajibika zaidi kwa ndoa yake au kuwajibika kwake kunazorota? Je, unafikiri kwamba anafanya iwe rahisi kwa mke wake kuendelea kuwajibika kwa ndoa yao? Je, anamtendea kama rafiki yake wa karibu zaidi?

Mwanamume mwaminifu Ayubu alieleza kuhusu uwajibikaji wake kwa ndoa na kwa Mungu kwa kufanya ‘agano pamoja na macho yake.’ Aliazimia ‘kutokaza fikira kwa bikira.’ (Ayubu 31:1) Unaweza kumwiga Ayubu jinsi gani?

Zaidi ya kuepuka ponografia, unahitaji kulinda moyo wako usipendezwe kwa njia isiyofaa na mtu wa jinsia nyingine. Ni kweli, wengi wanahisi kwamba kucheza kimapenzi na mtu wa jinsia tofauti hakuwezi kudhuru ndoa. Lakini Neno la Mungu linatuonya: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari. Ni nani anayeweza kuujua?” (Yeremia 17:9) Je, moyo wako umekudanganya? Jiulize: ‘Mimi ninapendezwa na nani zaidi, mwenzi wangu au mtu mwingine wa jinsia tofauti? Mimi ninamwambia nani kwanza habari njema, mwenzi wangu, au mtu mwingine? Mwenzi wangu akiniomba niache kushirikiana na mtu fulani wa jinsia tofauti, nitatenda jinsi gani? Je, nitakasirika, au nitafurahi kufanya mabadiliko hayo?’

JARIBU KUFANYA HIVI: Ukiona kwamba unavutiwa na mtu mwingine ambaye si mwenzi wako, usishirikiane naye isipokuwa iwe ni lazima kufanya hivyo. Usikazie fikira mambo yanayomfanya mtu huyo mwingine awe bora kuliko mwenzi wako. Badala yake, fikiria sifa nzuri za mwenzi wako. (Methali 31:29) Kumbuka ni kwa nini ulimpenda mwenzi wako. Jiulize, ‘Je, kweli mwenzi wangu amepoteza sifa hizo, au nimeacha kuziona?’

Chukua Hatua ya Kwanza

Michael na Maria walionukuliwa mwanzoni, waliamua kuomba mashauri kuhusu wanavyoweza kutatua matatizo yao. Bila shaka, kuomba mashauri ni hatua ya kwanza tu. Lakini kwa sababu walikuwa tayari kukabiliana na matatizo yao na kuomba msaada, Michael na Maria walionyesha waziwazi kwamba wamewajibika katika ndoa yao na kwamba walikuwa tayari kujitahidi kuifanya ifanikiwe.

Iwe ndoa yako ni imara au ina matatizo, mwenzi wako anahitaji kujua kwamba unajitahidi kufanikisha ndoa yenu. Chukua hatua zozote zinazohitajika ili umhakikishie mwenzi wako jambo hilo. Je, uko tayari kufanya hivyo?

^ fu. 3 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 5 Ingawa hapa tunataja mfano wa mwanamume aliyetazama ponografia, mwanamke anayefanya hivyo angekuwa pia akikosa kuwajibika katika ndoa.

JIULIZE . . .

  • Ni mambo gani ninayoweza kupunguza ili niwe na wakati zaidi wa kuwa na mwenzi wangu?

  • Ninaweza kufanya nini ili kumhakikishia mwenzi wangu kwamba ninawajibika kwa ndoa yetu?