Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unajenga Juu ya Mchanga au Mwamba?

Unajenga Juu ya Mchanga au Mwamba?

Unajenga Juu ya Mchanga au Mwamba?

JE, WEWE unafurahia kusoma Biblia? Je, unatenga wakati wa kujifunza Biblia kwa ukawaida na Mashahidi wa Yehova? Ikiwa ndivyo, bila shaka ujuzi ambao umepata umekusaidia kuelewa ni kwa nini ulimwengu wa sasa umekumbwa na matatizo mengi. (Ufunuo 12:9, 12) Kwa kuongezea, maandiko mengi ya Biblia yamekupa faraja nyakati za taabu na tumaini kwa ajili ya wakati ujao.—Zaburi 145:14; 147:3; 2 Petro 3:13.

Kupata ujuzi sahihi wa Biblia ni muhimu kwa wale wanaotaka kuwa wafuasi wa Kristo. Lakini je, hiyo ndiyo hatua pekee? Hapana. Ili kuendelea kuwa Mkristo wa kweli, hasa imani inapojaribiwa, mwanafunzi wa Biblia anahitaji kuchukua hatua nyingine muhimu. Hatua gani hiyo? Ili kupata jibu, acheni tuchunguze kwa ufupi Mahubiri ya Mlimani, hotuba ambayo Yesu alitoa juu ya mlima wa Galilaya.—Mathayo 5:1, 2.

Nyumba Mbili Zajaribiwa

Je, unafahamu habari zilizozungumziwa katika Mahubiri ya Mlimani? Unaweza kusoma hotuba hiyo maarufu katika vitabu vya Injili vya Mathayo na Luka. (Mathayo 5:1–7:29; Luka 6:20-49) Unaweza kuisoma yote kwa dakika 20 hivi. Hata hivyo, ina manukuu zaidi ya 20 kutoka kwenye Maandiko ya Kiebrania na zaidi ya mifano 50. Mfano mmoja, unaohusu ujenzi wa nyumba mbili, ni wa pekee kwa sababu Yesu aliutumia katika umalizio wa hotuba yake. Ukielewa umuhimu wa mfano huo, utaweza kuona jinsi unavyoweza kuendelea kusimama imara ukiwa mfuasi wa Kristo hata imani yako inapojaribiwa.

Yesu alisema: “Kila mtu anayesikia maneno yangu haya na kuyatenda atafananishwa na mtu mwenye busara, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba. Na mvua ikanyesha na mafuriko yakaja na pepo zikavuma na kuipiga nyumba hiyo, lakini haikuporomoka, kwa maana msingi wake ulikuwa umejengwa juu ya mwamba. Zaidi ya hayo, kila mtu anayesikia maneno yangu haya na hayatendi atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga. Na mvua ikanyesha na mafuriko yakaja na pepo zikavuma na kuigonga nyumba hiyo, nayo ikaporomoka, na anguko lake lilikuwa kubwa.”—Mathayo 7:24-27.

Mtu ‘Aliyechimba Akaenda Chini Kina Kirefu’

Ni kweli gani muhimu ambayo Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kwa mfano huo wa wajenzi wawili? Ili kupata jibu, chunguza kwa makini maneno ya Yesu. Unaona nini kuhusu nyumba hizo mbili? Zote mbili zilipatwa na hali mbaya zinazolingana. Huenda nyumba hizo zikawa zilifanana. Huenda hata zilijengwa katika eneo lilelile. Hata hivyo, moja ilijengwa juu ya mchanga, nyingine juu ya mwamba. Hilo lingewezekana namna gani? Kwa sababu, kama Injili ya Luka ilivyosema, yule mtu mwenye busara “alichimba akaenda chini kina kirefu” ili afikie mwamba. (Luka 6:48) Kwa sababu hiyo, nyumba ya mtu mwenye busara ilisimama imara.

Yesu alitaka kukazia jambo gani? Yesu alisimulia mfano huo ili kukazia, si sura au eneo la nyumba hizo au nguvu za hali ya hewa, lakini alitaka kuonyesha jinsi wajenzi walivyotenda. Mtu mmoja alichimba akaenda chini kina kirefu, lakini yule mwingine hakufanya hivyo. Unaweza kuwa kama mtu yule mwenye busara na kuchimba chini kina kirefu kwa njia gani? Yesu mwenyewe alieleza jambo kuu la mfano huo kwa kusema: “Kwa nini, basi, mnaniita ‘Bwana! Bwana!’ lakini hamfanyi mambo ninayosema? Kila mtu anayekuja kwangu na kusikia maneno yangu na kuyatenda, nitawaonyesha ninyi yeye anafanana na nani: Huyo anafanana na mtu . . . ambaye alichimba akaenda chini kina kirefu na kuweka msingi juu ya mwamba.”—Luka 6:46-48.

Kwa kweli, kusikiliza tu mafundisho ya Biblia au kusoma Biblia nyumbani ni kama kujenga nyumba juu ya mchanga bila kuchimba. Lakini kufanya, au kufuata, mafundisho ya Kristo kunahitaji jitihada. Kunahusisha kuchimba chini kina kirefu ili kufikia mwamba.

Hivyo, kusimama imara ukiwa mfuasi wa Kristo kunategemea ikiwa utafuata au hutafuata yale unayosikia. Kila siku unapofuata yale unayojifunza katika funzo la Biblia, utakuwa kama mtu mwenye busara aliyechimba chini kina kirefu. Hivyo, kila mwanafunzi wa Biblia anapaswa kujiuliza, ‘Mimi ni msikiaji, au mimi ni mtendaji? Je, mimi ninasoma tu na kujifunza Biblia, au je, mimi ninafuata amri za Biblia ninapofanya maamuzi?’

Matokeo ya Kuchimba Chini Kina Kirefu

Fikiria mfano wa José. Wazazi wake walimlea ili aheshimu viwango vya maadili vya Biblia, lakini hakujifunza Neno la Mungu kibinafsi. “Nilipoondoka nyumbani,” anasema José, “nilijaribu kuishi maisha mazuri lakini nilizungukwa na marafiki wabaya. Nilianza kutumia dawa za kulevya, nikafanya uasherati, na nilipigana mara nyingi na watu wengine.”

Mwishowe, José aliamua kubadili maisha yake na akaanza kujifunza Biblia kwa bidii. “Jambo moja lililonichochea kubadilika,” anasema José, “ni kusoma na kuelewa Mahubiri ya Mlimani ya Yesu. Lakini nilichukua muda kufanya mabadiliko katika utu na maisha yangu. Mwanzoni niliogopa ‘marafiki’ wangu wangesema nini, lakini nilikabiliana na wasiwasi huo. Niliacha kusema uwongo na kutumia matusi na nikaanza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Nilijifunza kwamba kama vile Yesu alivyoahidi, kuishi maisha rahisi na kufuata mashauri ya Biblia kunaleta furaha ya kudumu.”—Mathayo 5:3-12.

Utapata matokeo gani kwa kuchimba chini kina kirefu ili ujenge juu ya mwamba, yaani, unapofuata kwa bidii yale unayosoma katika Neno la Mungu? Yesu alisema: “Mafuriko yalipotokea, mto uliipiga nyumba hiyo kwa nguvu, lakini haukuwa na nguvu za kutosha kuitikisa, kwa sababu ilikuwa imejengwa vizuri.” (Luka 6:48) Bila shaka, ukijenga vizuri kwa kufuata yale unayojifunza, majaribu yanayofanana na dhoruba hayataweza kuvunja nyumba yako wala hayataweza kuitikisa. Hilo ni wazo lenye kufariji kama nini!

Mwanafunzi Yakobo, ndugu wa kambo wa Yesu, anataja baraka nyingine ambayo wanafunzi wa Biblia ambao si wasikiaji tu bali pia watendaji wa kweli wa Neno la Mungu lililoandikwa watapata. Yakobo aliandika: “Iweni watendaji wa neno, na si wasikiaji tu . . . Yeye anayechunguza ndani ya sheria kamilifu iliyo ya uhuru na ambaye hudumu katika hiyo, mtu huyo, kwa sababu amekuwa, si msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, atakuwa mwenye furaha katika kuitenda.”—Yakobo 1:22-25.

Kwa kweli, wale wanaofuata mashauri ya Biblia wana furaha ya kweli. Furaha kama hiyo inawapa wafuasi wa Kristo nguvu za kusimama imara wanapopatwa na majaribu yaliyo kama dhoruba yanayojaribu imani na kina cha ujitoaji wao kwa Mungu.

Utafanya Nini?

Yesu alipotoa Mahubiri yake ya Mlimani, alikazia kwamba mara nyingi kumtumikia Yehova Mungu kunahusisha, si kufanya hili na lile, bali kufanya hili au lile. Kwa mfano, Yesu alifundisha kwamba lazima mtu awe, ama na jicho rahisi ama na jicho bovu, kwamba atamtumikia Mungu au utajiri, kwamba atatembea ama kwenye barabara yenye nafasi ndogo ama kwenye ile pana. (Mathayo 6:22-24; 7:13, 14) Kisha, katika mfano wake wa kumalizia wa wajenzi wawili, Yesu aliwapa wafuasi wake jambo lingine la kujiamulia: Tendeni kama mtu mwenye busara au kama yule mpumbavu.

Ukiendelea kufuata kwa moyo wote mambo unayojifunza katika Biblia, unatenda kwa busara. Naam, kuchimba chini kina kirefu kwenye mwamba kutakuletea baraka sasa na wakati ujao.—Methali 10:25.

[Picha katika ukurasa wa 30]

Ili tusimame imara tunapaswa kufuata yale tunayojifunza