Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

BIBLIA INABADILI MAISHA

Nilifikiri Ninafurahia Maisha

Nilifikiri Ninafurahia Maisha
  • ALIZALIWA: 1982

  • NCHI: POLAND

  • HISTORIA: ALITUMIA DAWA ZA KULEVYA, ALIKUWA MWENYE JEURI, NA ALITAKA KAZI NZURI

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilizaliwa katika mji mdogo nchini Poland, ulio karibu na mpaka wa Ujerumani. Nilifurahia kuishi katika eneo hilo ambalo limezungukwa na mashamba pamoja na misitu. Wazazi wangu wapendwa walinichochea niwe mtu mzuri, nifanye vizuri shuleni, na hatimaye nipate kazi nzuri.

Matatizo yalianza nilipojiunga na chuo kikuu jijini Wrocław ili kusoma sheria. Nikiwa mbali na wazazi wangu, nilishirikiana na marafiki wabaya. Nilipenda mpira wa miguu, lakini kwa sababu ya uvutano wa marafiki hao wabaya nikawa shabiki mkubwa wa mchezo huo. Timu niliyoipenda sana ilitoka kwenye mji wa Warsaw, na kila mwisho juma ningeenda popote pale timu hiyo ilipokuwa ikicheza. Tulipokuwa huko tulitumia dawa za kulevya, tulikunywa pombe kupita kiasi, na mara nyingine tulianzisha vurugu na kupigana na mashabiki wa timu pinzani. Nilifanya hivyo ili kuondoa mawazo, lakini nilijua kwamba ningekatisha ndoto zangu za kuwa mwanasheria ikiwa ningekamatwa na polisi.

Mimi na rafiki zangu tulipenda kwenda disko na kwenye kumbi za starehe. Mara nyingi, tulishiriki katika vurugu za mitaani. Nilikamatwa na polisi mara kadhaa, lakini sikuzote niliepuka kupelekwa mahakamani na hata nyakati nyingine nilitoa rushwa ili niachiliwe. Kwa kweli nilifikiri ninafurahia maisha. Hata hivyo, moyoni nilijua kwamba mambo niliyofanya yalikuwa mabaya. Ili kuituliza dhamiri yangu, nilikwenda kanisani kila Jumapili.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Mwaka 2004, Mashahidi wawili wa Yehova walinitembelea nyumbani kwangu, nami nilikubali kujifunza Biblia. Kadiri nilivyoendelea kujifunza jinsi Mkristo wa kweli anavyopaswa kuwa, dhamiri yangu ilianza kunisumbua sana. Nilijua ninapaswa kuacha kunywa pombe kupita kiasi, kutumia dawa za kulevya, na kushirikiana na watu ambao hawafuati viwango vya Biblia. Pia nilihitaji kuacha ugomvi. Ingawa nilitambua kwamba nilihitaji kubadilika, bado niliendelea kufanya mambo mabaya.

Mambo yalibadilika usiku mmoja nilipoanzisha ugomvi na wanaume nane. Nakumbuka waliniangusha chini na kunipiga ngumi na mateke kichwani. Nilipohisi nakaribia kufa, nilisali hivi: “Yehova, ninaomba unisamehe kwa kutozingatia Neno lako. Ikiwa nitatoka salama, ninaahidi kujifunza Biblia na Mashahidi na kurekebisha maisha yangu.” Jambo la kushangaza ni kwamba niliponyoka. Nami nikatimiza ahadi yangu ya kujifunza Biblia.

Mwaka 2006, nilihamia Uingereza. Lengo langu lilikuwa kutafuta pesa nyingi ili nirudi Poland kuendelea kusomea zaidi sheria. Nilipoendelea kujifunza Biblia, andiko moja lilinigusa sana. Mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa kweli naviona vitu vyote kuwa hasara kwa sababu ya thamani bora zaidi ya kumjua Kristo Yesu Bwana wangu. Kwa sababu yake nimekubali hasara ya vitu vyote nami naviona kuwa takataka nyingi, ili niweze kumpata Kristo.” (Wafilipi 3:8) Paulo alisomea sheria na pia alikuwa mtu mwenye jeuri kama mimi. (Matendo 8:3) Lakini alitambua njia bora ya kutumia maisha yake, yaani, kumtumikia Mungu na kufanya yote awezayo kumwiga Yesu. Nilipotafakari mfano wa Paulo, nilitambua kwamba furaha ya kweli haitokani na kazi nzuri au kuwa mwenye jeuri. Nilitambua kwamba ikiwa Paulo alibadilika basi hata mimi ningeweza kubadilika. Hivyo, niliamua kubaki Uingereza na kusitisha mipango yangu ya kuendelea na masomo ya sheria.

Kadiri nilivyojifunza kumhusu Yehova, ndivyo nilivyomkaribia zaidi. Niliguswa na ahadi ya Yehova ya kuwasamehe wale ambao kwa unyofu wanataka kufanya mabadiliko. (Matendo 2:38) Nilipotafakari andiko la 1 Yohana 4:16, linalosema “Mungu ni upendo,” nilianza kuelewa kwa nini Mungu anachukia jeuri.

Nilitaka kuwa miongoni mwa Mashahidi wenye furaha

Pia nilishangazwa na mwenendo wa Mashahidi. Niliona kwamba wanajitahidi kuishi kulingana na viwango vya juu vya maadili vya Biblia. Nilitaka kuwa miongoni mwa waabudu hao wenye furaha. Baada ya jitihada nyingi na kufanya mabadiliko mengi maishani, nilibatizwa mwaka 2008 na kuwa Shahidi wa Yehova.

Mimi na Esther tunafurahia sana kuwafundisha Biblia watu wanaozungumza Kipolandi

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Biblia imenibadili kutoka kuwa mtu anayependa makuu, mgomvi, anayetumia dawa za kulevya, mlevi, shabiki mkubwa wa mpira wa miguu hadi kuwa mtumishi wa Mungu ambaye anafurahia kuwafundisha wengine Biblia. Bado ninapenda kutazama mpira wa miguu, lakini siruhusu burudani hiyo itawale maisha yangu.

Sasa ninafurahia maisha ya ndoa pamoja na mke wangu mrembo Esther, ambaye pia ni mwabudu mwenzangu wa Yehova. Tunafurahia sana kuwafundisha Biblia watu wanaozungumza Kipolandi hapa kaskazini magharibi mwa Uingereza. Kwa mara ya kwanza maishani, ninahisi nimeridhika kabisa. Nina dhamiri safi na maisha yenye kusudi.