Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

BIBLIA INABADILI MAISHA

Sikutaka Kufa!

Sikutaka Kufa!
  • ALIZALIWA: 1964

  • NCHI: UINGEREZA

  • HISTORIA: BINTI ALIYEKUWA MWASI

MAISHA YANGU YA ZAMANI

Nilizaliwa Paddington, eneo lenye watu wengi jijini London, Uingereza. Niliishi na mama na dada zangu watatu. Baba alikuwa mraibu wa pombe, hivyo, kwa muda mrefu hakuishi nasi.

Nilipokuwa mtoto, mama alinifundisha kusali kila usiku. Nilikuwa na Biblia ndogo iliyokuwa na kitabu cha Zaburi pekee na niliitumia kutunga nyimbo ambazo niliimba. Ninakumbuka siku moja nilisoma kwenye kitabu fulani jambo ambalo lilinishtua sana: “Siku moja kesho haitakuwepo.” Mara kwa mara maneno hayo yalifanya nikose usingizi nikifikiria kuhusu wakati ujao. Niliwaza hivi: ‘Bila shaka maisha yana kusudi. Kwa nini niko hai?’ Sikutaka kufa!

Nilianza kupendezwa sana na mambo ya ushirikina. Nilijaribu kuwasiliana na wafu, tulienda makaburini na wanafunzi wenzangu, na tulitazama sinema zenye kutisha. Ingawa mambo hayo yalifurahisha, yalituogopesha pia.

Nilipokuwa na umri wa miaka kumi tu, nilianza kuwa mtukutu. Nilianza kuvuta sigara na punde si punde nikawa mraibu. Baadaye, nilianza kuvuta bangi. Nikiwa na umri wa miaka 11, nilianza kunywa pombe. Ingawa sikufurahia ladha yake, nilipenda kulewa. Pia, nilipenda muziki na kucheza dansi. Kila nilipopata fursa nilienda kwenye karamu na vilabu vya usiku. Nilitoroka nyumbani usiku na kurudi kabla hakujapambazuka. Kwa sababu ya uchovu, siku iliyofuata nisingeweza kwenda shuleni. Na ikiwa ningefaulu kwenda, nilikunywa pombe wakati wa masomo.

Nilipata alama za chini sana nilipofanya mtihani wa mwisho. Kwa kuwa mama hakujua kuhusu mwenendo wangu mbaya, matokeo niliyopata yalifunua jambo hilo, hivyo alikasirika sana na kuvunjika moyo. Mimi na mama tulizozana, na kisha nikatoroka nyumbani. Kwa muda fulani, niliishi na Tony, rafiki yangu wa kiume ambaye alikuwa Rastafari. Tony alikuwa mwizi, aliuza dawa za kulevya na alikuwa mjeuri sana. Muda mfupi baadaye, nikiwa na umri wa miaka 16, nilipata mtoto.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU

Nilikutana na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza nilipokuwa nikiishi katika makao ya kuwatunzia watoto na mama zao ambao hawajaolewa. Nilipewa chumba na wenye mamlaka. Mashahidi wawili walikuwa na kawaida ya kuwatembelea mama wengine wenye umri mdogo. Siku moja nilijiunga kwenye mazungumzo yao. Nia yangu ilikuwa kuwakosoa Mashahidi. Hata hivyo, kwa upole walijibu maswali yangu yote kupitia Biblia. Nilipendezwa sana na jinsi walivyonitendea kwa fadhili na upole. Hivyo, nikakubali kujifunza Biblia.

Muda si muda, nilijifunza jambo fulani katika Biblia ambalo lilibadili maisha yangu. Tangu nilipokuwa mdogo, niliogopa kufa. Hata hivyo, nikajifunza kwamba Yesu alifundisha kuhusu ufufuo! (Yohana 5:28, 29) Pia, nilijifunza kuwa Mungu ananijali kibinafsi. (1 Petro 5:7) Niliguswa moyo sana na andiko la Yeremia 29:11 linalosema hivi: “‘Kwa maana mimi najua vema mawazo ninayofikiria kuwaelekea ninyi,’ asema Yehova, ‘mawazo ya amani, wala si ya msiba, ili kuwapa ninyi wakati ujao na tumaini.’” Nilianza kuwa na tumaini la kuishi milele katika dunia itakayokuwa Paradiso.—Zaburi 37:29.

Mashahidi wa Yehova walinipenda kutoka moyoni. Nilipohudhuria mikutano yao kwa mara ya kwanza, wote walinikaribisha kwa furaha na uchangamfu! (Yohana 13:34, 35) Hilo lilikuwa tofauti kabisa na nilivyotendewa katika kanisa nililoshirikiana nalo awali. Mashahidi walinikaribisha licha ya hali yangu. Walitumia muda pamoja nami, walinitunza na kunisikiliza, na pia walinipatia msaada wa kimwili. Nilijihisi kuwa sehemu ya familia kubwa yenye upendo.

Nilipojifunza Biblia, nilitambua kwamba nilihitaji kufanya mabadiliko maishani ili niishi kulingana na viwango vya juu vya Mungu vya maadili. Haikuwa rahisi kuacha kuvuta sigara. Wakati huo pia, nilitambua kuwa kusikiliza aina fulani ya muziki kulichochea hamu yangu ya kuvuta bangi, hivyo nikaacha kusikiliza muziki huo. Niliacha kwenda kwenye tafrija na vilabu vya usiku ili nisishawishike kunywa pombe. Pia nilitafuta marafiki wenye mwenendo mzuri ili wanisaidie kudumisha maisha safi.—Methali 13:20.

Wakati huohuo, Tony pia alikuwa akijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Kwa kuwa Mashahidi walimjibu maswali yake kwa kutumia Biblia, aliamini kwamba yale aliyokuwa akijifunza ni kweli. Alifanya mabadiliko makubwa sana maishani mwake: aliacha kushirikiana na watu wenye jeuri, kuiba, na akaacha kuvuta bangi. Ili sote tumpendeze Yehova kikamili, tuliamua kubadili maisha yetu mapotovu, na hivyo kumlea mtoto wetu katika mazingira yanayofaa. Tulifunga ndoa mwaka wa 1982.

“Sasa, sikosi usingizi kwa sababu ya kuhofu kuhusu wakati ujao au kifo”

Nakumbuka nikitafuta makala kwenye magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! * zilizokuwa na masimulizi ya watu ambao walifanya mabadiliko kama yangu. Mifano yao ilinitia moyo sana. Nilichochewa kuendelea kuwa na bidii na kutovunjika moyo. Niliendelea kumwomba Yehova anisaidie kufanya mabadiliko. Mimi na Tony tulibatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova mwaka wa 1982.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA

Kusitawisha urafiki pamoja na Yehova kuliokoa maisha yangu. Pia, mimi na Tony tumetegemezwa sana na Yehova wakati wa shida. Tumejifunza kumtegemea Mungu tunapopatwa na magumu, na kwa hakika ametusaidia na kututegemeza.—Zaburi 55:22.

Nilifurahia kumsaidia mwana na binti yetu wamjue Yehova. Nina shangwe ninapowaona wajukuu wangu pia wakijifunza na kumjua Mungu.

Sasa, sikosi usingizi kwa sababu ya kuhofu kuhusu wakati ujao au kifo. Kila juma, mimi na Tony huyatembelea makutaniko mbalimbali ya Mashahidi wa Yehova ili kuwatia moyo. Pia, tunashirikiana nao kuwafundisha wengine kwamba wakimwamini Yesu watafurahia maisha milele.

^ fu. 19 Linalochapishwa na Mashahidi wa Yehova.