Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 28

Kwa Nini Wanafunzi wa Yesu Hawafungi?

Kwa Nini Wanafunzi wa Yesu Hawafungi?

MATHAYO 9:14-17 MARKO 2:18-22 LUKA 5:33-39

  • WANAFUNZI WA YOHANA WAMUULIZA YESU KUHUSU KUFUNGA

Yohana Mbatizaji amekuwa gerezani kwa kipindi fulani baada ya Yesu kuhudhuria Pasaka ya mwaka wa 30 W.K. Yohana alitaka wanafunzi wake wawe wafuasi wa Yesu, lakini si wote wanaofanya hivyo miezi inayofuata baada ya Yohana kufungwa gerezani.

Sasa, Pasaka ya mwaka wa 31 W.K. inapokaribia, baadhi ya wanafunzi wa Yohana wanamjia Yesu na kuuliza: “Kwa nini sisi na Mafarisayo hufunga lakini wanafunzi wako hawafungi?” (Mathayo 9:14) Mafarisayo hufunga kwa kuwa ni desturi yao ya kidini. Baadaye, hata Yesu anatumia mfano wa Farisayo anayejiona mwadilifu na kusali hivi: “Ee Mungu, ninakushukuru kwa sababu mimi si kama watu wengine . . . Mimi hufunga mara mbili kwa juma.” (Luka 18:11, 12) Labda pia wanafunzi wa Yohana walikuwa na desturi ya kufunga. Au huenda walikuwa wakifunga ili kuombolezea kifungo cha Yohana gerezani. Wengine pia wanashangaa kwa nini wanafunzi wa Yesu hawafungi, labda ili kuonyesha kwamba wao pia wanahuzunishwa na mambo ambayo Yohana ametendewa.

Yesu anawajibu kwa kutumia mfano: “Rafiki za bwana harusi hawahitaji kuomboleza bwana harusi anapokuwa pamoja nao, sivyo? Lakini siku zitakuja ambapo bwana harusi ataondolewa kwao, ndipo watakapofunga.”—Mathayo 9:15.

Yohana mwenyewe alimtaja Yesu kuwa bwana harusi. (Yohana 3:28, 29) Kwa hiyo, Yesu akiwapo wanafunzi wake hawahitaji kufunga. Baadaye, Yesu atakapokufa, wanafunzi wake wataomboleza na hawatakuwa na hamu ya kula. Hata hivyo, mambo yatabadilika sana atakapofufuliwa! Wakati huo hawatakuwa na sababu ya kuomboleza na kufunga.

Kisha, Yesu anawapa mifano hii miwili: “Hakuna mtu anayeshona kiraka cha kitambaa kipya juu ya vazi la nje la zamani; kwa maana hicho kitambaa kipya kitatoka kwenye hilo vazi nalo litararuka vibaya zaidi. Wala watu hawaweki divai mpya katika viriba vya divai vilivyochakaa. Wakifanya hivyo, viriba hivyo vitapasuka na divai itamwagika navyo viriba vitaharibika. Lakini watu huweka divai mpya katika viriba vipya vya divai.” (Mathayo 9:16, 17) Yesu anamaanisha nini?

Yesu anawasaidia wanafunzi wa Yohana Mbatizaji waelewe kwamba mtu yeyote asitarajie kwamba wafuasi wa Yesu watafuata desturi za zamani za Kiyahudi, kama vile desturi ya kufunga. Hakuja kuweka viraka na kuendeleza mfumo wa zamani wa ibada uliochakaa, uliokuwa karibu kutupiliwa mbali. Ibada ambayo Yesu anapendekeza si ile inayofuata dini ya Kiyahudi ya wakati huo na desturi zake za wanadamu. Hapana, Yesu hajaribu kuweka kitambaa kipya juu ya vazi la zamani au divai mpya kwenye kiriba cha zamani kilichokauka.