Hamia kwenye habari

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Hawasherehekei Krismasi?

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Hawasherehekei Krismasi?

Maoni yasiyo sahihi

 Uwongo: Mashahidi wa Yehova hawasherehekei Krismasi kwa sababu hawamwamini Yesu.

 Ukweli: Sisi ni Wakristo. Tunaamini kwamba wokovu hupatikana kupitia Yesu Kristo.—Matendo 4:12.

 Uwongo: Mnaleta mgawanyiko katika familia kwa kuwafundisha watu wasisherehekee Krismasi.

 Ukweli: Tunajali sana familia, na hivyo tunatumia Biblia kusaidia kujenga familia imara.

 Uwongo: Hamfurahii kipindi cha Krismasi kinachohusisha ukarimu, kuleta amani duniani, na nia njema kwa watu wote.

 Ukweli: Tunajitahidi kuwa wakarimu na wenye kufanya amani kila siku. (Methali 11:25; Waroma 12:18) Kwa mfano, katika mikutano na mahubiri yetu tunafuata agizo hili la Yesu: “Mlipokea bure, toeni bure.” (Mathayo 10:8) Kwa kuongezea, tunakazia Ufalme wa Mungu kuwa tumaini pekee la kuleta amani duniani.—Mathayo 10:7.

Kwa nini Mashahidi wa Yehova hawasherehekei Krismasi?

  •   Yesu aliagiza tukumbuke kifo chake, bali si kuzaliwa kwake.—Luka 22:19, 20.

  •   Mitume na wanafunzi wa mapema wa Yesu hawakusherehekea Krismasi. Kitabu New Catholic Encyclopedia kinasema kwamba “sherehe ya Krismasi ilianzishwa baada ya 243 [W.K.],” zaidi ya karne moja baada ya mtume wa mwisho kufa.

  •   Yesu hakuzaliwa Desemba 25; tarehe yake ya kuzaliwa haijaandikwa katika Biblia.

  •   Tunaamini kwamba Mungu hapendezwi na Krismasi kwa sababu chanzo chake ni desturi na itikadi za kipagani.—2 Wakorintho 6:17.

Kwa nini msifuate maoni ya wengi?

 Bado wengi wanasherehekea Krismasi ingawa wanajua chanzo chake ni cha kipagani na haiungwi mkono na Biblia. Huenda watu kama hao wakauliza: Kwa nini msiwe kama watu wengine? Kwa nini muwe tofauti?

 Biblia inatuhimiza tufikirie kwa makini, tutumie ‘nguvu zetu za kufikiri.’ (Waroma 12:1, 2) Inatufundisha tuthamini ukweli. (Yohana 4:23, 24) Basi, ingawa tunajali jinsi watu wanavyotuona, bado tutafuata kanuni za Biblia hata kama tutachukiwa.

 Ingawa tumeamua kutosherehekea Krismasi, tunaheshimu haki ya kila mtu ya kujiamulia jambo hilo. Hatuwazuii wengine kusherehekea Krismasi.