Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SEHEMU YA KUULIZA MAULIZO | FENG-LING YANG

Mwanasayansi wa Mikrobiolojia Anaeleza Imani Yake

Mwanasayansi wa Mikrobiolojia Anaeleza Imani Yake

Feng-Ling Yang ni muchunguzi-musaidizi kwenye masomo makubwa ya uchunguzi katika muji wa Taipei, kisiwa cha Taiwan. Kazi yake imechapishwa katika magazeti ya kisayansi. Alikuwa anaamini fundisho la mageuzi. Lakini alibadilisha mawazo yake. Gazeti Amuka! lilimuuliza juu ya kazi yake ya sayansi na juu ya imani yake.

Tuambie kuhusu familia yenu.

Wazazi wangu walikuwa maskini sana, na mama yangu hakujua kusoma. Tulikuwa tunafuga nguruwe na tulikuwa tunalima mboga za majani katika eneo lililokuwa likifunikwa na maji karibu na muji wa Taipei. Wazazi wangu walinifundisha ulazima wa kutumika sana, na walinifundisha pia kuwasaidia wengine.

Je, watu wa familia yako walikuwa na dini?

Watu wa familia yangu walikuwa katika dini ya Utao. Tulikuwa tunatoa zabihu za kidini lakini hatukujua jambo lolote juu ya Mungu wa kweli. Nilikuwa ninajiuliza: ‘Sababu gani watu wanateseka? Sababu gani watu ni wachoyo?’ Nilisoma vitabu juu ya dini ya Utao na dini ya Kibudha na juu ya historia ya Asia na Ulaya. Nilienda hata kwenye kanisa fulani. Lakini sikupata majibu ya maulizo yangu.

Sababu gani ulijifunza sayansi?

Nilipenda sana hesabu na nilivutiwa sana na namna sheria za asili na za kemia zinavyoongoza muundo wa vitu. Kila kitu, kuanzia ulimwengu mukubwa sana mupaka vidudu vidogo sana, vina muundo unaoongozwa na sheria. Na nilipenda nielewe sheria hizo.

Sababu gani uliamini fundisho la mageuzi?

Sikujua fundisho lingine isipokuwa mageuzi. Kuanzia kwenye masomo ya musingi mupaka kwenye masomo ya juu, nilikuwa ninasikia tu mafasirio juu ya fundisho la mageuzi. Na kisha kwa sababu ya kuwa muchunguzi katika mambo ya sayansi, nilipaswa tu kukubali mageuzi.

Kwa sababu ya kuwa muchunguzi katika mambo ya sayansi, nilipaswa tu kukubali mageuzi

Ni nini iliyokufanya uanze kusoma Biblia?

Katika mwaka wa 1996, nilienda kuishi Ujerumani ili kuendelesha masomo yangu ya juu. Mwaka uliofuata nilikutana na kijana mwanamuke anayeitwa Simone. Alikuwa Shahidi wa Yehova, na alisema kwamba atanionyesha majibu ya Biblia kwa maulizo yangu. Nilipendezwa wakati aliniambia kwamba Biblia inaeleza kusudi la maisha. Nilianza kuamuka saa kumi na nusu kila asubuhi ili kusoma Biblia kwa muda wa saa moja. Kisha nilikuwa ninaenda kujitembeza kidogo ili kufikiri juu ya mambo niliyosoma. Mwaka uliofuata, nilisoma Biblia yote. Nilishangaa na namna Biblia ilivyotabiri mambo bila makosa. Polepole, nilisadiki kwamba Biblia iliongozwa na roho ya Mungu.

Ulikuwa na mawazo gani kuhusu namna uzima ulivyoanza?

Nilipoanza kufikiria jambo hilo kwa uzito mwishoni mwa miaka ya 1990 na kitu, wanabiolojia wa molekuli walianza kutambua kwamba ni vigumu sana kuelewa namna mwili unavyofanya kazi, watu hawakuwazia hivyo zamani. Bila shaka, kwa muda murefu wanasayansi walikuwa wanajua kwamba protini zilizo katika chembe zenye uzima ndizo molekuli zilizo na kemikali ngumu zaidi kueleweka. Lakini sasa, wamevumbua namna mikusanyo ya protini inavyopangwa ili kuunda mashini zenye kuvutia zilizo na sehemu zinazozunguka ndani ya mwili. Mashini ya molekuli inaweza kuundwa na protini zaidi ya 50. Na hata chembe rahisi zaidi ina lazima ya muungano wa mashini mbalimbali, kwa mufano, ili kutokeza nishati ao nguvu, kuweka habari, na kuzuia mambo yasiingie katika utando wa chembe.

Ulifikia uamuzi gani?

Nilijiuliza, ‘Namna gani mashini hizo za protini zimetengenezwa kwa njia ya ajabu hivyo?’ Wakati fulani, muundo wa ajabu wa chembe ambao haukutazamiwa kuwa hivyo ulifanya wanasayansi wengi wajiulize ulizo lilelile. Mwalimu mumoja wa biokemia katika inchi ya Amerika alichapisha kitabu kilichoeleza kwamba mashini za molekuli zilizo katika chembe zenye uzima ni za ajabu sana, hilo linaonyesha kwamba hazikujitokeza zenyewe tu. Nilikubaliana naye. Niliona kwamba uzima unapaswa kuwa uliumbwa.

Nilijiuliza, ‘Namna gani mashini hizo za protini zimetengenezwa kwa njia ya ajabu hivyo?’

Ni nini kilikufanya uwe Shahidi wa Yehova?

Nilishangaa kuona kwamba hata ikiwa Simone alikuwa mugonjwa, alisafiri kilometa 56 hivi kila juma ili kunifundisha Biblia. Nilisikia kwamba wakati wa utawala wa Wanazi katika Ujerumani, Mashahidi fulani walifungwa katika kambi za mateso kwa sababu walikataa kuunga mukono mambo ya siasa. Nilipendezwa sana na ujasiri wao. Upendo wao kwa Mungu ulinifanya nitake kuwa kama wao.

Je, kumuamini Mungu kumekuletea faida?

Wafanyakazi wenzangu wanasema kwamba sasa mimi ni mwenye furaha zaidi. Nilikuwa ninajisikia kuwa mutu wa hali ya chini kwa sababu nilizaliwa katika familia maskini, kwa hiyo sikumueleza mutu yeyote juu ya mahali nilipokomalia na juu ya wazazi wangu. Lakini nimejifunza kupitia Biblia kwamba Mungu haangalie hali ya mutu, awe tajiri ao maskini. Kwa kweli, Yesu pia alizaliwa katika familia ambayo labda ilikuwa maskini kama yetu. Sasa ninachunga wazazi wangu na ninafurahia kuwajulisha kwa marafiki wangu.