Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MAONI YA BIBLIA

Uumbaji

Uumbaji

Je, Mungu aliumba dunia kwa kipindi cha siku sita zenye urefu wa saa 24 kila moja, kama vile watu fulani wanavyosema?

“Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.”​—Mwanzo 1:1.

MAMBO BIBLIA INASEMA:

Mungu aliumba ulimwengu, kutia ndani dunia, wakati fulani usiojulikana wa zamani, ni kusema, “hapo mwanzo,” kama andiko la Mwanzo 1:1 linavyosema. Sayansi ya leo inakubali kwamba ulimwengu ulikuwa na mwanzo. Hivi karibuni, wanasayansi walikadiria kwamba ulimwengu uliumbwa kumepita miaka miliare 14.

Biblia pia inazungumuzia “siku” sita za uumbaji. Lakini, haiseme kwamba siku hizo zilikuwa siku za saa 24 kila moja. (Mwanzo 1:31) Kwa kweli, Biblia inatumia neno “siku” ili kumaanisha vipindi vya wakati vyenye urefu mbalimbali. Kwa mufano, Biblia inaita kipindi chote cha uumbaji “siku ambayo Yehova Mungu aliifanya dunia na mbingu.” (Mwanzo 2:4) Inawezekana “siku” hizo za uumbaji zilidumu maelfu ya miaka.​—Zaburi 90:4.

SABABU GANI NI LAZIMA UJUE JAMBO HILO?

Mawazo ya uongo ya watu wanaoamini kwamba ulimwengu uliumbwa kwa kipindi cha siku sita zenye saa 24 kila moja yanaweza kukufanya uzarau kabisa Biblia. Kwa upande mwengine, ikiwa Biblia ina habari za kweli juu ya uumbaji, unaweza kufaidika na hazina yake ya “hekima inayotumika.”​—Methali 3:21.

Je, Mungu alitumia mageuzi ili kuumba uzima duniani?

“Mungu akaendelea kusema: ‘Dunia na itokeze nafsi zilizo hai kulingana na aina zake.’”​—Mwanzo 1:24.

MAMBO BIBLIA INASEMA:

Mungu hakuumba uzima katika aina iliyo nyepesi na kuuacha ugeuke​-geuke katika aina nyingi za uzima zilizo ngumu kueleweka. Lakini, aliumba “aina” za kwanza​-kwanza za mimea na wanyama zilizokuwa ngumu kueleweka, zilizozaana “kulingana na aina zake.” (Mwanzo 1:11, 21, 24) Tendo hilo la kuzaana, ambalo linaendelea mupaka leo, limefanya dunia ijae “aina” za uzima ambazo Mungu aliumba hapo mwanzoni.​—Zaburi 89:11.

Biblia haieleze waziwazi mabadiliko mbalimbali yanayoweza kutokea katika aina moja ya uzima, kwa mufano wakati wanyama wa aina moja wanazaana na wakati wanajipatanisha na hali. Hata ikiwa wengine wanaona mabadiliko hayo kuwa ni mageuzi, hakuna aina mupya ya uzima inayotokezwa. Wachunguzi wa kisasa wanaunga mukono wazo la kwamba aina za kwanza​-kwanza za mimea na za wanyama zimebadilika kidogo kwa muda wa vipindi virefu vya wakati.

SABABU GANI NI LAZIMA UJUE JAMBO HILO?

Namna Biblia inavyoeleza bila makosa mambo ya sayansi kuhusu “aina” za kwanza​-kwanza za uzima inahakikisha kwamba Biblia inasema kweli kuhusu mambo mengine, kutia ndani mambo ya historia na ya unabii.

Vitu vilivyotumiwa kuumba ulimwengu vilitoka wapi?

“Mikono yangu mwenyewe imezitandaza mbingu.”​—Isaya 45:12.

MAMBO BIBLIA INASEMA:

Mungu ndiye Chanzo cha uwezo usio na mipaka ao nguvu. (Ayubu 37:23) Hilo ni jambo la maana, kwa sababu wanasayansi wamejifunza kwamba nishati ao nguvu inaweza kugeuzwa kuwa kitu. Biblia inasema kwamba Mungu yeye mwenyewe ndiye Chanzo cha ‘wingi wa nguvu zenye musukumo’ ambazo zilitokeza ulimwengu. (Isaya 40:26) Mungu anaahidi kutumia nguvu zake ili kutegemeza uumbaji wake, kwa sababu Biblia inasema hivi kuhusu jua, mwezi, na nyota: ‘Mungu anaendelea kuvisimamisha milele, mupaka wakati usio na kipimo.’​—Zaburi 148:3-6.

SABABU GANI NI LAZIMA UJUE JAMBO HILO?

Wakati fulani, Allan Sandage, mutu mwenye elimu ya nyota, alisema hivi: “Sayansi haiwezi kujibu maulizo magumu. Unapouliza sababu gani kitu hiki kiko hapa kuliko kusiwe na kitu, unaenda kinyume na sayansi.” Biblia inaeleza mambo ya uumbaji kwa njia inayopatana na sayansi lakini pia inajibu maulizo ambayo sayansi haiwezi kujibu, kwa mufano ulizo kama hili, Mungu ana kusudi gani juu ya dunia na juu ya wanadamu? *

^ Ili kupata habari zingine, soma sura ya 3 ya kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.