Hamia kwenye habari

Mungu Aliniumba kwa Kusudi Gani?

Mungu Aliniumba kwa Kusudi Gani?

Jibu la Biblia

 Mapenzi ya Mungu ni kwamba umjue Yeye vizuri, umkaribie, na kisha umpende na kumtumikia kwa moyo wako wote. (Mathayo 22:37, 38; Yakobo 4:8) Unaweza kujifunza jinsi ya kufanya mapenzi ya Mungu kwa kuchunguza maisha na mafundisho ya Yesu. (Yohana 7:16, 17) Yesu hakuongea tu kuhusu mapenzi ya Mungu—aliishi kupatana na mapenzi hayo. Kwa kweli, Yesu alisema kwamba kusudi kuu maishani mwake ni ‘kufanya, si mapenzi yake, bali mapenzi ya aliyemtuma.’—Yohana 6:38.

Je, ninahitaji ishara, maono, au mwito wa pekee ili nijue Mungu aliniumba kwa kusudi gani?

 Hapana, kwa sababu Biblia ina ujumbe wa Mungu kwa wanadamu. Ina kila kitu unachohitaji ili ‘uwe na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.’ (2 Timotheo 3:16, 17) Mungu anataka utumie Biblia pamoja na ‘nguvu zako za kufikiri’ ili ujifunze mapenzi yake.—Waroma 12:1, 2; Waefeso 5:17.

Je, kweli ninaweza kufanya mapenzi ya Mungu?

 Ndiyo, unaweza, kwa kuwa Biblia inasema hivi: “Amri za Mungu si ngumu sana kwetu.” (1 Yohana 5:3, Easy-to-Read Version) Hilo halimaanishi kwamba ni rahisi kufuata amri za Mungu kila siku. Lakini, faida unazopata ni nyingi sana zinapolinganishwa na jitihada zako. Yesu mwenyewe alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!”—Luka 11:28.