Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kukabiliana na Tatizo la Afya

Jinsi ya Kukabiliana na Tatizo la Afya

 Je, afya yako imezorota ghafla? Basi unajua jinsi tatizo la afya linavyoweza kuchosha, iwe ni la kiakili, kihisia, na kifedha. Ni nini kinachoweza kukusaidia kukabiliana nalo? Unaweza kumsaidiaje mshiriki wa familia au rafiki anayekabiliana na tatizo la afya? Ingawa Biblia si kitabu cha afya, kina kanuni zinazofaa zinazoweza kukusaidia kuvumilia tatizo lako kwa njia bora kadiri uwezavyo.

Madokezo yanayoweza kukusaidia kukabiliana na tatizo la afya

  •   Tafuta matibabu

     Biblia inasema nini: “Watu wenye afya hawahitaji daktari, lakini wagonjwa wanamhitaji.”—Mathayo 9:12.

     Matumizi: Tafuta msaada wa wataalamu wa afya ikiwa inahitajika.

     Jaribu kufanya hivi: Tafuta matibabu bora unayoweza kupata. Nyakati fulani, huenda likawa jambo la hekima kutafuta maoni ya daktari mwingine. (Methali 14:15) Waeleze madaktari hali yako waziwazi. Hakikisha unawaelewa na kwamba wanaelewa vizuri dalili za ugonjwa wako. (Methali 15:22) Jifunze kuhusu ugonjwa wako, kutia ndani matibabu mbalimbali yanayopatikana. Unapoelewa vizuri ugonjwa wako na mambo yanayohusika, utakuwa umejiandaa vizuri kihisia kukabiliana na hali yako na kufanya maamuzi mazuri kuhusu matibabu.

  •   Tunza afya yako

     Biblia inasema nini: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida.”—1 Timotheo 4:8.

     Matumizi: Ukiwa na mazoea mazuri ya kudumisha afya yako, kama vile kufanya mazoezi kwa ukawaida, utapata faida.

     Jaribu kufanya hivi: Dumisha ratiba nzuri ya kufanya mazoezi, kula chakula chenye lishe, na ulale vya kutosha. Ingawa unaweza kuwa unajaribu kukabiliana na tatizo la afya ambalo limejitokeza karibuni, wataalamu wanakubaliana kwamba ukitia jitihada kusitawisha mazoea mazuri ya kutunza afya yako, utapata faida. Bila shaka, hakikisha kwamba aina yoyote ya mazoezi utakayochagua haitadhuru afya wala matibabu unayopata.

  •   Tafuta msaada wa wengine

     Biblia inasema nini: “Rafiki wa kweli hupenda nyakati zote naye ni ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.”—Methali 17:17.

     Matumizi: Rafiki zako wanaweza kukusaidia kuvumilia hali ngumu.

     Jaribu kufanya hivi: Zungumza na rafiki unayemwamini ambaye unaweza kumweleza hisia zako. Kufanya hivyo kunaweza kukusaidia kuvumilia mkazo wa kihisia na kiakili unaotokezwa na kuzorota kwa afya yako. Huenda watu wa familia na marafiki wanataka kukusaidia katika njia nyingine, lakini labda hawajui jambo la kufanya. Kwa hiyo, waeleze waziwazi njia nzuri zaidi ambayo wanaweza kukusaidia. Uwe na matarajio halisi ya kile ambacho wanaweza kukufanyia, na sikuzote uwashukuru kwa msaada wanaokupa. Wakati uleule, ingawa marafiki wenye nia nzuri wanaweza kufanya mengi kukusaidia, huenda ukahitaji kuweka mipaka fulani. Kwa mfano, huenda ukahitaji kudhibiti ni mara ngapi na kwa muda gani wanaweza kukutembelea, ili usilemewe na jitihada zao.

  •   Dumisha mtazamo unaofaa

     Biblia inasema nini: “Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri, lakini roho iliyopondeka humfyonza mtu nguvu.”—Methali 17:22.

     Matumizi: Kudumisha mtazamo mzuri na kutarajia mema kunaweza kukusaidia kuwa mtulivu na kukabiliana vizuri na tatizo la afya lenye kuhangaisha.

     Jaribu kufanya hivi: Unapojitahidi kuzoea hali yako mpya, kazia fikira mambo unayoweza kutimiza. Epuka kujilinganisha na wengine au na jinsi hali yako ilivyokuwa kabla ya kuwa mgonjwa. (Wagalatia 6:4) Jiwekee malengo yenye usawaziko na unayoweza kufikia kwa sababu yatakusaidia kuwa na mtazamo mzuri kuhusu wakati ujao. (Methali 24:10) Wasaidie wengine kadiri hali zako zinavyokuruhusu. Furaha unayopata kwa kuwasaidia wengine inaweza kukusaidia uepuke kukazia fikira hali yako.—Matendo 20:35.

Je, Mungu atakusaidia kukabiliana na tatizo la afya?

 Biblia inaonyesha kwamba Yehova Mungu a anaweza kumsaidia mtu kukubaliana na matatizo ya afya. Ingawa hatuwezi kutazamia kuponywa kimuujiza, wale wanaomwabudu Mungu wanaweza kupata msaada wake katika njia zifuatazo:

 Amani. Yehova anaweza kumpa mtu “amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote.” (Wafilipi 4:6, 7) Amani hiyo, au utulivu wa moyoni, unaweza kumsaidia mtu asihangaike kupita kiasi. Mungu huwapa amani hiyo watu wanaomwomba na kumweleza mahangaiko yao.—1 Petro 5:7.

 Hekima. Yehova anaweza kutupa hekima ya kufanya maamuzi mazuri. (Yakobo 1:5) Mtu anaweza kupata hekima hiyo kwa kujifunza na kutumia kanuni zinazopatikana katika Biblia.

 Tumaini la wakati ujao linalotia moyo. Yehova anatuahidi kwamba wakati ujao “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24) Tumaini hilo linawasaidia watu wengi kuwa na mtazamo unaofaa licha ya kuwa na matatizo makubwa sana ya afya.—Yeremia 29:11, 12.

a Yehova ni jina la Mungu kama linavyofunuliwa katika Biblia.—Zaburi 83:18.