Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Waroma 6:23—“Mshahara wa Dhambi Ni Kifo; Lakini Zawadi Anayotoa Mungu Ni Uhai wa Milele”

Waroma 6:23—“Mshahara wa Dhambi Ni Kifo; Lakini Zawadi Anayotoa Mungu Ni Uhai wa Milele”

 “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo, lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.”—Waroma 6:23, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Mshahara wa dhambi ni kifo; lakini zawadi anayotoa Mungu ni uhai wa milele katika kuungana na Kristo Yesu, Bwana wetu.”—Waroma 6:23,, Biblia Habari Njema.

Maana ya Waroma 6:23

 Kwa maneno hayo, mtume Paulo anaeleza kwamba wanadamu wanakufa kwa sababu wana dhambi. Hata hivyo, Mungu anawapa waabudu wake waaminifu taraja lenye kupendeza sana—zawadi ya uzima wa milele.

 “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” Watu wanazaliwa wakiwa si wakamilifu na hivyo wana mwelekeo wa kutenda dhambi. a (Zaburi 51:5; Mhubiri 7:20) Kwa sababu wanadamu wanazaliwa wakiwa na dhambi, wote wanazeeka na kufa.—Waroma 5:12.

 Ili kufafanua wazo hilo, Paulo analinganisha dhambi na bwana anayelipa mshahara. Kama tu mfanyakazi anavyotarajia kulipwa kwa sababu ya kazi aliyofanya, ndivyo wanadamu wanavyotarajia kufa kwa sababu ya hali yao ya kutokamilika.

 Hata hivyo, Paulo anaeleza kwamba mtu “ambaye amekufa ameondolewa hatia ya dhambi yake.” (Waroma 6:7) Mtu anapokufa, anaachiliwa, au kuwekwa huru, kutokana na dhambi zozote ambazo ametenda. Hiyo ndiyo sababu hatupaswi kufikiri kwamba watu waliokufa wanaendelea kuteseka mahali fulani kwa sababu ya makosa waliyofanya zamani. Kwa kweli, Biblia inasema waziwazi kwamba waliokufa hawawezi kufikiri, kutenda, au kuhisi chochote.—Mhubiri 9:5.

 “Lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu.” Tofauti na “mshahara” ambao dhambi hulipa, Mungu hutoa zawadi ya uzima wa milele. Neno la awali la “zawadi” linaweza pia kutafsiriwa kuwa “zawadi isiyostahiliwa” au “zawadi ya neema.” Inarejelea kitu ambacho mtu anapewa bila kukistahili. Hakuna mwanadamu mwenye dhambi anayeweza kujipatia wokovu na uzima wa milele. (Zaburi 49:7, 8) Hata hivyo, kwa hiari Mungu anawapa bure zawadi yenye thamani sana ya uzima wa milele wote wanaomwamini Yesu.—Yohana 3:16; Waroma 5:15, 18.

Muktadha wa Waroma 6:23

 Paulo aliwaandikia Wakristo Waroma barua hii katika mwaka wa 56 W.K. hivi. Inaonekana kwamba baadhi ya Wakristo walioishi wakati huo walikuwa na maoni yasiyo sahihi kuhusu rehema za Mungu. Kwa sababu ya kuathiriwa na falsafa za Kigiriki, huenda walifikiri kwamba kadiri walivyotenda dhambi nyingi zaidi, ndivyo wangenufaika kutokana na msamaha wa Mungu. (Waroma 6:1) Huenda wengine walihisi kwamba hawangeweza kuadhibiwa kwa makosa yao kwa sababu hawakuwa tena chini ya Sheria ya Musa. (Waroma 6:15) Katika barua yake, Paulo anakazia kwamba Wakristo hawawezi kunufaika kutokana na rehema za Mungu ikiwa wataruhusu dhambi itawale maisha yao.—Waroma 6:12-14, 16.

 Maneno ya Paulo yanawahakikishia waabudu wa Mungu leo kwamba ingawa wamezaliwa wakiwa na dhambi, bado wana tumaini. Wakitii viwango vya Mungu vya maadili na kukataa kushindwa na tamaa zao mbaya, Mungu anaahidi atawapa uzima wa milele.—Waroma 6:22.

 Tazama video hii fupi inayoonyesha muhtasari wa kitabu cha Waroma.

a Katika Biblia, neno “dhambi” linarejelea tendo lolote au mtazamo ambao haupatani na viwango vya Mungu. (1 Yohana 3:4) Ona makala yenye kichwa “Dhambi Ni Nini?