Hamia kwenye habari

Unapaswa Kufanya Nini Ili Uishi Milele?

Unapaswa Kufanya Nini Ili Uishi Milele?

Jibu la Biblia

 Biblia inaahidi hivi: “Mtu atendaye atakalo Mungu, anaishi milele.” (1 Yohana 2:​17, Biblia Habari Njema) Mungu anataka ufanye nini?

  •   Jifunze kumhusu Mungu na Mwana wake, Yesu. Alipokuwa akisali kwa Mungu, Yesu alisema hivi: “Uzima wa milele ndio huu, wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Ni nini kinachohusika katika ‘kumjua’ Mungu na Yesu? Tunaweza kuwajua kwa kujifunza Biblia na kutumia ujumbe wake maishani mwetu. a Biblia inafunua kufikiri kwa Muumba wetu, Yehova Mungu, ambaye ndiye Mpaji-uhai. (Matendo 17:24, 25) Pia, Biblia inatuambia kuhusu Mwana wake, Yesu, ambaye alifundisha “maneno ya uzima wa milele.”​—Yohana 6:​67-​69.

  •   Onyesha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu. Yesu alikuja duniani “kuhudumu na kutoa uhai wake uwe fidia.” (Mathayo 20:28) Dhabihu ya fidia ya Yesu iliwafungulia wanadamu njia ya kuishi milele katika Paradiso duniani. b (Zaburi 37:29) Yesu alisema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:​16) Ona kwamba mengi zaidi yanahitajika mbali tu na kumwamini Yesu. Lazima tudhihirishe imani katika Yesu, kwa kuchagua kuishi kupatana na mafundisho yake na mapenzi ya Baba yake.​—Mathayo 7:​21; Yakobo 2:​17.

  •   Mfanye Mungu awe rafiki yako wa karibu. Mungu anataka tumkaribie na kuwa rafiki yake. (Yakobo 2:​23; 4:8) Mungu ni wa milele. Hatawahi kufa, naye anataka rafiki zake waishi milele pia. Kupitia Neno lake, Mungu anasema wazi kile ambacho anataka wale wanaomtafuta wapate: “Na ufurahie maisha milele.”​—Zaburi 22:26.

Maoni Yasiyo Sahihi Kuhusu Kuishi Milele

 Maoni yasiyo sahihi: Wanadamu watajivumbulia njia ya kuishi milele.

 Ukweli: Ingawa maendeleo fulani ya kitiba yanaonyesha kwamba huenda yakaongeza muda wa kuishi wa wanadamu, jitihada hizo haziwezi kuongoza kwenye uzima wa milele. Ni Mungu peke yake anayeweza kutupa uzima wa milele kwa kuwa yeye tu ndiye “chanzo cha uhai.” (Zaburi 36:9) Anaahidi kwamba “atameza kifo milele,” na kuwapa wanadamu wote waaminifu uzima wa milele.​—Isaya 25:8; 1 Yohana 2:​25.

 Maoni yasiyo sahihi: Ni watu wa jamii fulani tu watakaoishi milele.

 Ukweli: Mungu hana upendeleo. Tofauti na hilo, “katika kila taifa mtu anayemwogopa na kutenda uadilifu anakubaliwa naye.” (Matendo 10:34, 35) Watu wa malezi na utamaduni mbalimbali wanaomtii Mungu wanaweza kuishi milele.

 Maoni yasiyo sahihi: Kuishi milele kutachosha.

 Ukweli: Uzima wa milele unatoka kwa Mungu, ambaye anatupenda na anataka tuwe na furaha. (Yakobo 1:​17; 1 Yohana 4:8) Anajua kwamba ili tuwe na furaha, tunahitaji kuwa na kazi yenye kusudi. (Mhubiri 3:​12) Mungu anaahidi kwamba wale wanaoishi milele duniani watakuwa na kazi yenye kuridhisha na yenye kusudi ambayo itawanufaisha wao na wapendwa wao.​—Isaya 65:22, 23.

 Isitoshe, wale watakaoishi milele wataendelea kujifunza mambo mapya kumhusu Muumba wao na kazi zake nyingi za uumbaji. Aliwaumba wanadamu wakiwa na tamaa ya kuishi milele na kujifunza kumhusu, hata ingawa “hawatajua kamwe kazi ambayo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho.” (Mhubiri 3:​10, 11) Hivyo, wale watakaoishi milele hawatawahi kukosa mambo yenye kupendeza ya kufanya na kujifunza.

a Mashahidi wa Yehova wana programu ya kujifunza Biblia bila malipo. Ili upate habari zaidi, tazama video Ni Nini Hutendeka Kwenye Funzo la Biblia?

b Ona makala yenye kichwa “Yesu Huokoa​—Jinsi Gani?