Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

IGENI IMANI YAO | ENOKO

‘Alimpendeza Mungu Vema’

‘Alimpendeza Mungu Vema’

ENOKO alikuwa ameishi miaka mingi. Alikuwa na umri wa miaka 365, mara nne ya umri wa mtu aliyeishi maisha marefu sana leo. Si rahisi kwetu kuwazia mtu akiishi miaka yote hiyo! Hata hivyo, katika siku zake, Enoko hakuonekana kuwa mzee sana. Siku hizo, zaidi ya karne 50 zilizopita, watu waliishi miaka mingi sana kuliko ilivyo leo. Adamu, mwanadamu wa kwanza, alikuwa na miaka mia sita Enoko alipozaliwa, na akaishi miaka mia tatu zaidi! Baadhi ya wazao wa Adamu waliishi muda mrefu kuliko yeye. Kwa hiyo, akiwa na miaka 365, Enoko alionekana kuwa mwanamume mwenye nguvu, ambaye angeishi miaka mingi tu zaidi ya hiyo. Lakini haikuwa hivyo.

Uhai wa Enoko ulikuwa hatarini. Mwazie akikimbia, akifikiria jinsi watu walivyoitikia ujumbe wa Mungu aliokuwa amewapatia. Walikuwa wamewaka hasira. Watu hao walimchukia. Waliuchukia ujumbe wa Enoko, na walimchukia Mungu aliyemtuma. Hawangeweza kumshambulia Yehova, Mungu wa Enoko, lakini wangeweza kumshambulia yule aliyeleta ujumbe! Huenda Enoko alijiuliza ikiwa angeweza kuiona familia yake tena au la. Je, alimfikiria mke na binti zake, au mwanaye Methusela, au labda mjukuu wake aliyeitwa Lameki? (Mwanzo 5:21-23, 25) Je, huo ndio ungekuwa mwisho wa maisha yake?

Biblia haielezi mambo mengi kumhusu Enoko. Masimulizi ya Biblia yanayomtaja ni matatu tu, nayo ni mafupi. (Mwanzo 5:21-24; Waebrania 11:5; Yuda 14, 15) Hata hivyo, habari zinazopatikana kwenye mistari hiyo zinatosha kutusadikisha kwamba Enoko alikuwa mtu mwenye imani yenye nguvu. Je, wewe ni kichwa cha familia? Au je, umewahi kukabili changamoto ya kudumisha msimamo wako wa kile unachoamini kuwa sahihi? Ikiwa ndivyo, unaweza kujifunza mengi kutokana na imani ya Enoko.

“ENOKO AKAENDELEA KUTEMBEA PAMOJA NA MUNGU WA KWELI”

Enoko aliishi wakati ambao jamii ya wanadamu haikuwa na maadili. Kilikuwa ni kizazi cha saba kutoka kwa Adamu. Wanadamu walikuwa karibu sana na ukamilifu ambao Adamu na Hawa walikuwa nao lakini wakaupoteza. Hiyo ndio sababu watu waliishi miaka mingi. Ingawa hivyo, hali yao ya kiroho na kiadili ilikuwa mbaya sana. Jeuri ilikuwa imekithiri. Hali hiyo ilianzia kwenye kizazi cha pili, Kaini alipomuua ndugu yake, Abeli. Inaonekana kwamba mmoja wa wazao wa Kaini alijitutumua kwa sababu ya kuwa mwenye jeuri na mkorofi kuliko Kaini! Katika kizazi cha tatu, aina nyingine ya uovu ilitokea. Watu walianza kuliitia jina la Yehova, lakini si kwa nia ya kumwabudu. Ni wazi kwamba walikufuru jina takatifu la Mungu, na kulitumia kwa njia isiyofaa.—Mwanzo 4:8, 23-26.

Ibada hiyo iliyopotoka ilikuwa ya kawaida katika siku za Enoko. Hivyo, Enoko alipozidi kukua, alihitaji kufanya uamuzi. Je, angetenda kama watu wengine katika siku zake? Au je, angemtafuta Mungu wa kweli, Yehova, ambaye aliumba mbingu na dunia? Bila shaka, alifurahi kujifunza kumhusu Abeli, ambaye alikufa akiwa mfia imani kwa sababu ya kumtumikia Yehova kwa njia inayofaa. Enoko aliamua kuchukua msimamo kama wa Abeli. Andiko la Mwanzo 5:22 linasema hivi: “Enoko akaendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli.” Maneno hayo yanaonyesha kwamba Enoko alikuwa mtu aliyemwogopa Mungu ingawa aliishi katika ulimwengu wa watu wasiomwogopa Mungu. Enoko ni mwanadamu wa kwanza kuelezwa kwa njia hiyo katika Biblia.

Mstari huohuo wa Biblia unasema kwamba Enoko aliendelea kutembea na Yehova baada ya kumzaa Methusela. Kwa hiyo, Enoko alikuwa na familia alipokuwa na umri wa miaka 65 hivi. Alikuwa na mke, ambaye Maandiko hayataji jina lake, na pia akawa na “wana na mabinti.” Ili kichwa cha familia awe na kibali cha Mungu anapoitunza familia yake, anapaswa kufanya hivyo kwa njia ambayo Mungu anakubali. Enoko alielewa kwamba Yehova alimtazamia ashikamane kwa uaminifu na mke wake. (Mwanzo 2:24) Pia, alijitahidi kadiri alivyoweza kuwafundisha watoto wake kumhusu Yehova Mungu. Matokeo yalikuwaje?

Biblia inataja mambo machache tu kuhusu jambo hilo. Haisemi chochote kuhusu imani ya mwana wa Enoko, Methusela, ambaye aliishi muda mrefu zaidi kuliko watu wote wanaotajwa katika Biblia, na hatimaye akafa mwaka ambao Gharika ilitokea duniani. Hata hivyo, Methusela alikuwa na mwana aliyeitwa Lameki. Lameki aliishi wakati uleule na Enoko, babu yake, kwa zaidi ya miaka 100. Lameki alikuwa mtu mwenye imani. Yehova alimtumia kutoa unabii kumhusu Noa, mwana wa Lameki, na unabii huo ulitimia baada ya Gharika. Noa, kama babu yake, Enoko, alikuwa mtu pekee aliyemwogopa Mungu katika kipindi chake. Noa hakuwahi kukutana na Enoko. Lakini Enoko aliwaachia wazao wake kielelezo kizuri. Huenda Noa alijifunza kuhusu imani ya Enoko kutoka kwa baba yake, Lameki, au kutoka kwa babu yake, Methusela, au labda kutoka kwa baba ya Enoko aliyeitwa Yaredi, ambaye alikufa Noa alipokuwa na umri wa miaka 366.—Mwanzo 5:25-29; 6:9; 9:1.

Hebu fikiria tofauti iliyopo kati ya Enoko na Adamu. Ingawa Adamu alikuwa mkamilifu, alimkosea Yehova na kuwarithisha wazao wake matokeo ya uasi yaliyojaa majonzi. Enoko hakuwa mkamilifu, lakini alitembea na Mungu na kuwaachia wazao wake kielelezo cha imani. Adamu alikufa Enoko alipokuwa na umri wa miaka 308. Je, familia ya Adamu iliomboleza kifo chake ingawa alikuwa mfano mbaya? Hatujui. Vyovyote vile, Enoko “[aliendelea] kutembea pamoja na Mungu wa kweli.”—Mwanzo 5:24.

Ikiwa wewe ni kichwa cha familia, fikiria mambo unayoweza kujifunza kutokana na imani ya Enoko. Ingawa ni muhimu kuiandalia familia mahitaji ya kimwili, mahitaji ya kiroho ni muhimu hata zaidi. (1 Timotheo 5:8) Unaweza kutimiza mahitaji ya kiroho kupitia maneno na matendo yako. Ukiamua kutembea na Mungu kwa kukubali kuongozwa na viwango vyake kama Enoko, utaiachia familia yako mfano mzuri wa kuigwa ambao ni urithi wenye thamani kwelikweli.

ENOKO ‘ALITOA UNABII KUWAHUSU’

Huenda Enoko alihisi upweke kwa sababu ya kuwa mtu pekee mwenye imani katika siku zake. Lakini je, Yehova Mungu, alitambua imani yake? Ndiyo. Siku moja, Yehova aliwasiliana na Enoko, mtumishi wake mwaminifu. Alimpa ujumbe kwa ajili ya watu walioishi siku hizo. Hivyo, akamfanya Enoko kuwa nabii wa kwanza ambaye ujumbe wake umeandikwa katika Biblia. Tunajua hilo kwa kuwa karne nyingi baadaye, Yuda, ndugu wa kambo wa Yesu aliandika maneno ya kinabii ya Enoko akiongozwa na roho ya Mungu. *

Unabii wa Enoko ulisemaje? Ulisema hivi: “Tazama! Yehova alikuja pamoja na watakatifu wake makumi ya maelfu, ili kufanya hukumu juu ya wote, na kuwathibitisha kuwa ni wenye hatia wote wasiomwogopa Mungu kuhusu matendo yao yote ya kutomwogopa Mungu ambayo walitenda kwa njia ya kutomwogopa Mungu, na kuhusu mambo yote ya kushtua ambayo watenda-dhambi wasiomwogopa Mungu walisema juu yake.” (Yuda 14, 15) Jambo moja ambalo huenda umegundua ni kwamba Enoko alizungumza kwa wakati uliopita, kana kwamba Mungu tayari alikuwa amefanya kile kilichosemwa kwenye unabii huo. Manabii wengi baadaye walitumia njia hiyo walipotoa unabii wao. Wazo ni hili: Uhakika wa kutimia kwa jambo linalozungumziwa ni mkubwa sana hivi kwamba linaelezwa kana kwamba tayari limetukia!—Isaya 46:10.

Enoko alitangaza ujumbe wa Mungu katika ulimwengu wa watu wenye vichwa vigumu bila woga

Hali ilikuwaje Enoko alipokuwa akitangaza ujumbe wake, labda akimhubiria kila mtu aliyekutana naye? Hebu fikiria jinsi ambavyo onyo hilo lilikuwa kali. Maneno “wasiomwogopa Mungu” yalitumiwa mara nne ili kuelezea watu, matendo yao, na jinsi walivyofanya matendo hayo. Hivyo, unabii huo ulionyesha wazi kwamba ulimwengu wa wanadamu tangu kufukuzwa Edeni, ulikuwa umepotoka kwelikweli. Ulimwengu huo ungefikia mwisho wakati ambapo Yehova angekuja kuuharibu akiwa na “watakatifu wake makumi ya maelfu,” yaani, malaika wenye nguvu waliopangwa kivita. Enoko alitangaza onyo hilo bila woga, tena akiwa peke yake! Huenda Lameki ambaye wakati huo alikuwa mdogo, alitazama na kustaajabia ujasiri wa babu yake. Ikiwa alifanya hivyo, tunajua ni kwa nini.

Kutafakari imani ya Enoko kunatuchochea kujichunguza ikiwa tunauona ulimwengu huu kama Yehova anavyouona. Hukumu ambayo Enoko alitangaza kwa ujasiri inahusu kipindi chetu pia. Kama tu Enoko alivyotabiri, Yehova alileta Gharika katika siku za Noa ili kuangamiza watu wasiomwogopa. Uharibifu huo uliweka kielezo cha uharibifu mkubwa zaidi utakaokuja hivi karibuni. (Mathayo 24:38, 39; 2 Petro 2:4-6) Leo pia, kama ilivyokuwa katika siku za Enoko, Mungu akiwa pamoja na watakatifu wake makumi ya maelfu, anajiandaa kuleta hukumu ya uadilifu kwa ulimwengu wa watu wasiomwogopa. Sote tunapaswa kufikiria kwa uzito onyo la Enoko na kuwahubiria wengine kulihusu. Huenda familia na marafiki wasituunge mkono. Huenda nyakati nyingine tukahisi tuko peke yetu. Lakini Yehova hakumwacha Enoko kamwe; na hatawaacha watumishi wake waaminifu leo!

“ALIHAMISHWA ILI ASIONE KIFO”

Mwisho wa maisha ya Enoko ulikuwaje? Kwa kweli, kifo cha Enoko kilikuwa cha ajabu sana hata kuliko maisha yake. Simulizi lililo kwenye kitabu cha Mwanzo linasema hivi kwa ufupi: “Enoko akaendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli. Kisha, hakuwapo tena, kwa maana Mungu alimchukua.” (Mwanzo 5:24) Mungu alimchukua Enoko jinsi gani? Mtume Paulo alieleza hivi baadaye: “Kwa imani Enoko alihamishwa ili asione kifo, naye hakupatikana popote kwa sababu Mungu alikuwa amemhamisha; kwa maana kabla ya kuhamishwa kwake alikuwa ametolewa ushahidi kwamba amempendeza Mungu vema.” (Waebrania 11:5) Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba Enoko “alihamishwa ili asione kifo”? Baadhi ya tafsiri za Biblia zinasema kwamba Mungu alimchukua Enoko na kumpeleka mbinguni. Lakini jambo hilo si kweli. Biblia inaonyesha kwamba Yesu Kristo ndiye mtu wa kwanza kufufuliwa na kwenda mbinguni.—Yohana 3:13.

Kwa hiyo, inamaanisha nini kwamba Enoko “alihamishwa ili asione kifo”? Inaelekea kwamba Yehova alikatisha uhai wa Enoko na hivyo kumwepusha na kifo chenye maumivu makali. Lakini kabla ya kufa, Enoko alipokea “ushahidi kwamba amempendeza Mungu vema.” Jinsi gani? Kabla ya kifo chake, huenda Enoko alipata ono kutoka kwa Mungu lililomwonyesha dunia ikiwa Paradiso. Baada ya kuona wazi kwamba alikuwa na kibali cha Yehova, Enoko akalala usingizi katika kifo. Alipokuwa akimzungumzia Enoko pamoja na wanaume na wanawake wengine wenye imani, mtume Paulo aliandika hivi: “Katika imani hawa wote walikufa.” (Waebrania 11:13) Baada ya Enoko kufa, huenda adui zake waliutafuta mwili wake, lakini ‘haukupatikana popote.’ Inaelekea Yehova aliuharibu, na hivyo kuzuia usitumiwe vibaya, labda katika ibada ya uwongo. *

Tukiwa na wazo hilo la Kimaandiko akilini, acheni tuwazie jinsi mwisho wa maisha ya Enoko ulivyokuwa. Wazia hali hii, ukikumbuka kwamba tunajaribu tu kuwazia jinsi mambo yalivyokuwa. Enoko alikuwa anakimbia akiwa amechoka. Adui zake walikuwa wanamkimbiza wakiwa wamekasirishwa na ujumbe wake wa hukumu. Enoko akapata eneo la kujificha na kupumzika kidogo, lakini alijua kwamba hawezi kujificha kwa muda mrefu. Alikuwa karibu sana kuuawa kikatili. Alipokuwa amepumzika, alisali kwa Mungu. Kisha, akahisi utulivu wa hali ya juu. Akaanza kuona maono yaliyokuwa halisi sana kwake.

Inaelekea Enoko alikuwa karibu kuuawa kikatili Yehova alipomchukua

Mwazie Enoko akiona ulimwengu tofauti kabisa na ule alioufahamu. Ulimwengu huo ulikuwa mzuri kama bustani ya Edeni, lakini haukuwa na makerubi wanaolinda wanadamu wasiingie. Kulikuwa na wanaume na wanawake wengi, wote wakiwa wenye afya na nguvu. Amani ilitawala katikati yao. Hakukuwa na chuki na upinzani wa kidini kama ule ambao Enoko alikuwa amezoea. Enoko akapata uhakika kwamba alikuwa na kibali na anapendwa na Yehova. Akahisi kwamba alipaswa kuwa mahali hapo; makazi yake yangekuja kuwa hapo. Kadiri alivyohisi amani na utulivu, Enoko alifumba macho na kulala usingizi mzito.

Mpaka leo bado Enoko amelala usingizi katika kifo, lakini akiwa kwenye kumbukumbu ya Yehova Mungu! Kama Yesu alivyoahidi, siku moja wale wote walio kwenye kumbukumbu ya Mungu, watasikia sauti ya Kristo na kutoka kaburini, kisha, wataingia kwenye dunia mpya, inayopendeza na yenye amani tele.—Yohana 5:28, 29.

Je, ungependa kuwa katika dunia hiyo? Wazia jinsi itakavyosisimua kukutana na Enoko. Fikiria mambo yenye kupendeza tutakayojifunza kutoka kwake! Atatusimulia ikiwa mwisho wa maisha yake ulikuwa kama tulivyowazia. Lakini kuna jambo moja muhimu tunalopaswa kujifunza kutoka kwa Enoko na kulitumia katika maisha yetu leo. Baada ya kumzungumzia Enoko, Paulo alisema hivi: “Bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza [Mungu] vema.” (Waebrania 11:6) Hiyo ni sababu muhimu ya kutufanya tuige imani ya Enoko!

^ fu. 14 Baadhi ya wasomi wa Biblia wanasema kwamba Yuda alinukuu maneno hayo kutoka kwenye kitabu cha hekaya kinachoitwa Kitabu cha Enoko, ambacho kina habari za kubuniwa kumhusu Enoko. Kitabu hicho kimenukuu kwa usahihi unabii wa Enoko, lakini huenda unabii huo ulitolewa kwenye chanzo cha kale ambacho sasa hakipo kama vile nakala ya maandishi au masimulizi. Huenda Yuda alitumia chanzo hichohicho au alijifunza kuhusu Enoko kupitia Yesu ambaye aliona maisha ya Enoko kutoka Mbinguni.

^ fu. 20 Vivyo hivyo, inaelekea Mungu alihakikisha kwamba mwili wa Musa na wa Yesu hautumiwi kwa njia isiyofaa.—Kumbukumbu la Torati 34:5, 6; Luka 24:3-6; Yuda 9.