Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Mungu Hasikilizi Baadhi ya Sala?

Kwa Nini Mungu Hasikilizi Baadhi ya Sala?

Baba yetu wa mbinguni, Yehova Mungu, anapenda kusikiliza sala zinazotoka moyoni. Hata hivyo, kuna mambo yanayoweza kumfanya asisikilize sala zetu. Ni mambo gani, na tunapaswa kukumbuka nini tunaposali? Ona baadhi ya miongozo tunayopata kwenye Biblia.

“Mnaposali msiseme mambo yaleyale tena na tena.”​—Mathayo 6:7.

Yehova hataki turudie-rudie sala ambazo tumekariri au kuzisoma kutoka kwenye kitabu cha sala. Badala yake, anataka tusali kutoka moyoni. Ungehisije ikiwa una rafiki ambaye anakwambia maneno yaleyale kila siku? Marafiki wa kweli huzungumza waziwazi na kutoka moyoni. Tunaposali kwa maneno yetu wenyewe, tunamweleza Baba yetu wa mbinguni mambo yaliyo moyoni mwetu.

“Mnapoomba, hampokei kwa sababu mnaomba kwa kusudi baya.”​—Yakobo 4:3.

Tunajua kwamba Mungu hawezi kujibu sala zetu ikiwa tutamwomba mambo ambayo hayampendezi au yasiyofaa. Kwa mfano, je, Yehova anaweza kusikiliza sala ya mcheza-kamari, anayeomba bahati njema ilhali Yehova amekataza waziwazi pupa na kuamini mambo yasiyo ya kweli kama vile, bahati? (Isaya 65:11; Luka 12:15) Bila shaka, hatuwezi kutarajia Yehova ajibu sala kama hizo! Ili Mungu ajibu sala zetu, tunapaswa kuhakikisha kwamba mambo tunayomwomba yanapatana kabisa na kile anachotuambia kwenye Biblia.

“Anayekataa kusikiliza sheria​—hata sala yake inachukiza.”​—Methali 28:9.

Katika nyakati za Biblia, Mungu hakusikiliza sala za watu ambao hawakutii sheria zake. (Isaya 1:15, 16) Mungu hajabadilika. (Malaki 3:6) Ikiwa tunataka asikilize sala zetu, ni lazima tujitahidi kutii na kuishi kulingana na sheria zake. Namna gani ikiwa zamani tulifanya makosa fulani? Je, inamaanisha kwamba Yehova hatasikiliza sala zetu kamwe? Bila shaka la! Mungu atatusamehe kwa upendo ikiwa tutaonyesha kweli tunajutia mambo tuliyofanya na tunajitahidi kufanya yote tuwezayo ili kumpendeza.—Matendo 3:19.