Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unapaswa Kusali kwa Njia Gani ili Mungu Akusikilize?

Unapaswa Kusali kwa Njia Gani ili Mungu Akusikilize?

Yehova Mungu ni “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2) Tunaweza kuzungumza naye wakati wowote, mahali popote, kwa sauti au kimya-kimya. Yehova anataka tumwite “Baba”, na kwa kweli yeye ndiye Baba bora zaidi tuliye naye. (Mathayo 6:9) Kwa upendo, Yehova anatufundisha jinsi ya kusali kwake ili atusikilize.

SALI KWA YEHOVA MUNGU KUPITIA JINA LA YESU

“Mkimwomba Baba jambo lolote, atawapa katika jina langu.”​Yohana 16:23.

Maneno ya Yesu yanaonyesha wazi kwamba Yehova anataka tusali kwake na si kupitia sanamu, watakatifu, malaika, au mababu waliokufa, bali katika jina la Yesu Kristo. Tunaposali kwa Mungu kupitia jina la Yesu, tunaonyesha kwamba tunatambua jukumu muhimu la Yesu. Yesu alisema, “Hakuna mtu anayekuja kwa Baba bila kupitia kwangu.”—Yohana 14:6.

ZUNGUMZA KUTOKA MOYONI

“Mwageni mioyo yenu mbele zake.”​—Zaburi 62:8.

Tunaposali kwa Yehova, tunapaswa kuzungumza kama tunavyozungumza na baba anayetupenda. Badala ya kusoma sala zetu kutoka kwenye kitabu au kurudia-rudia sala tulizokariri, tunapaswa kuzungumza naye kwa heshima na kutoka moyoni.

SALA ZAKO ZIPATANE NA MAPENZI YA MUNGU

“Tukiomba chochote kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.”​—1 Yohana 5:14.

Kwenye Biblia, Yehova Mungu anatuambia mambo atakayotufanyia na mambo anayotaka tufanye. Ili Mungu akubali sala zetu, tunapaswa kusali “kulingana na mapenzi yake.” Tunahitaji kujifunza Biblia ili kumjua vizuri, na hilo litafanya sala zetu zimpendeze.

TUNAWEZA KUSALI KUHUSU NINI?

Sali kwa Ajili ya Mahitaji Yako. Tunaweza kumwomba Mungu mahitaji yetu ya kila siku kama vile chakula, mavazi, na mahali pa kuishi. Vilevile, tunaweza kusali ili tupate hekima itakayotuwezesha kufanya maamuzi yanayofaa na kupata nguvu za kuvumilia majaribu. Pia, tunaweza kusali ili tupate imani, tusamehewe dhambi zetu, na kumwomba Mungu msaada.​—Luka 11:3, 4, 13; Yakobo 1:5, 17.

Sali kwa Ajili ya Wengine. Wazazi wanaowapenda watoto wao hufurahi wanapoona watoto wao wanapendana pia. Sisi ni watoto wa Yehova, naye hufurahi anapoona tunapendana na kuwajali wengine. Hivyo, ni jambo linalofaa kusali kwa ajili ya mwenzi wetu wa ndoa, watoto wetu, familia yetu, na rafiki zetu. Mwanafunzi wa Yesu aliyeitwa Yakobo aliandika hivi: “[Salini] kwa ajili ya mtu na mwenzake.”​—Yakobo 5:16.

Mshukuru Mungu. Biblia inasema hivi kuhusu Muumba wetu: “Alitenda mema, akiwapa ninyi mvua kutoka mbinguni na majira ya mavuno, akiwashibisha kwa chakula na kuijaza mioyo yenu furaha.” (Matendo 14:17) Tunapofikiria mambo yote ambayo Mungu ametufanyia, tunachochewa kumshukuru. Bila shaka, tunaonyesha kwamba tunamshukuru kwa mambo aliyotufanyia kwa kumtii.​—Wakolosai 3:15.

UWE MWENYE SUBIRA NA UENDELEE KUSALI

Nyakati nyingine, tunaweza kuvunjika moyo kwa sababu Mungu hajibu haraka sala zetu zinazotoka moyoni. Je, tunapaswa kufikiri Mungu hatujali? La hasha! Fikiria masimulizi yafuatayo yanayoonyesha umuhimu wa kuendelea kusali.

Steve aliyetajwa katika makala ya kwanza anasema hivi: “Ikiwa ningeacha kusali, ningepoteza furaha kabisa maishani.” Ni nini kilichofanya abadili mtazamo wake? Alianza kujifunza Biblia na akatambua umuhimu wa kuendelea kusali bila kuacha. Steve anasema hivi: “Ninamshukuru Mungu kwa sababu ya msaada niliopokea kutoka kwa rafiki zangu wapendwa. Na sasa nina furaha zaidi.”

Namna gani kuhusu Jenny ambaye alihisi hastahili kumwomba Mungu jambo lolote? Jenny anasema hivi: “Nilipokuwa nimeshuka moyo sana nilimsihi Mungu anisaidie kuelewa kwa nini nilihisi sifai.” Kusali kwa njia hiyo kulimsaidiaje? “Kuzungumza na Mungu kulinisaidia kuwa na mtazamo wenye usawaziko kujihusu na kuona hata moyo wangu ukinihukumu, yeye hanihukumu. Vilevile, kusali kumenisaidia kutokata tamaa na kuendelea kupambana na hisia hizo.” Sala zimemsaidiaje? Jenny anaendelea kusema hivi: “Sala zimenisaidia kumwona Yehova kuwa Mungu halisi, Baba, na Rafiki mwenye upendo na anayenijali. Sikuzote atanitegemeza na kunisaidia, maadamu ninajitahidi kuendelea kufanya mambo anayotaka.”

Isabel anapoona mtoto wake akifurahia maisha, anasema hivi, “Ninatambua kwamba Yehova Mungu amejibu sala zangu kwa njia bora zaidi.”

Mfikirie pia mwanamke anayeitwa Isabel. Alipokuwa mjamzito, madaktari walimwambia kwamba mtoto wake angezaliwa akiwa na ulemavu mkubwa. Alivunjika moyo kabisa. Hata baadhi ya watu walimshauri atoe mimba. Anasema, “Nilihisi ningekufa kwa sababu ya uchungu niliokuwa nao moyoni.” Isabel alifanya nini? Anasema, “Nilisali tena na tena kwa Mungu ili anisaidie.” Baada ya muda alijifungua mtoto anayeitwa Gerard, na alikuwa na ulemavu. Je, Isabel anahisi kwamba Mungu alijibu sala zake? Ndiyo! Kwa njia gani? Isabel anasema, “Mtoto wangu ana umri wa miaka 14 na anafurahia maisha licha ya kuwa mlemavu. Yeye ni baraka kwangu. Ninatambua kwamba Yehova Mungu amejibu sala zangu kwa njia bora zaidi.”

Hisia kama hizo zinazotoka moyoni zinafanya tufikirie maneno ya mtunga-zaburi aliyesema: “Utasikia ombi la wapole, Ee Yehova. Utaiimarisha mioyo yao na kuwasikiliza kwa makini.” (Zaburi 10:17) Hizo ni sababu nzuri za kuendelea kudumu katika sala!

Kwenye Biblia, kuna sala nyingi ambazo Yesu alitoa. Sala inayojulikana zaidi ni ile aliyowafundisha wanafunzi wake. Tunaweza kujifunza nini kutokana na sala hiyo?