Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”​—Yakobo 4:8.

Je, Mungu Husikiliza Sala Zetu?

Je, Mungu Husikiliza Sala Zetu?

Je, umewahi kujiuliza ikiwa Mungu anasikiliza sala zako? Ikiwa ndivyo, hauko peke yako. Watu wengi wanamwomba Mungu aondoe matatizo yao, lakini bado matatizo yanabaki palepale. Je, hilo linamaanisha Mungu hasikilizi sala zetu? Hapana! Biblia inatuhakikishia kwamba Mungu anatusikiliza ikiwa tunasali kwake kwa njia inayofaa. Biblia inasema nini kuhusu jambo hilo?

MUNGU ANASIKILIZA.

“Ee Msikiaji wa sala, watu wa kila aina watakujia.”​—Zaburi 65:2.

Watu wengi husema kwamba wanaposali wanahisi vizuri ingawa hawaamini kwamba kuna mtu yeyote anayewasikiliza. Hata hivyo, hatusali ili tu tuhisi vizuri tunapokuwa na matatizo au mahangaiko maishani. Biblia inatuhakikishia kwamba, “Yehova * yuko karibu na wote wanaomwitia, wote wanaomwitia yeye katika ukweli. . . . Husikia kilio chao cha kuomba msaada.”​—Zaburi 145:18, 19.

Hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova Mungu husikiliza sala za waabudu wake. Kwa upendo, anasema hivi: “Nanyi mtaniita na kuja na kusali kwangu, nami nitawasikiliza.”​—Yeremia 29:12.

MUNGU ANATAKA USALI KWAKE.

“Dumuni katika sala.”​—Waroma 12:12.

Biblia inatuhimiza ‘tusali bila kuacha’ na ‘tuendelee kusali kila wakati.’ Ni wazi kwamba Yehova Mungu anataka tusali kwake.​—Mathayo 26:41; Waefeso 6:18.

Kwa nini Mungu anataka tusali kwake? Fikiria hili: Ni mzazi gani ambaye hapendi mtoto wake amwombe msaada? Inawezekana mzazi akawa anajua mambo ambayo mtoto anahitaji au jinsi anavyohisi, lakini anapomsikia akimwomba msaada, mzazi anatambua kwamba mtoto wake anamwamini na anamwona kuwa rafiki yake wa karibu. Vivyo hivyo, tunaposali kwa Yehova Mungu, tunaonyesha kwamba tunamwamini na tunataka kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye.​—Methali 15:8; Yakobo 4:8.

MUNGU ANAKUJALI.

“[Tupeni] mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.”​—1 Petro 5:7.

Mungu anataka tusali kwake kwa sababu anatupenda na kutujali. Anaelewa kikamili matatizo na mahangaiko yetu, na anataka kutusaidia.

Katika kipindi chote cha maisha yake, Mfalme Daudi alimwomba Yehova amsaidie na alimweleza hisia na mawazo yake. (Zaburi 23:1-6) Mungu alimwonaje Daudi? Mungu alimpenda na alisikiliza sala zake. (Matendo 13:22) Vivyo hivyo, Mungu anasikiliza sala zetu kwa sababu anatujali.

“NINAMPENDA YEHOVA KWA SABABU YEYE HUISIKIA SAUTI YANGU”

Hayo ni maneno ya mmoja wa waandishi wa kitabu cha Biblia cha Zaburi. Alikuwa na uhakika kwamba Mungu alisikiliza sala zake, na hilo lilimwimarisha sana. Alihisi akiwa karibu na Mungu na pia alipata nguvu za kukabiliana na mkazo na matatizo maishani.​—Zaburi 116:1-9.

Tukiwa na uhakika kwamba Mungu anasikiliza sala zetu, tutaendelea kusali kwake. Mfikirie mwanamume anayeitwa Pedro anayeishi kaskazini mwa Hispania. Mtoto wake aliyekuwa na umri wa miaka 19 alikufa kwenye aksidenti. Akiwa na huzuni nyingi, Pedro alimmiminia Mungu moyo wake, na alisali mara kwa mara ili Mungu amfariji na kumtegemeza. Matokeo yalikuwa nini? Pedro anasema: “Yehova alijibu sala zangu kupitia faraja na msaada ambao mimi na mke wangu tulipokea kutoka kwa Wakristo wenzetu.”

Mara nyingi, Mungu hujibu sala zetu kupitia faraja na msaada kutoka kwa marafiki wanaotujali

Ingawa bado walikabiliana na huzuni ya kumpoteza mtoto wao, kusali kwa Mungu kuliwasaidia sana Pedro na familia yake. Mke wake anayeitwa María Carmen anasema: “Sala zilinisaidia sana kukabiliana na huzuni yangu. Nilijua kwamba Yehova Mungu alinielewa kabisa kwa sababu niliposali nilipata amani na utulivu.”

Mambo ambayo watu wengi wamejionea maishani na masimulizi mbalimbali ya Biblia yanathibitisha kwamba Mungu anasikiliza sala zetu. Lakini, ni wazi kwamba Mungu hasikilizi baadhi ya sala. Kwa nini?

^ fu. 5 Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu.​—Zaburi 83:18.