Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuchagua Tafsiri Nzuri ya Biblia

Jinsi ya Kuchagua Tafsiri Nzuri ya Biblia

Jinsi ya Kuchagua Tafsiri Nzuri ya Biblia

BIBLIA iliandikwa mwanzoni katika lugha za kale za Kiebrania, Kiaramu, na Kigiriki. Kwa hiyo, watu wengi wanaotaka kuisoma wanategemea Biblia iliyotafsiriwa.

Leo, Biblia ndicho kitabu kilichotafsiriwa katika lugha nyingi zaidi ulimwenguni. Imetafsiriwa kwa sehemu katika lugha zaidi ya 2,400. Lugha fulani zina tafsiri nyingi sana za Biblia. Ikiwa kuna tafsiri mbalimbali katika lugha yenu, bila shaka ungependa kutumia tafsiri iliyo bora zaidi.

Ili uchague tafsiri nzuri, unahitaji kujua majibu kwa maswali yafuatayo: Kuna tafsiri gani mbalimbali? Tafsiri fulani ni bora kuliko nyingine katika njia gani? Na kwa nini unapaswa kuwa mwangalifu unaposoma tafsiri fulani za Biblia?

Zinatofautiana Kabisa

Biblia imetafsiriwa kwa njia mbalimbali, lakini kuna aina tatu kuu za tafsiri. Kwa upande mmoja, kuna tafsiri zinazoonyesha maandishi ya awali pamoja na tafsiri ya neno kwa neno.

Kwa upande mwingine, kuna tafsiri zilizofafanuliwa. Watafsiri wa Biblia hizo wanaeleza kwa maneno yao wenyewe ujumbe wa Biblia kama wanavyouelewa na kwa njia ambayo wanafikiri itavutia wasomaji wao.

Aina ya tatu ni tafsiri zenye usawaziko ambazo hazijafafanuliwa wala si za neno kwa neno. Tafsiri hizo za Biblia zinajitahidi kutokeza maana na ladha ya maneno ya lugha ya awali na wakati huohuo zinasomeka kwa urahisi.

Je, Tafsiri za Neno kwa Neno Ni Bora?

Mara nyingi tafsiri ya neno kwa neno haitokezi maana ya kila mstari wa Biblia kwa njia bora iwezekanavyo. Kwa nini? Kwa sababu kadhaa. Hapa pana sababu mbili:

1. Hakuna lugha zozote mbili ambazo zinalingana kabisa katika sarufi, maneno, na mpangilio wa sentensi. Profesa wa Kiebrania S. R. Driver anasema kwamba lugha “zinatofautiana si katika sarufi na maneno tu, bali pia . . . katika njia ambayo mawazo yanaunganishwa ili kuunda sentensi.” Watu wanaozungumza lugha tofauti wanafikiri kwa njia tofauti. “Hivyo, lugha mbalimbali zina mpangilio tofauti wa sentensi,” akaendelea kusema Profesa Driver.

Kwa kuwa hakuna lugha yoyote yenye maneno na sarufi kama za Kiebrania na Kigiriki cha Biblia, tafsiri ya neno kwa neno ya Biblia haiwezi kueleweka au hata huenda ikatoa maana isiyo sahihi. Fikiria mifano ifuatayo.

Katika barua yake kwa Waefeso, mtume Paulo alitumia usemi ambao unatafsiriwa kihalisi kuwa “katika dadu ya watu.” (Waefeso 4:14, The Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures) * Usemi huo ulihusu zoea la kuwadanganya wengi katika mchezo wa dadu au kamari. Hata hivyo, usemi huo unapotafsiriwa moja kwa moja katika lugha nyingi hauna maana yoyote. Usemi huo unapotafsiriwa kuwa “udanganyifu wa watu” unakuwa wazi zaidi na maana yake inaeleweka.

Paulo alipowaandikia Waroma, alitumia neno la Kigiriki linalomaanisha kihalisi “kwa roho kuchemka.” (Waroma 12:11, Kingdom Interlinear) Je, usemi huo unaeleweka katika lugha yenu? Kwa kweli, usemi huo unamaanisha ‘kuwaka roho.’

Katika moja ya hotuba zake maarufu, Yesu alitumia usemi ambao mara nyingi unatafsiriwa hivi: “Heri walio maskini wa roho.” (Mathayo 5:3) Lakini tafsiri ya neno kwa neno ya usemi huo haieleweki katika lugha nyingi. Katika lugha nyingine, tafsiri ya neno kwa neno hata inadokeza kwamba watu “walio maskini wa roho” hawana usawaziko wa kiakili au hawana nguvu na azimio. Hata hivyo, katika andiko hilo Yesu alikuwa akiwafundisha watu kwamba furaha inategemea kutambua kwamba wanahitaji mwongozo wa Mungu bali haitegemei kutosheleza mahitaji yao ya kimwili. (Luka 6:20) Kwa hivyo, tafsiri kama vile “wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho” au “wale wanaojua kwamba wanamhitaji Mungu” zinaonyesha maana sahihi ya usemi huo.—Mathayo 5:3; The New Testament in Modern English.

2. Maana ya neno au usemi inaweza kubadilika ikitegemea habari inayozungumziwa. Kwa mfano, neno la Kiebrania ambalo kwa kawaida linarejelea mkono wa mwanadamu linaweza kuwa na maana nyingi sana. Kwa mfano, ikitegemea habari inayozungumziwa, linaweza kumaanisha “mamlaka,” “ukunjufu wa mkono,” au “nguvu.” (2 Samweli 8:3; 1 Wafalme 10:13; Methali 18:21) Kwa kweli, katika Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kiingereza neno hilo limetafsiriwa kwa njia zaidi ya 40.

Kwa kuwa habari inaweza kuamua jinsi neno linavyotafsiriwa, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kiingereza inatumia semi karibu 16,000 ili kutafsiri maneno 5,500 ya Kigiriki cha Biblia, na inatumia semi zaidi ya 27,000 za Kiingereza ili kutafsiri maneno 8,500 hivi ya Kiebrania. * Kwa nini maneno yanatafsiriwa katika njia hizo mbalimbali? Halmashauri iliyotafsiri Biblia hiyo iliamua kwamba kutafsiri maneno hayo kwa usahihi zaidi kupatana na habari inayozungumziwa ni muhimu zaidi kuliko kutafsiri neno kwa neno. Hata hivyo, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatafsiri maneno yaleyale ya Kiebrania na Kigiriki kwa njia ileile kadiri inavyowezekana.

Ni wazi kwamba kazi ya kutafsiri Biblia inahusisha mengi zaidi ya kutafsiri tu maneno ya lugha ya awali kwa njia ileile kila mahali yanapotumiwa. Ni lazima watafsiri wachague kwa hekima maneno ambayo yanatokeza maana ya maandishi ya lugha ya awali kwa usahihi na kwa njia inayoeleweka. Kwa kuongezea, wanahitaji kuunganisha maneno na sentensi katika tafsiri yao kupatana na sheria za lugha yao.

Namna Gani Kuhusu Tafsiri Huru?

Watafsiri ambao wanatafsiri zile Biblia ambazo mara nyingi zinaitwa Biblia zilizofafanuliwa, au tafsiri huru, wanatafsiri kwa njia ambayo ni tofauti kabisa na maandishi ya lugha za awali. Jinsi gani? Huenda wakaongeza maoni yao kuhusu maana ya maandishi ya awali au wakaondoa habari fulani zilizo katika maandishi ya awali. Huenda tafsiri ambazo zimefafanuliwa zikavutia kwa sababu ni rahisi kusoma. Hata hivyo, nyakati nyingine kutafsiri kwa uhuru hivyo kunaficha au kubadili maana ya maandishi ya awali.

Fikiria jinsi Biblia moja iliyofafanuliwa inavyotafsiri ile sala maarufu ya Yesu ya mfano: “Baba yetu uliye mbinguni, funua wewe ni nani.” (Mathayo 6:9, The Message: The Bible in Contemporary Language) Tafsiri iliyo sahihi zaidi inatafsiri hivi maneno hayo ya Yesu: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.” Ona pia jinsi andiko la Yohana 17:26 lilivyotafsiriwa katika Biblia fulani. Tafsiri moja huru inasema kwamba usiku ambao Yesu alikamatwa, alisali hivi kwa Baba yake: “Nimekufanya ujulikane kwao.” (Today’s English Version) Hata hivyo, Biblia inayotafsiri kwa uaminifu zaidi sala hiyo ya Yesu, inasema hivi: “Nimewajulisha jina lako.” Je, unaona jinsi ambavyo watafsiri fulani kwa wazi wanaficha ukweli wa kwamba Mungu ana jina ambalo linapaswa kutumiwa na kuheshimiwa?

Kwa Nini Tunahitaji Kujihadhari?

Tafsiri fulani huru zinaficha viwango vya maadili vinavyokaziwa katika maandishi ya awali. Kwa mfano, tafsiri moja (The Message: The Bible in Contemporary Language) inasema hivi kwenye 1 Wakorintho 6:9, 10: “Je, hamtambui kwamba hampaswi kuishi hivi? Watu wasio haki ambao hawajali kuhusu mapenzi ya Mungu hawatajiunga katika ufalme wake. Wale wanaowatumia wengine na kutumiana vibaya, wanaoitumia na kuipotosha ngono, wanaotumia na kuiharibu dunia na kila kitu kilicho ndani yake, hawastahili kuwa raia katika ufalme wa Mungu.”

Linganisha tafsiri hiyo na tafsiri iliyo sahihi zaidi, yaani, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya: “Kwani! Je, hamjui kwamba watu wasio waadilifu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msipotoshwe. Wala waasherati, wala waabudu-sanamu, wala wazinzi, wala wanaume wanaowekwa kwa ajili ya makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume wanaolala na wanaume, wala wezi, wala watu wenye pupa, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi hawataurithi ufalme wa Mungu.” Ona kwamba mambo mengi yanayotajwa na mtume Paulo waziwazi kuhusu aina ya mwenendo tunaopaswa kuepuka hata hayatajwi katika ile tafsiri huru.

Maoni ya mtafsiri kuhusu mafundisho ya Biblia yanaweza pia kubadili maana katika tafsiri yake. Kwa mfano, Today’s English Version, ambayo kwa kawaida inaitwa Good News Bible, inasema kwamba Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake: “Ingieni kupitia lango jembamba. Kwa maana lango linaloongoza kwenye moto wa mateso ni pana na barabara inayoongoza huko ni rahisi, na kuna wengi wanaosafiri kwenye barabara hiyo.” (Mathayo 7:13) Watafsiri waliongeza neno “moto wa mateso” hata ingawa simulizi la Mathayo linasema waziwazi “uharibifu.” Kwa nini walifanya hivyo? Inaelekea kwamba walifanya hivyo kwa sababu walitaka kutetea wazo la kwamba waovu watateswa milele, hawataharibiwa. *

Kupata Tafsiri Bora

Biblia iliandikwa kwa lugha ya kila siku inayotumiwa na watu wa kawaida, kama vile wakulima, wachungaji, na wavuvi. (Nehemia 8:8, 12; Matendo 4:13) Kwa hiyo, tafsiri nzuri ya Biblia inawasaidia watu wanyoofu wa malezi yoyote yale waelewe ujumbe wake. Tafsiri bora itafanya pia mambo yafuatayo:

◗ Itatoa kwa usahihi ujumbe wa awali ambao uliandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu.—2 Timotheo 3:16.

◗ Itatafsiri maana neno kwa neno wakati inapowezekana kutafsiri kwa njia hiyo maneno na muundo wa maandishi ya awali.

◗ Itatoa maana sahihi ya neno au usemi wakati ambapo kutafsiri neno la lugha ya awali moja kwa moja kutapotosha au kuficha maana.

◗ Itatumia lugha ya kawaida, inayoeleweka kwa urahisi na inayowachochea watu kusoma.

Je, kuna tafsiri ya aina hiyo? Mamilioni ya wasomaji wa gazeti hili wanapenda kutumia Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Kwa nini? Kwa sababu wanakubaliana na njia iliyotumiwa na halmashauri iliyotafsiri Biblia hiyo, kama inavyoelezwa katika utangulizi wa toleo la kwanza la Kiingereza la Biblia hiyo: “Hatutafsiri Maandiko kwa njia ya ufafanuzi. Tangu mwanzo tumejitahidi sana kutafsiri neno kwa neno kadiri inavyowezekana, mahali ambapo Kiingereza cha kisasa kinaruhusu na mahali ambapo tafsiri ya neno kwa neno haifichi wala kupotosha maana kwa njia yoyote ile.”

Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imechapishwa ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha zaidi ya 60 na jumla ya nakala zaidi ya 145,000,000 zimechapishwa! Ikiwa inapatikana katika lugha yenu, kwa nini usiwaombe Mashahidi wa Yehova nakala na ujionee faida za tafsiri hiyo sahihi?

Wanafunzi wanyoofu wa Biblia wanataka kuelewa na kutenda kupatana na ujumbe ambao Mungu aliandika kwa mwongozo wa roho yake. Ikiwa wewe ni mmoja wao, unastahili kupata Biblia iliyo sahihi ambayo unaweza kusoma na kuelewa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Tafsiri yenye maandishi ya awali inamwezesha msomaji kuona tafsiri ya moja kwa moja ya kila neno pamoja na maneno ya lugha ya awali.

^ fu. 17 Tafsiri nyingine za Kiingereza zinatafsiri maneno yaleyale kwa njia nyingi zaidi kuliko Tafsiri ya Ulimwengu Mpya na hivyo hazina upatano.

^ fu. 25 Biblia inafundisha kwamba tunapokufa tunarudi katika mavumbi, nafsi inakufa, na hatuwi tena na mawazo au hisia. (Mwanzo 3:19; Mhubiri 9:5, 6; Ezekieli 18:4) Biblia haifundishi popote kwamba nafsi za waovu zinateseka milele katika moto wa mateso.

[Blabu katika ukurasa wa 21]

Huenda tafsiri ambazo zimefafanuliwa zikavutia kwa sababu ni rahisi kusoma. Hata hivyo, nyakati nyingine kutafsiri kwa uhuru hivyo kunaficha au kubadili maana ya maandishi ya awali

[Blabu katika ukurasa wa 22]

Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imechapishwa ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha zaidi ya 60 na jumla ya nakala zaidi ya 145,000,000 zimechapishwa!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20]

TAFSIRI YA ZAMANI ILIYOFAFANULIWA

Tafsiri huru za Biblia au zilizofafanuliwa zilianza zamani sana. Katika nyakati za zamani, Wayahudi walikusanya na kurekebisha tafsiri ambazo leo zinaitwa Targumi za Kiaramu, au tafsiri zilizofafanuliwa kabisa za Maandiko. Ingawa si tafsiri sahihi, zinaonyesha jinsi Wayahudi walivyoelewa maandiko fulani na zinawasaidia watafsiri kuelewa maana ya maandiko fulani magumu. Kwa mfano, katika Ayubu 38:7, ‘wana wa Mungu’ wanaelezwa kuwa “makundi ya malaika.” Katika Mwanzo 10:9, Targumi zinaonyesha kwamba usemi wa Kiebrania uliotumiwa kumhusu Nimrodi hauna maana nzuri, unamaanisha “kinyume cha” au “kwa kumpinga” bali haumaanishi “mbele za,” usemi ambao hauna maana mbaya. Ufafanuzi huo ulitumiwa pamoja na maandiko ya Biblia lakini haukukusudiwa kamwe uchukue mahali pa Biblia.

[Picha]

SEHEMU YA “BIBLIA POLYGLOTTA” YA WALTON, ILIYOKAMILISHWA MWAKA WA 1657 AYUBU 38:1-15

Maandishi ya Kiebrania ya Biblia (ikiwa na Tafsiri ya Interlinear ya Kilatini)

Tafsiri ya andiko hilo katika Targumi ya Kiaramu

[Picha katika ukurasa wa 19]

SEHEMU YA “THE KINGDOM INTERLINEAR TRANSLATION OF THE GREEK SCRIPTURES,” WAEFESO 4:14

Safu ya kushoto inaonyesha tafsiri ya neno kwa neno. Safu ya kulia inaonyesha tafsiri inayotegemea maana

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 18]

Background: Shrine of the Book, Israel Museum, Jerusalem