Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wafundishe Watoto Wako

Pupa Ilimfanya Gehazi Apoteze Kibali cha Mungu

Pupa Ilimfanya Gehazi Apoteze Kibali cha Mungu

JE, UMEWAHI kutamani sana kitu fulani? * Ikiwa ndivyo, wewe ni kama tu watu wengine. Lakini je, unapaswa kujaribu kupata kile unachokitamani kwa kusema uwongo?—Hapana, hupaswi kufanya hivyo. Mtu anayefanya hivyo ana pupa. Acheni tuone jinsi mwanaume aliyeitwa Gehazi alivyopoteza kibali cha Mungu kwa sababu ya pupa. Alikuwa mtumishi wa Elisha, nabii wa Mungu wa kweli, Yehova.

Elisha na Gehazi waliishi zamani sana, karibu miaka elfu moja kabla ya Mwana wa Mungu, Yesu, kuzaliwa duniani. Yehova alimtumia Elisha kufanya miujiza yenye kustaajabisha! Kwa mfano, Biblia inaeleza kuhusu mwanaume mwenye cheo katika jeshi la Siria ambaye alikuwa na ugonjwa mbaya wa ukoma. Hakuna mtu ambaye angeweza kumponya, lakini Elisha anamponya.

Mungu anapomtumia Elisha kuwaponya watu, Elisha hakubali kamwe kupokea pesa. Je, unajua ni kwa nini?— Kwa sababu Elisha anajua kwamba miujiza hiyo inatoka kwa Yehova​—na si kwake. Naamani anapoponywa na Elisha, anafurahi sana hata anataka kumpa zawadi za dhahabu, fedha, na nguo nzuri. Elisha hataki kuchukua kitu chochote lakini Gehazi anataka sana zawadi hizo.

Baada ya Naamani kuondoka, Gehazi anakimbia na kumfuata bila kumwambia Elisha. Anapompata Naamani, unajua Gehazi anamwambia nini?— ‘Elisha amenituma nikwambie kwamba wageni wawili wamekuja tu sasa hivi. Angependa kuwa na mavazi mawili ya kubadilisha ili awape hao wageni.’

Lakini huo ni uwongo! Gehazi ametunga habari kuhusu wageni wawili. Anamdanganya kwa sababu anataka kupata zile nguo ambazo Naamani alijaribu kumpa Elisha. Bila shaka, Naamani hajui jambo hilo. Kwa hiyo, anafurahia kumpa Gehazi zawadi hizo. Naamani anampa Gehazi vitu vingi zaidi ya vile alivyomwomba. Unajua ni nini kinachotokea baadaye?

Gehazi anaporudi nyumbani, Elisha anamuuliza: ‘Umetoka wapi?’

Gehazi anajibu, ‘Ah, sijatoka popote.’ Hata hivyo, Yehova amemwezesha Elisha kujua kile ambacho Gehazi amefanya. Kwa hiyo, Elisha anasema: ‘Huu si wakati wa kupokea fedha na nguo!’

Gehazi amechukua fedha na nguo ambazo si zake. Kwa hiyo Mungu anafanya ukoma wa Naamani umpate Gehazi. Unafikiri tunaweza kujifunza nini kutokana na jambo hilo?— Jambo moja tunalojifunza ni kwamba hatupaswi kutunga na kusema habari za uwongo.

Kwa nini Gehazi alitunga habari ambazo, kwa kweli, zilikuwa za uwongo?— Ni kwa sababu Gehazi alikuwa na pupa. Alitaka kupata vitu ambavyo havikuwa vyake, na alijaribu kuvipata vitu hivyo kwa kusema uwongo. Kwa sababu hiyo aliugua ugonjwa mbaya sana kwa muda wote uliobaki wa maisha yake.

Kwa kweli, Gehazi alipatwa na jambo baya sana hata kuliko ukoma. Unajua ni jambo gani hilo?— Alipoteza kibali na upendo wa Mungu. Tusifanye kamwe jambo lolote litakalosababisha tupoteze mambo hayo! Badala yake, acheni tuwe wenye fadhili na tayari kushiriki vitu tulivyo navyo.

^ fu. 3 Ikiwa unasoma sehemu hii pamoja na mtoto, unapoona kistari kama hiki (—), tua na umtie moyo mtoto atoe maoni yake.