Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Je, Mashahidi wa Yehova Wanawaruhusu Wanawake Kufundisha?

Je, Mashahidi wa Yehova Wanawaruhusu Wanawake Kufundisha?

Ndiyo, ulimwenguni pote Mashahidi wa Yehova wana mamilioni kadhaa ya wanawake wanaofundisha. Wanawake hao ni umati mkubwa wa wahubiri wa habari njema za Ufalme wa Mungu. Unabii wa Zaburi 68:11 unaohusu wahudumu hao unasema hivi: “Yehova mwenyewe anasema neno hili; wanawake wanaotangaza habari njema ni jeshi kubwa.”

Hata hivyo, usichanganye kazi ya kufundisha inayofanywa na wanawake ambao ni Mashahidi wa Yehova na huduma inayofanywa na makasisi au wachungaji wanawake walio katika dini nyingine. Kuna tofauti kubwa kati yao. Ni katika njia gani wao ni tofauti?

Watu wanaowafundisha ni tofauti. Makasisi wa kike, hasa wa dini zinazodai kuwa za Kikristo huongoza mambo ndani ya makanisa yao, na huwafundisha washiriki wote wa kanisa. Wanawake ambao ni Mashahidi wa Yehova, hufundisha watu walio nje ya kutaniko, yaani, hadharani ambako wanahubiri nyumba kwa nyumba na kwingineko.

Njia nyingine inayowatofautisha wanawake ambao ni Mashahidi wa Yehova na wale wanaofundisha katika dini nyingine ni utendaji wao ndani ya kutaniko. Makasisi wa kike wa dini zinazodai kuwa za Kikristo pamoja na wa dini nyingine huongoza na kufundisha washiriki wa makanisa yao kuamini mafundisho ya dini zao. Hata hivyo, wanawake ambao ni Mashahidi wa Yehova, hawafundishi ndani ya kutaniko ikiwa kuna wanaume waliobatizwa. Ni wanaume tu waliowekwa rasmi kuwa walimu ndio wanaofundisha.​—1 Timotheo 3:2; Yakobo 3:1.

Biblia inaeleza kwamba wanaume peke yao ndio waliopewa daraka la kusimamia kutaniko. Ona kielelezo kilichowekwa na mtume Paulo alipomwandikia mwangalizi mwenzake, Tito: “Kwa sababu hii nilikuacha wewe Krete, ili . . . uweke rasmi wanaume wazee katika jiji baada ya jiji.” Paulo aliongezea kusema kwamba kila mwanamume aliyewekwa rasmi alipaswa kuwa “asiye na shtaka, mume wa mke mmoja.” (Tito 1:5, 6) Katika barua yake ya uchungaji, Paulo alimpa Timotheo mwongozo kama huo: “Ikiwa mwanamume yeyote anajitahidi kufikia cheo cha mwangalizi, yeye anatamani kazi njema. Mwangalizi anapaswa kuwa asiyelaumika, mume wa mke mmoja, . . . mwenye sifa za kustahili kufundisha.”​—1 Timotheo 3:1, 2.

Kwa nini wanaume peke yao ndio wenye madaraka ya kusimamia kutaniko? Paulo anasema: “Simruhusu mwanamke kufundisha, wala kuwa na mamlaka juu ya mwanamume, bali kuwa kimya. Kwa maana Adamu aliumbwa kwanza, kisha Hawa.” (1 Timotheo 2:12, 13) Hivyo, utaratibu wa uumbaji unaonyesha ni kwa nini Mungu amewapa wanaume daraka la kufundisha na la kusimamia kutaniko.

Wahudumu wa Yehova wanaiga mfano wa kiongozi wao, Yesu Kristo. Mwanafunzi Luka aliandika hivi kuhusu huduma ya Yesu: “Akaanza kusafiri kutoka jiji mpaka jiji na kutoka kijiji mpaka kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.” Baadaye, Yesu aliwatuma wanafunzi wake kufanya kazi hiyohiyo: “Wakapita katika eneo hilo kutoka kijiji mpaka kijiji, wakitangaza habari njema.”​—Luka 8:1; 9:2-6.

Leo wahudumu wa Yehova​—wanaume na wanawake—​wanashiriki kwa bidii kutimiza kazi iliyotabiriwa na Yesu: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”​—Mathayo 24:14.