Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Barua zilitumwaje katika nyakati za Biblia?

Mkuu fulani wa serikali ya Uajemi anatuma barua rasmi za serikali kwa kuzipeleka kwa shirika la Kiserikali linalotoa huduma za posta. Kitabu cha Biblia cha Esta kinaeleza jinsi mfumo wa Uajemi ulivyofanya kazi: “Naye [Mordekai] akaandika kwa jina la Mfalme Ahasuero na kutia muhuri kwa pete ya mfalme na kupeleka barua kwa mkono wa wajumbe waliopanda farasi wenye kusafirisha barua wanaotumiwa katika utumishi wa kifalme, wana-farasi wenye mbio.” (Esta 8:10) Pia, Milki ya Roma ilikuwa na mfumo kama huo kwa ajili barua za usimamizi na za wanajeshi.

Barua za kibinafsi, kama vile barua zilizoandikwa na mtume Paulo au wengine, hazikustahili kutumwa kupitia mfumo huo. Ikiwa mtu alikuwa tajiri, angemtuma mtumwa wake apeleke barua hiyo. Hata hivyo, watu wengi waliwatuma rafiki zao, au hata watu wasiowajua, ambao walikuwa wakisafiri kuelekea sehemu walikotaka barua zao zipelekwe. Watu wa familia, marafiki, wanajeshi, au wafanyabiashara walitumwa wapeleke barua. Hata hivyo, hangaiko kuu lilikuwa kama mtu aliyetumwa kupeleka barua alikuwa mwenye kutegemeka na ikiwa angeweza kufikisha ujumbe kwa makini bila kuuharibu. Biblia inadokeza kwamba Paulo alituma baadhi ya barua zake kupitia Wakristo wenzake waliokuwa wakisafiri.​—Waefeso 6:21, 22; Wakolosai 4:7.

Watu waliuzaje na kununua vitu katika Israeli la kale?

Uchumi wa taifa hilo ulitegemea kilimo, ufugaji, na biashara ya kubadilishana bidhaa na huduma. Biblia hutaja masoko katika malango ya jiji, kama vile “Lango la Kondoo,” “Lango la Samaki,” na “Lango la Vigae.” (Nehemia 3:1, 3; Yeremia 19:2) Inaonekana kwamba majina hayo yalitegemea bidhaa iliyouzwa katika kila soko. Pia, Maandiko yanataja “barabara ya waokaji” iliyokuwa jijini Yerusalemu na bidhaa fulani zilizouzwa.​—Yeremia 37:21.

Vipi kuhusu bei? Kitabu kimoja kinachofafanua Biblia kinasema: “Bei zilibadilika-badilika kadiri muda ulivyopita, na ni vigumu kutambua kihususa bei ya bidhaa wakati fulani, na mahali hususa.” Hata hivyo, vyanzo vya habari, kutia ndani Biblia, vinaonyesha kwamba hata wakati huo bei za bidhaa zilipanda. Kwa mfano, zamani za kale kulikuwa na biashara ya kuuza watumwa. Yosefu aliuzwa kwa vipande 20 vya fedha, ambavyo huenda vilikuwa shekeli na labda hiyo ndiyo iliyokuwa bei ya watumwa katika karne ya 18 K.W.K. (Mwanzo 37:28) Miaka mia tatu baadaye, bei ya watumwa ilikuwa shekeli 30. (Kutoka 21:32) Kufikia karne ya nane K.W.K., bei yao ilikuwa shekeli 50. (2 Wafalme 15:20) Karne mbili baadaye, wakati wa utawala wa Waajemi, bei ilikuwa shekeli 90 au zaidi. Inaonekana kwamba tatizo la kupanda kwa bei za bidhaa limekuwepo tangu zamani.