Hamia kwenye habari

Nifanye Nini Ili Niwe Shahidi wa Yehova?

Nifanye Nini Ili Niwe Shahidi wa Yehova?

 Hatua zinazopaswa kufuatwa ili mtu awe Shahidi wa Yehova, zilielezwa na Yesu kwenye Mathayo 28:19, 20. Mistari hiyo inataja mambo ambayo mtu anapaswa kufanya ili awe mwanafunzi wa Kristo, jambo linalotia ndani kuzungumza, au kutoa ushahidi, kumhusu Yehova.

 Hatua ya 1: Jifunze yale ambayo Biblia inafundisha. Yesu aliwaamuru wafuasi wake ‘wafanye wanafunzi, na kuwafundisha.’ (Mathayo 28:19, 20) Neno linalotafsiriwa “mwanafunzi” kihalisi humaanisha “mtu anayejifunza.” Katika Biblia, hasa katika vitabu vyenye mafundisho ya Yesu Kristo, kuna habari unazohitaji ili uwe na furaha na maisha yenye kuridhisha. (2 Timotheo 3:​16, 17) Tutafurahi kukusaidia ujifunze mambo ambayo Biblia inafundisha kupitia mpango wetu wa kujifunza Biblia bila malipo.​—Mathayo 10:​7, 8; 1 Wathesalonike 2:​13.

 Hatua ya 2: Tenda kupatana na yale unayojifunza. Yesu alisema kwamba wale wote wanaojifunza wanapaswa pia ‘kushika mambo yote ambayo anawaamuru.’ (Mathayo 28:20) Hilo linamaanisha kwamba kujifunza Biblia kunahusisha mengi zaidi ya kujielimisha tu​—huenda ukahitaji kufanya mabadiliko makubwa katika mawazo na mwenendo wako. (Matendo 10:42; Waefeso 4:​22-​29; Waebrania 10:24, 25) Wale wanaotii yale ambayo Yesu aliamuru wanachochewa kufanya uamuzi wa kibinafsi wa kumfuata kwa kujitoa kumtumikia Yehova Mungu maishani mwao.​—Mathayo 16:24.

 Hatua ya 3: Ubatizwe. (Mathayo 28:19) Katika Biblia, ubatizo unafananishwa na kuzikwa. (Linganisha Waroma 6:​2-4.) Unawakilisha kufa kuhusiana na njia ya maisha ya zamani na kuanza njia mpya ya maisha. Unapobatizwa, unatangaza hadharani kwamba umetimiza hatua mbili za kwanza zilizotajwa na Yesu na unamwomba Mungu akupe dhamiri njema.​—Waebrania 9:​14; 1 Petro 3:​21.

Nitajuaje ikiwa ninastahili kubatizwa?

 Zungumza na wazee wa kutaniko. Watazungumza na wewe ili kuhakikisha ikiwa unaelewa mambo yanayohusika, ikiwa unatenda kupatana na yale uliyojifunza, na ikiwa umejiweka wakfu kwa Mungu kwa hiari.​—Matendo 20:28; 1 Petro 5:​1-3.

Je, hatua hizo zinatumika kwa watoto ambao wazazi wao ni Mashahidi?

 Ndiyo. Tunawalea watoto wetu “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova,” kama Biblia inavyoamuru. (Waefeso 6:4) Hata hivyo, wanapoendelea kukua wanapaswa kufanya uamuzi wao binafsi wa kujifunza, kukubali, na kutenda kupatana na yale ambayo Biblia inafundisha kabla ya kustahili kubatizwa. (Waroma 12:2) Hivyo, kila mtu anapaswa kujifanyia maamuzi yake binafsi kuhusiana na ibada.​—Waroma 14:12; Wagalatia 6:5.