Hamia kwenye habari

Inamaanisha Nini ‘Kumheshimu Baba Yako na Mama Yako’?

Inamaanisha Nini ‘Kumheshimu Baba Yako na Mama Yako’?

Jibu la Biblia

 Amri inayosema “mheshimu baba yako na mama yako” inapatikana mara nyingi katika Biblia. (Kutoka 20:12; Kumbukumbu la Torati 5:16; Mathayo 15:4; Waefeso 6:2, 3) Kutii amri hiyo kunahusisha kufanya mambo manne muhimu.

  1.   Wathamini. Unawaheshimu baba na mama yako unaposhukuru kwa ajili ya mambo yote ambayo wamekufanyia. Unaweza kuonyesha unawathamini kwa kutodharau mwongozo wanaotoa. (Methali 7:1, 2; 23:26) Biblia inakutia moyo uwaone wazazi wako kuwa “utukufu” wako, yaani, ujivunie kuwa nao.—Methali 17:6.

  2.   Kubali mamlaka yao. Hasa ikiwa wewe ni kijana, unaonyesha kwamba unamheshimu baba yako na mama yako unapotambua mamlaka ambayo Mungu amewapa. Wakolosai 3:20 inawaambia vijana hivi: “Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika kila jambo, kwa maana hilo humpendeza Bwana.” Hata Yesu alipokuwa kijana aliwatii wazazi wake kwa hiari.—Luka 2:51.

  3.   Watendee kwa heshima. (Mambo ya Walawi 19:3; Waebrania 12:9) Mara nyingi hilo linahusisha jambo unalosema na jinsi unavyolisema. Ni kweli kwamba nyakati fulani kuna wazazi ambao hutenda kwa njia ambayo ni vigumu kuwaheshimu. Hata hivyo, watoto wanaweza kuwaheshimu wazazi wao kwa kuepuka kuzungumza na kutenda kwa njia isiyo na heshima. (Methali 30:17) Biblia inafundisha kwamba kumtukana baba au mama yako ni kosa zito sana.—Mathayo 15:4.

  4.   Waandalie mahitaji yao. Wazazi wako wanapozeeka, huenda wakahitaji kutunzwa. Unaweza kuwaheshimu kwa kujitahidi kadiri uwezavyo kuhakikisha kwamba wanapata mahitaji yao. (1 Timotheo 5:4, 8) Kwa mfano, muda mfupi kabla ya Yesu kufa, alifanya mpango ili mama yake atunzwe.—Yohana 19:25-27.

Maoni yasiyo sahihi kuhusu kumheshimu baba na mama

 Maoni yasiyo sahihi: Ili kumheshimu baba yako na mama yako, unapaswa kuwaruhusu waiongoze ndoa yako.

 Ukweli: Biblia inafundisha kwamba kifungo cha ndoa kinapaswa kutangulizwa mbele ya uhusiano mwingine wowote wa familia. Mwanzo 2:24 inasema hivi: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake.” (Mathayo 19:4, 5) Bila shaka, wenzi wa ndoa wanaweza kunufaika kutokana na mashauri ya wazazi wao au wakwe zao. (Methali 23:22) Hata hivyo, huenda wenzi wa ndoa wakaamua kuweka mpaka unaoonyesha wazi ni masuala gani ambayo watu wa ukoo hawapaswi kujihusisha nayo katika ndoa yao.​—Mathayo 19:6.

 Maoni yasiyo sahihi: Baba yako na mama yako wana mamlaka kamili.

 Ukweli: Ingawa Mungu amewapa wazazi mamlaka katika familia, mamlaka yote ya wanadamu ina mipaka—haiwezi kuzidi mamlaka ya Mungu. Kwa mfano, mahakama kuu ilipowaamuru wanafunzi wa Yesu wasimtii Mungu, wao walijibu hivi: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.” (Matendo 5:27-29) Vivyo hivyo, watoto wanawatii wazazi wao “katika muungano na Bwana,” yaani, katika mambo yote ambayo hayapingani na sheria za Mungu.—Waefeso 6:1.

 Maoni yasiyo sahihi: Ni lazima ufuate dini ya baba yako na mama yako ili uonyeshe kwamba unawaheshimu.

 Ukweli: Biblia inatutia moyo tuyajaribu mambo tunayofundishwa tuone ikiwa ni ya kweli. (Matendo 17:11; 1 Yohana 4:1) Mtu anayefanya hivyo huenda hatimaye akachagua kufuata imani inayotofautiana na ile ya wazazi wake. Biblia inataja baadhi ya watumishi waaminifu wa Mungu ambao hawakufuata dini ya wazazi wao, kama vile Abrahamu, Ruthu, na mtume Paulo.—Yoshua 24:2, 14, 15; Ruthu 1:15, 16; Wagalatia 1:14-16, 22-24.

 Maoni yasiyo sahihi: Ili umheshimu baba yako na mama yako, unapaswa kushiriki desturi za kitamaduni za kuabudu mababu.

 Ukweli: Biblia inasema: “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.” (Luka 4:8) Mtu anayeabudu mababu zake anamchukiza Mungu. Isitoshe, Biblia inafundisha kwamba “waliokufa hawajui jambo lolote kamwe.” Hawajui wanapoabudiwa; wala hawawezi kuwasaidia au kuwadhuru walio hai.​—Mhubiri 9:5, 10; Isaya 8:19.