Hamia kwenye habari

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kutunza Wazazi Waliozeeka?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kutunza Wazazi Waliozeeka?

Jibu la Biblia

 Watoto ambao sasa ni watu wazima wana jukumu muhimu la kuhakikisha kwamba wazazi wao waliozeeka wanatunzwa. Biblia inasema watoto wanapaswa “kujifunza kutimiza wajibu wao wa kidini kwa jamaa zao wenyewe na hivyo kuwalipa wazazi wao . . . , kwani hilo ni jambo la kupendeza mbele za Mungu.” (1 Timotheo 5:4, Biblia Habari Njema) Watoto wanapohakikisha kwamba wazazi wao wanatunzwa vizuri, wanatii amri iliyo katika Biblia ya kuwaheshimu wazazi wao.—Waefeso 6:2, 3

 Biblia haitoi mwongozo hususa unaohusu kutunza wazazi wanaozeeka. Lakini inatoa mifano ya wanaume na wanawake wenye imani ambao walifanya hivyo. Pia, inatoa ushauri unaoweza kuwasaidia wale wanaotunza.

 Baadhi ya washiriki wa familia wa nyakati za Biblia waliwatunzaje wazazi wao waliozeeka?

 Walifanya hivyo kwa njia mbalimbali kwa kutegemea hali.

  •   Yosefu aliishi mbali na baba yake Yakobo aliyekuwa amezeeka. Hali ziliporuhusu, Yosefu alifanya mipango ili baba yake awe karibu naye. Kisha Yosefu akampatia baba yake makao, chakula, na ulinzi.—Mwanzo 45:9-11; 47:11, 12.

  •   Ruthu alihamia nchi ya mama mkwe wake na kufanya kazi kwa bidii ili amtunze.—Ruthu 1:16; 2:2, 17, 18, 23.

  •   Yesu, muda mfupi kabla ya kifo chake, alichagua mtu ambaye angemtunza mama yake, Maria, ambaye alikuwa mjane.—Yohana 19:26, 27. a

 Biblia inatoa ushauri gani unaoweza kuwasaidia wale wanaotunza wazazi waliozeeka?

 Biblia ina kanuni ambazo zinaweza kuwasaidia wale wanaotunza wazazi waliozeeka kukabiliana na changamoto ambazo wakati mwingine huchosha kimwili na kihisia.

  •   Waheshimu wazazi wako.

     Biblia inasema nini: “Mheshimu baba yako na mama yako.”—Kutoka 20:12.

     Kanuni hii inaweza kutumikaje? Onyesha kwamba unawaheshimu wazazi wako kwa kuwapa uhuru kadiri hali zao zinavyoruhusu. Pia, kwa kadiri inavyowezekana waruhusu wafanye uamuzi kuhusu utunzaji wanaohitaji. Wakati huo huo waonyeshe kwamba unawaheshimu kwa kufanya kwa kiasi unachoweza ili kuwasaidia.

  •   Elewa hali zao na uwe mwenye kusamehe.

     Biblia inasema nini: “Ufahamu wa mtu hakika hutuliza hasira yake, na ni fahari kwake kuachilia kosa.”—Methali 19:11

     Kanuni hii inaweza kutumikaje? Ikiwa mzazi aliyezeeka atasema jambo lisilo la fadhili au kuonyesha kwamba hathamini utunzaji wako, jiulize, ‘Ningehisije ikiwa hali zangu zingenifanya nishindwe kutimiza mambo fulani au kuniletea mikazo? Unapojaribu kuelewa hali zake na kuwa mwenye kusamehe unaweza kuepuka kufanya hali mbaya kuwa mbaya zaidi.

  •   Zungumza na wengine.

     Biblia inasema nini: “Mipango huvunjika watu wasiposhauriana, lakini mambo hufanikiwa kupitia washauri wengi.”—Methali 15:22.

     Kanuni hii inaweza kutumikaje? Fanya utafiti kuhusu jinsi ya unavyoweza kukabiliana na matatizo ya kiafya ambayo wazazi wako wanayo. Fanya uchunguzi juu ya njia za utunzaji zinazopatikana katika jamii unayoishi. Zungumza na wengine ambao wamewahi kutunza wazazi waliozeeka. Ikiwa una watu wa ukoo, fikiria kuwa na kikao cha familia kitakachozungumzia mahitaji ya wazazi wenu, yaani jinsi ya kuwatunza, na jinsi ya kugawana majukumu.

    Fikiria kukutana na familia yako ili kuzungumzia utunzaji wa wazazi waliozeeka

  •   Uwe na kiasi.

     Biblia inasema nini: “Wenye kiasi wana hekima”—Methali 11:2.

     Kanuni hii inaweza kutumikaje? Tambua mipaka yako. Kwa mfano, sisi sote hatuna muda wala nguvu nyingi sana kutimiza mambo mengi kadiri ambavyo tungependa. Kwa kawaida mipaka hiyo huathiri kile unachoweza kutimiza kwa ajili ya wazazi wako. Ukipata mkazo kwa sababu ya majukumu unayopaswa kuwatimizia wazazi wako, kwa nini usijaribu kuomba msaada kutoka kwa watu wengine wa familia au kutoka kwa wataalamu?

  •   Jitunze mwenyewe.

     Biblia inasema nini: “Hakuna mtu anayeuchukia mwili wake, bali huulisha na kuutunza.”—Waefeso 5:29.

     Kanuni hii inaweza kutumikaje? Licha ya kwamba una jukumu la kutunza wazazi wako, ni muhimu ujitunze wewe mwenyewe, na pia familia yako ikiwa umefunga ndoa. Unahitaji kula vizuri. Unahitaji kupumzika vya kutosha na kulala. (Mhubiri 4:6) Na inapowezekana unahitaji kubadilisha mazingira. Unapofanya mambo haya utakuwa na hali nzuri zaidi—kihisia, kiakili, na hata kimwili—ili uweze kuendelea kuwatunza wazazi wako.

 Je, Biblia inasema kwamba ni lazima wazazi watunzwe wakiwa nyumbani?

 Biblia haitoi mwongozo wowote hususa inapohusu kutunza wazazi wakiwa nyumbani. Baadhi ya familia huamua kuishi na wazazi wao wenye umri mkubwa nyumbani kwao kwa muda mrefu kwa kadiri inavyowezekana. Lakini inapofikia hatua fulani wanaona wanahitaji msaada kutoka kwa makao ya kuwatunzia wazee. Watu wa familia wanaweza kukutana na kujadiliana ikiwa hilo ndilo jambo litakalofaa watu wote.—Wagalatia 6:4, 5.

a Kuhusiana na simulizi hili, kitabu kimoja kinachofafanua Biblia kinasema hivi: “Inawezekana Yosefu [mume wake Maria] alikuwa amekufa muda mrefu uliopita, hivyoYesu alimtegemeza mama yake, na kwa kuwa sasa muda wake wa kufa ulikuwa umefika mama yake angeishije?. . .Kupitia jambo hilo Yesu aliwafundisha watoto wawafariji wazazi wao waliozeeka.”—Kitabu The NIV Matthew Henry Commentary in One Volume, ukurasa 428-429.