Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

JINSI MZIZI WA TATIZO UTAKAVYONG’OLEWA KIKAMILI

Wakati Huo “Amani Itakuwa Nyingi”

Wakati Huo “Amani Itakuwa Nyingi”

Hivi karibuni, serikali iliyosimamishwa na Mungu, yaani, Ufalme wa Mungu ambao tumekuwa tukiusubiri kwa muda mrefu, italeta amani na umoja duniani pote. Andiko la Zaburi 72:7 linaahidi kwamba, wakati huo “amani itakuwa nyingi.” Lakini Ufalme wa Mungu utaanza kutawala lini? Utachukua mamlaka jinsi gani? Na utawala huo utakunufaishaje?

UFALME WA MUNGU UTAANZA KUTAWALA LINI?

Biblia ilitabiri matukio ya kushtua ambayo yangeonyesha kwamba Ufalme wa Mungu umekaribia. Kwa pamoja, matukio hayo ndio ile “ishara” iliyotabiriwa, na yanatia ndani vita vinavyohusisha mataifa kadhaa, njaa, magonjwa, matetemeko mengi ya ardhi, na kuongezeka kwa uasi sheria.—Mathayo 24:3, 7, 12; Luka 21:11; Ufunuo 6:2-8.

Unabii mwingine unasema: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, . . . wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, . . . waliojaa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.” (2 Timotheo 3:1-4) Sikuzote, sifa za aina hii zimekuwepo kwa kiasi fulani. Lakini siku hizi zinaonekana waziwazi kila mahali.

Mambo hayo yaliyotabiriwa yalianza kutukia mwaka wa 1914. Wanahistoria, wanasiasa, na waandishi mbalimbali wameeleza jinsi ulimwengu ulivyobadilika tangu mwaka huo. Kwa mfano, Peter Munch, mwanahistoria kutoka Denmark, aliandika: “Vita vilivyotokea mwaka wa 1914 vilibadili kabisa maisha ya wanadamu. Badala ya maendeleo yaliyokuwa yameanza kushamiri, . . . tuliingia kipindi kilichojaa majanga, hofu, chuki, na ukosefu wa usalama kila mahali.”

Kwa upande mwingine, matukio hayo ni kama dhoruba inayotokea kabla hali hazijawa shwari. Ni ishara ya kwamba Ufalme wa Mungu uko karibu kuanza kutawala duniani. Isitoshe, Yesu alipokuwa akitaja ishara ya siku za mwisho, alisema hivi pia: “Na hii habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.

Habari hiyo njema ndio ujumbe wa msingi ambao Mashahidi wa Yehova wanatangaza. Na hata kichwa cha chapisho lao kuu ni: Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova. Kwa kawaida huzungumzia mambo mazuri ambayo Ufalme wa Mungu utawafanyia wanadamu na jinsi utakavyoiboresha dunia.

UFALME WA MUNGU UTACHUKUA MAMLAKA JINSI GANI?

Kuna mambo manne tunayojua kwa hakika:

  1. Ufalme huo hautawakilishwa wala kutawala kwa kutumia viongozi wa kisiasa waliopo leo.

  2. Viongozi wa kisiasa watajaribu kung’ang’ania mamlaka na kwa njia hiyo kupinga utawala wa Ufalme wa Mungu.—Zaburi 2:2-9.

  3. Ufalme wa Mungu utalazimika kuharibu serikali za kisiasa ambazo zinataka kuendelea kuwatawala wanadamu. (Danieli 2:44; Ufunuo 19:17-21) Vita hivyo vya mwisho vitakavyohusisha dunia nzima vinaitwa Har–Magedoni.—Ufunuo 16:14, 16.

  4. Wakati wa vita vya Har–Magedoni, Mungu atawaokoa wale wote watakaokuwa tayari kujitiisha chini ya Ufalme wake, nao watafurahia maisha kwenye ulimwengu mpya uliojaa amani. Hao ndio “umati mkubwa” unaotajwa kwenye Biblia, ambao inaelekea idadi yake itakuwa mamilioni ya watu.—Ufunuo 7:9, 10, 13, 14.

UFALME WA MUNGU UTAKUNUFAISHAJE?

Ili kuwa raia wa Ufalme wa Mungu, hatua ya kwanza ambayo mtu anapaswa kuchukua ni kupata elimu. Ndio sababu Yesu alisema hivi alipokuwa akisali kwa Mungu: “Uzima wa milele ndio huu, wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.

Kuna faida nyingi sana ambazo mtu hupata baada ya kumjua Yehova Mungu vizuri. Fikiria faida mbili: Kwanza, utasitawisha imani yenye nguvu kwa Mungu. Imani hiyo ambayo inategemea mambo yaliyothibitishwa, itafanya usadiki kwamba Ufalme wa Mungu ni halisi na uko karibu kuanza kutawala. (Waebrania 11:1) Pili, upendo wako kwa Mungu na jirani utaongezeka. Kumpenda Mungu kutakuchochea umtii kwa hiari. Kumpenda jirani kutakuchochea utumie kanuni ya msingi ambayo Yesu alifundisha. Inasema: “Kama vile mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni vivyo hivyo.”—Luka 6:31.

Kama baba mwenye upendo, Muumba wetu anataka tuwe na maisha bora kabisa. Biblia huyaita maisha hayo “uzima ulio wa kweli.” (1 Timotheo 6:19) Maisha hayo ni tofauti kabisa na tunayoishi leo. Kwa mamilioni ya watu, maisha ni magumu sana na wanahangaika kupata mahitaji yao. Ili upate picha ya jinsi “uzima ulio wa kweli” ulivyo, tafadhali chunguza baadhi ya mambo mazuri ambayo Ufalme wa Mungu utawafanyia raia wake.

Ufalme wa Mungu utakapokuwa ukitawala, watu wataishi kwa amani na usalama na watakuwa na chakula tele