Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia​—Kwa Nini Ziko Nyingi?

Biblia​—Kwa Nini Ziko Nyingi?

Kwa nini leo kuna matoleo au tafsiri nyingi tofauti-tofauti za Biblia? Je, unaona tafsiri hizo kuwa msaada ama kizuizi cha kuielewa Biblia? Kujifunza historia ya tafsiri za Biblia kutakusaidia uwe na maoni yanayofaa kuzihusu.

Hata hivyo, ni nani walioandika Biblia, na waliiandika lini?

BIBLIA YA AWALI KABISA

Kwa kawaida, Biblia imegawanyika katika sehemu mbili. Sehemu ya kwanza ina vitabu 39 vyenye “maneno matakatifu ya Mungu.” (Waroma 3:2) Mungu aliwaongoza wanaume waaminifu kuandika vitabu hivyo kwa kipindi kirefu cha miaka 1,100 hivi, kuanzia mwaka wa 1513 K.W.K. hadi wakati fulani baada ya mwaka wa 443 K.W.K. Wengi wao waliandika kwa lugha ya Kiebrania, ndio sababu vitabu hivyo huitwa Maandiko ya Kiebrania, na pia vinajulikana kuwa Agano la Kale.

Sehemu ya pili ina vitabu 27 ambavyo pia ni “neno la Mungu.” (1 Wathesalonike 2:13) Mungu aliwaongoza wanafunzi waaminifu wa Yesu Kristo kuandika vitabu hivyo kwa kipindi kifupi zaidi cha karibu miaka 60, kuanzia mwaka wa 41 W.K. hivi hadi 98 W.K. Wengi wao waliandika kwa lugha ya Kigiriki, ndio sababu vitabu hivyo huitwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, na pia vinajulikana kuwa Agano Jipya.

Kwa pamoja vitabu hivyo 66 vilivyoongozwa na roho ya Mungu vinafanyiza Biblia—ujumbe wa Mungu kwa wanadamu. Lakini kwa nini tafsiri nyingine za Biblia zilitokezwa? Angalau kuna sababu tatu za msingi.

  • Ili kuwawezesha watu wasome Biblia katika lugha zao.

  • Ili kuondoa makosa yaliyofanywa na wanakili na hivyo kurudisha maneno ya awali ya Biblia.

  • Ili kuboresha lugha iliyotumika.

Acheni tufikirie jinsi sababu hizo zilivyohusika katika tafsiri mbili za awali.

SEPTUAJINTI YA KIGIRIKI

Karibu miaka 300 kabla ya siku za Yesu, wasomi Wayahudi walianza kutafsiri Maandiko ya Kiebrania katika lugha ya Kigiriki. Tafsiri hiyo ilikuja kujulikana kama Septuajinti ya Kigiriki. Kwa nini ilitokezwa? Ili kuwasaidia Wayahudi wengi ambao wakati huo walizungumza Kigiriki badala ya Kiebrania waelewe “maandishi matakatifu.”—2 Timotheo 3:15.

Septuajinti pia iliwasaidia mamilioni ya watu ambao hawakuwa Wayahudi, lakini walizungumza Kigiriki, wajifunze mafundisho ya Biblia. Jinsi gani? Profesa W. F. Howard anasema hivi: “Katikati ya karne ya kwanza, [Septuajinti] ilikuwa Biblia kwa ajili ya Kanisa la Kikristo, ambalo wamishonari wake walitembelea sinagogi moja baada ya jingine ‘wakithibitisha kwa kutumia maandiko kwamba Yesu alikuwa ndiye Masihi.’” (Matendo 17:3, 4; 20:20) Kulingana na msomi wa Biblia F. F. Bruce, hiyo ni moja ya sababu zilizofanya Wayahudi wengi “waache kupendezwa na Septuajinti.”

Wanafunzi wa Yesu walipoendelea kupata vitabu vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, waliviunganisha pamoja na toleo la Septuajinti la Maandiko ya Kiebrania, na hivyo kufanyiza Biblia nzima tuliyo nayo leo.

VULGATE YA KILATINI

Miaka 300 hivi baada ya Biblia kukamilika, msomi wa kidini, Jerome, alitoa tafsiri ya Kilatini ya Biblia, ambayo baadaye iliitwa Vulgate ya Kilatini. Kwa kuwa tafsiri mbalimbali za Kilatini tayari zilikuwepo, kwa nini tafsiri mpya ilihitajika? Kitabu The International Standard Bible Encyclopedia kinasema kwamba Jerome alitaka kurekebisha “habari ambazo hazikutafsiriwa kwa usahihi, makosa ya waziwazi, na maneno yaliyoongezwa au kuondolewa kimakosa.”

Jerome alirekebisha makosa mengi kati ya hayo. Lakini baada ya muda, viongozi wa kanisa walifanya uamuzi ambao ungekuwa na madhara zaidi! Waliitangaza Vulgate ya Kilatini kuwa tafsiri pekee ya Biblia inayokubaliwa na wakadumisha msimamo huo kwa karne nyingi! Hatua kwa hatua lugha ya Kilatini ilififia na watu wengi hawakuielewa. Hivyo, badala ya kuwasaidia watu wa kawaida kuielewa Biblia, Vulgate iliifanya kuwa kitabu kisichoeleweka.

TAFSIRI MPYA ZAONGOZEKA

Wakati huohuo, watu waliendelea kutokeza tafsiri nyingine za Biblia, kama vile tafsiri maarufu sana inayoitwa Peshitta ya Kisiria, iliyotolewa karibu karne ya tano W.K. Lakini, tangu wakati huo, hakukuwa na jitihada zozote za kuhakikisha watu wengi wa kawaida wanapata Biblia katika lugha zao, hadi kufikia karne ya 14.

Nchini Uingereza, mwishoni mwa karne ya 14, John Wycliffe alianza kazi ya kuwatoa watu kwenye utumwa wa lugha isiyoeleweka, kwa kutokeza Biblia katika Kiingereza, lugha ambayo watu wengi katika eneo lake waliielewa. Muda mfupi baadaye, mbinu ya uchapishaji iliyovumbuliwa na Johannes Gutenberg, iliongeza kasi ya wasomi wengi wa Biblia kuchapisha na kugawanya matoleo mapya ya Biblia katika lugha mbalimbali zilizozungumzwa barani Ulaya.

Tafsiri mpya za Kiingereza zilipoongezeka, baadhi ya watu walidai hakuna haja ya kuwa na matoleo mbalimbali ya lugha ileile. Kasisi Mwingereza aliyeishi karne ya 18, John Lewis, aliandika: “Lugha huzeeka na kuacha kutumika, hivyo kuna uhitaji wa kupitia upya Tafsiri za zamani na kuziboresha ili ziwe na Lugha ambayo inatumiwa, na kufanya zieleweke kwa watu wa kizazi kilichopo.”

Leo, wasomi wa Biblia wana fursa nzuri zaidi ya kupitia upya tafsiri za zamani. Wanaelewa vizuri zaidi lugha za kale zilizotumiwa kuandika Biblia, na wana hati muhimu sana za kale ambazo zimepatikana hivi karibuni. Hati hizo huwasaidia kutambua kwa usahihi zaidi maneno ya awali ya Biblia.

Hivyo, kuna faida kubwa ya kuwa na matoleo mapya ya Biblia. Ni kweli kwamba, kuna baadhi ya tafsiri za Biblia ambazo si nzuri. * Lakini ikiwa wale wanaotoa toleo jipya la Biblia wamechochewa na upendo wa kweli kwa Mungu, toleo lao linaweza kutusaidia sana.

 

^ fu. 24 Soma makala “Jinsi ya Kuchagua Tafsiri Nzuri ya Biblia” katika toleo la Mei 1, 2008, la gazeti hili.