Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Biblia Inavyoweza Kukusaidia Kuwa Mstahimilivu

Jinsi Biblia Inavyoweza Kukusaidia Kuwa Mstahimilivu

 Amani inaweza kupatikana tu ikiwa watu watakuwa na ustahimilivu.”—Azimio la Kanuni za Uvumilivu la UNESCO, 1995.

 Kwa upande mwingine, kutokuwa wastahimilivu kunaweza kutokeza ukosefu wa heshima na hata chuki. Mara nyingi hisia hizo huongezeka na kutokeza matusi, ubaguzi, na jeuri.

 Watu wana maoni mbalimbali kuhusu maana ya ustahimilivu. Wengine hufikiri kwamba watu wastahimilivu lazima wakubaliane na tabia na za aina zote. Wengine wana maoni yanayopatikana katika Biblia kwamba mtu mstahimilivu anaheshimu haki ya kila mtu ya kuchagua viwango na itikadi zake mwenyewe, hata kama yeye wenyewe hakubaliani na viwango na itikadi hizo.

 Je, Biblia inaweza kuwasaidia watu kuwa wastahimilivu kikweli katika ulimwengu huu wa sasa?

Msingi wa Biblia wa kusitawisha ustahimilivu

 Biblia hututia moyo tuwe wastahimilivu. Inasema hivi: “Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.” (Wafilipi 4:5) Biblia inatutia moyo tuwatendee wengine kwa ufikirio, adabu, bila ubaguzi. Wale wanaotumia ushauri huo huenda wasikubaliane au kuishi kulingana na viwango vya mtu mwingine, lakini wanamruhusu mtu huyo kuishi kulingana na viwango alivyochagua mwenyewe.

 Hata hivyo, Biblia inaonyesha wazi kwamba Mungu amewawekea wanadamu viwango vya kufuata. Inasema hivi: “Ee mwanadamu, [Mungu] amekuambia yaliyo mema.” (Mika 6:8) Biblia inaonyesha mwongozo ambao Mungu amewapa wanadamu utakaowasaidia kuishi maisha bora kabisa.​—Isaya 48:17, 18.

 Mungu hajatupa mamlaka ya kuwahukumu wengine. Kulingana na Biblia, “Kuna mmoja tu ambaye ni Mpaji-sheria na Mwamuzi . . . Wewe ni nani ili umhukumu jirani yako?” (Yakobo 4:12) Mungu amempa kila mmoja wetu uhuru wa kufanya maamuzi yake mwenyewe na kuwajibika kwa sababu ya maamuzi hayo.​—Kumbukumbu la Torati 30:19.

Kile ambacho Biblia inasema kuhusu heshima

 Biblia inasema ‘tuwaheshimu watu wa namna zote.’ (1 Petro 2:17) Kwa hiyo, wale wanaochagua kuishi kulingana na viwango vya Biblia wanawatendea watu wote kwa heshima, bila kujali itikadi zao au mtindo wao wa maisha. (Luka 6:31) Hilo halimaanishi kwamba wale wanaofuata Biblia wanakubaliana na imani au maoni yote ya watu wengine au kwamba wanaunga mkono maamuzi yote yanayofanywa na wengine. Lakini badala ya kutenda kwa jeuri au bila heshima, wanajaribu sana kuiga jinsi Yesu alivyowatendea wengine.

 Kwa mfano, wakati mmoja Yesu alikutana na mwanamke ambaye alikuwa wa dini ambayo hakukubaliana nayo. Mwanamke huyo pia alikuwa akiishi na mwanamume ambaye hakuwa mume wake. Yesu hakukubaliana na maisha hayo. Lakini, Yesu aliongea na mwanamke huyo kwa heshima.​—Yohana 4:9, 17-24.

 Kama Yesu, Wakristo wako tayari kuwaeleza watu wanaotaka kusikiliza sababu za imani yao, lakini wanafanya hivyo kwa “heshima kubwa.” (1 Petro 3:15) Biblia inawaagiza Wakristo wasiwalazimishe wengine wakubali maoni yao. Inasema kwamba mfuasi wa Kristo “hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote,” kutia ndani wale walio na imani tofauti.​—2 Timotheo 2:24.

Kile ambacho Biblia inasema kuhusu chuki

 Biblia inatuambia ‘tufuatilie amani pamoja na watu wote.’ (Waebrania12:14) Mtu anayefuatilia amani hukataa chuki. Ingawa hatafanya chochote kinachopingana na viwango vyake, yeye hujitahidi kuishi na wengine kwa amani. (Mathayo 5:9) Kwa kweli, Biblia inawatia moyo Wakristo kuwapenda adui zao kwa kuwatendea kwa fadhili wale wanaowatendea vibaya.​—Mathayo 5:44.

 Ni kweli kwamba Biblia inasema Mungu ‘huchukia’ au ‘huchukizwa’ na matendo yanayovunjia wengine heshima au yanayowaumiza wengine. (Methali 6:16-19) Lakini hapa Biblia inatumia neno “chukia” kufafanua hisia yenye nguvu ya kutopenda matendo maovu. Biblia inaonyesha kwamba Mungu yuko tayari kusamehe na kuwasaidia watu wanaotaka kubadili njia zao na kuishi kupatana na viwango vyake.​—Isaya 55:7.

Mistari ya Biblia inayohusiana na ustahimilivu na heshima

 Tito 3:2: ‘Uwe na usawaziko, ukionyesha upole wote kwa watu wote.’

 Mtu mwenye usawaziko anapokabili maoni tofauti, yeye hutenda kwa upole na kuwasaidia watu kuheshimiana.

 Mathayo 7:12: “Basi, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima ninyi pia mwatendee vivyo hivyo.”

 Sisi sote tunathamini wengine wanapotuheshimu na wanapoonyesha kwamba wanajali maoni na hisia zetu. Ili ujifunze jinsi ya kutumia amri hiyo ambayo Yesu alifundisha, ona makala yenye kichwa “Ile Kanuni Bora Inamaanisha Nini?

 Yoshua 24:15: “Chagueni leo yule mtakayemtumikia.”

 Tunapoheshimu haki ya wengine kufanya maamuzi yao wenyewe, tunaendeleza amani.

 Matendo 10:34: “Mungu hana ubaguzi.”

 Mungu hambagui yeyote kulingana na utamaduni wake, jinsia, taifa, jamii, au malezi. Wale wanaotaka kumwiga Mungu wanawaonyesha heshima watu wote.

 Habakuki 1:12, 13: “[Mungu hawezi] kuvumilia uovu.”

 Uvumilivu wa Mungu una mipaka. Hatawaruhusu wanadamu waendelee kutenda maovu milele. Ili ujifunze zaidi, tazama video Kwa Nini Mungu Anaruhusu Kuteseka?

 Waroma 12:19: “Iachieni nafasi ghadhabu [ya Mungu]; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa,’ asema Yehova.” a

 Yehova hajamruhusu mtu yeyote alipize kisasi. Atahakikisha kwamba haki inatekelezwa kwa wakati wake mwenyewe. Ili ujifunze habari zaidi, soma makala “Je, Kilio cha Haki Kitasikika?

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala “Yehova Ni Nani?