Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA TATU

“Baba ya Wale Wote Walio na Imani”

“Baba ya Wale Wote Walio na Imani”

1, 2. Mambo yalikuwa yamebadilikaje duniani tangu siku za Noa, na Abramu alihisije?

ABRAMU, aliutazama mnara mrefu uliokuwa huko Uru, mji wa nyumbani kwao. * Kulikuwa na kelele za watu na moshi kwenye mnara huo. Makuhani wa mungu-mwezi walikuwa wakitoa dhabihu tena. Mwazie Abramu akigeuka na kutikisa kichwa, huku uso wake ukiwa umekunjamana. Akiwa njiani kuelekea nyumbani, huenda alifikiria ibada ya sanamu iliyoenea huko Uru. Ibada hiyo haramu ilikuwa imeenea sana duniani tangu siku za Noa!

2 Noa alikufa miaka miwili tu kabla Abramu hajazaliwa. Noa na familia yake walipotoka katika safina baada ya ile Gharika kubwa, mzee huyo wa ukoo alimtolea Yehova Mungu dhabihu, naye Mungu akatokeza upinde wa mvua angani. (Mwa. 8:20; 9:12-14) Wakati huo, watu wote walimwabudu Yehova. Lakini sasa, kizazi cha kumi kutoka kwa Noa kilipokuwa kikienea duniani, watu wachache tu ndio waliomwabudu Yehova. Kila mahali, watu walikuwa wakiabudu miungu ya kipagani. Hata Tera, baba ya Abrahamu alijihusisha na ibada ya sanamu, labda alikuwa mtengeneza-sanamu.​—Yos. 24:2.

Ni nini kilichomsaidia Abramu kuwa na imani yenye nguvu?

3. Abramu alipoendelea kuzeeka, alisitawisha sifa gani, na tunajifunza nini kutoka kwake?

3 Abramu alikuwa tofauti. Na alipoendelea kuzeeka, alizidi kuwa tofauti kwa sababu ya imani yake. Hata baadaye, mtume Paulo aliongozwa na roho kumwita “baba ya wale wote walio na imani”! (Soma Waroma 4:11.) Acheni tuone kilichomsaidia Abramu kuwa na imani yenye nguvu. Hilo litatusaidia kuona jinsi tunavyoweza kusitawisha imani thabiti.

Kumtumikia Yehova Baada ya Gharika

4, 5. Huenda Abramu alijifunza kumhusu Yehova kutoka kwa nani, na kwa nini tuseme hivyo?

4 Abramu alijifunzaje kumhusu Yehova Mungu? Tunajua kwamba siku hizo Yehova alikuwa na watumishi waaminifu duniani. Shemu ni mmoja wao. Ingawa hakuwa mzaliwa wa kwanza kati ya wana watatu wa Noa, mara nyingi ndiye anayetajwa kwanza. Inaelekea ni kwa sababu Shemu alikuwa na imani yenye nguvu. * Muda fulani baada ya Gharika, Noa alimwita Yehova “Mungu wa Shemu.” (Mwa. 9:26) Shemu alimheshimu Yehova na pia ibada safi.

5 Je, Abramu alimjua Shemu? Inawezekana alimjua. Mwazie Abramu akiwa mvulana. Bila shaka alisisimka sana alipotambua kulikuwa na mtu wa ukoo wao ambaye alikuwa ameishi kwa miaka zaidi ya 400. Shemu alikuwa ameona uovu uliokuwepo kabla ya ile Gharika kuu ambayo iliondoa uovu duniani, kutokezwa kwa taifa jipya huku wanadamu wakiongezeka duniani, na siku za uasi wa Nimrodi kwenye ule Mnara mkuu wa Babeli. Shemu mwaminifu alijitenga na uasi huo, hivyo, Mungu alipovuruga lugha ya wajenzi wa mnara huo, Shemu na familia yao waliendelea kuzungumza lugha iliyozungumzwa na wanadamu mwanzoni, lugha ya Noa. Familia hiyo ilitia ndani Abramu. Ni wazi kwamba Abramu alimheshimu sana Shemu. Zaidi ya hayo, Shemu alikuwa hai kwa kipindi kirefu cha maisha ya Abramu. Hivyo, huenda Abramu alijifunza kumhusu Yehova kutoka kwa Shemu.

Abramu alijitenga na ibada ya sanamu iliyoenea sana huko Uru

6. (a) Abramu alionyeshaje kwamba alielewa sababu iliyomfanya Yehova alete ile Gharika kuu? (b) Abramu na Sarai waliishi maisha ya aina gani?

6 Abramu alielewa vizuri sababu iliyofanya Yehova alete Gharika. Alijitahidi kutembea na Mungu kama Noa alivyofanya. Hiyo ndiyo sababu iliyomfanya Abramu aepuke ibada ya sanamu na akawa tofauti na wakaaji wa Uru, labda hata alijitenga na watu wa familia yake. Hata hivyo, baadaye alipata mke aliyemfaa sana. Alimwoa Sarai, mwanamke aliyekuwa bora sana si kwa urembo tu bali pia kwa imani yake katika Yehova! * Ingawa hawakuwa na mtoto, wenzi hao wa ndoa walipata shangwe nyingi kwa kumtumikia Yehova pamoja. Pia, walimlea Loti, mpwa wa Abramu, aliyekuwa yatima.

7. Wafuasi wa Yesu wanapaswa kumwiga Abramu katika njia gani?

7 Abramu hakumwacha kamwe Yehova na kuabudu sanamu za Uru. Yeye na Sarai walikuwa tayari kujitenga na waabudu hao wa sanamu. Ili tusitawishe imani ya kweli, tunapaswa kuwa na mtazamo kama huo. Ni lazima sisi pia tuwe tayari kuwa tofauti. Yesu alisema kwamba wafuasi wake hawangekuwa “sehemu ya ulimwengu” na hivyo ulimwengu ungewachukia. (Soma Yohana 15:19.) Ikiwa utakataliwa na familia yako au na watu wengine kwa sababu ya kuamua kumtumikia Yehova, kumbuka kwamba wengine pia walitendewa hivyo. Unaiga mfano wa Abramu na Sarai ambao pia walimtumikia Mungu kwa uaminifu.

“Toka Katika Nchi Yako”

8, 9. (a) Abramu alijionea jambo gani la kustaajabisha? (b) Yehova alimpa Abramu ujumbe gani?

8 Siku moja, Abramu alijionea jambo la kustaajabisha. Alipokea ujumbe kutoka kwa Yehova Mungu! Biblia haisemi mengi kuhusu tukio hilo, lakini inasema kwamba “Mungu wa utukufu” alimtokea mwanamume huyo mwaminifu. (Soma Matendo 7:2, 3.) Labda kupitia malaika, Abramu alijionea utukufu mwingi wa Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote. Tunaweza tu kuwazia jinsi Abramu alivyosisimka kuona tofauti kati ya Mungu aliye hai na sanamu zisizo hai ambazo ziliabudiwa na watu siku hizo.

9 Yehova alimpa Abramu ujumbe gani? “Toka katika nchi yako na kutoka kwa watu wa jamaa yako na uje mpaka katika nchi ambayo nitakuonyesha.” Yehova hakutaja kihususa nchi hiyo, alisema tu kwamba angemwonyesha Abramu. Hata hivyo, kwanza Abramu angelazimika kuacha nchi yake na watu wake wa ukoo. Katika tamaduni za kale huko Mashariki ya Kati, familia zilionwa kuwa muhimu sana. Ikiwa mtu angeondoka na kuacha watu wake wa ukoo lilionwa kuwa jambo baya, na kwa wengine lilikuwa baya kuliko kifo!

10. Kwa nini huenda ilikuwa vigumu kwa Abramu na Sarai kuacha makao yao huko Uru?

10 Haikuwa rahisi kwa Abramu kuacha maisha aliyozoea. Inaelekea Uru lilikuwa jiji lenye shughuli nyingi na utajiri. (Ona sanduku “ “Jiji Ambalo Abramu na Sarai Waliacha.”) Wachimbaji wa vitu vya kale wamegundua kwamba katika Uru la kale, kulikuwa na nyumba zenye kustarehesha; nyingine zilikuwa na vyumba 12 au zaidi kwa ajili ya familia na watumishi, vilivyokuwa vimepangwa kando ya ua wa ndani. Kulikuwa pia na maji safi, vyoo, na mifumo ya kuondoa taka. Pia, kumbuka kwamba Abramu na Sarai hawakuwa vijana; inaelekea Abramu alikuwa na umri uliozidi miaka sabini, naye Sarai zaidi ya miaka sitini. Bila shaka, Abramu alitaka Sarai aishi maisha ya starehe na atunzwe vizuri, jambo ambalo mume mzuri angemtakia mkewe. Wazia wakiulizana maswali na kuzungumzia wasiwasi wao kuhusu mgawo huo. Kwa kweli, Abramu alifurahi sana Sarai alipokubali mabadiliko hayo! Kama yeye, alikuwa tayari kuacha nyumba na maisha ya starehe.

11, 12. (a) Ni matayarisho na maamuzi gani yaliyohitaji kufanywa kabla ya kuondoka Uru? (b) Eleza mambo yalivyokuwa siku ya kuondoka ilipofika.

11 Baada ya kufanya uamuzi, Abramu na Sarai walikuwa na kazi nyingi. Walipaswa kufunga mizigo na kuipanga. Wangebeba nini kwenye safari ambayo hawakujua mwisho wake, na wangeacha nini? Hata hivyo, jambo muhimu zaidi lilikuwa watu wao wa ukoo. Nani angemtunza Tera aliyezeeka? Waliamua kwenda naye na kumtunza njiani. Huenda Tera alikubali bila kusita, kwa kuwa simulizi hilo linasema aliondoka pamoja na familia yake huko Uru. Inaonekana alikuwa ameacha kuabudu sanamu. Pia, Loti mpwa wa Abramu aliondoka pamoja nao.—Mwa. 11:31.

12 Mwishowe siku ya kuondoka ikafika. Wazia msafara huo ukikusanyika nje ya kuta za jiji la Uru. Ngamia na punda walikuwa wamepakiwa mizigo, mifugo ilikuwa imekusanywa, washiriki wa familia na watumishi walikuwa tayari kuondoka, na wote walikuwa na msisimko. * Labda wote walimtazama Abramu, wakisubiri atoe amri ya kuondoka. Hatimaye safari ikaanza, wakaondoka na kuacha jiji la Uru na hawangerudi kamwe.

13. Leo, watumishi wengi wa Yehova wanaonyeshaje mtazamo kama wa Abramu na Sarai?

13 Leo, watumishi wengi wa Yehova wanaamua kuhamia maeneo yaliyo na uhitaji wa wahubiri wa Ufalme. Wengine wameamua kujifunza lugha mpya ili wapanue huduma yao. Au wanaamua kujaribu njia mpya za kuhubiri ambazo hawajazoea. Kwa kawaida, ili mtu afanye maamuzi kama hayo anahitaji kujidhabihu, awe tayari kuacha starehe fulani za kimwili. Wanastahili kupongezwa kwa kuwa na mtazamo huo, na kwa kufanya hivyo wanamwiga Abramu na Sarai! Tukiwa na imani kama hiyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atatubariki sana. Hakosi kamwe kuwathawabisha watu wenye imani. (Ebr. 6:10; 11:6) Je, alimbariki Abramu?

Kuvuka Mto Efrati

14, 15. Safari ya kutoka Uru kwenda Harani ilikuwaje, na huenda ni kwa nini Abramu aliamua kukaa Harani kwa muda?

14 Baada ya muda, ule msafara ukazoea safari. Tunaweza kumwazia Abramu na Sarai wakisafiri juu ya mnyama au wakitembea na kuzungumza huku sauti za kengele zilizofungwa kwenye shingo za wanyama zikisikika. Hatua kwa hatua, wasafiri hao wasio na uzoefu wakazoea kujenga na kuvunja kambi huku wakimsaidia Tera aliyezeeka aketi vizuri juu ya ngamia au punda. Walisafiri kandokando ya Mto Efrati kuelekea kaskazini-magharibi. Siku baada ya siku, juma baada ya juma, waliendelea kusafiri polepole.

15 Mwishowe, baada ya kusafiri kilomita 960 hivi, walifika Harani, jiji lenye ufanisi lililokuwa kwenye makutano ya barabara za kibiashara kutoka Mashariki kwenda Magharibi. Familia hiyo ilisimama ilipofika huko, na wakakaa kwa muda fulani. Labda Tera alikuwa mnyonge sana asiweze kuendelea na safari.

16, 17. (a) Abramu alitiwa moyo na ahadi gani? (b) Yehova alimbarikije Abramu alipokuwa Harani?

16 Baada ya muda, Tera akafa akiwa na umri wa miaka 205. (Mwa. 11:32) Abramu alifarijiwa sana wakati huo alipopokea tena ujumbe kutoka kwa Yehova. Alirudia maagizo aliyokuwa ametoa huko Uru, na akaongezea ahadi nyingine. Abramu angekuwa “taifa kubwa,” na familia zote duniani zingebarikiwa kwa sababu yake. (Soma Mwanzo 12:2, 3.) Akiwa ametiwa moyo na agano hilo kati yake na Mungu, Abramu alichochewa kuendelea na safari.

17 Hata hivyo, wakati huo walikuwa na mizigo mingi zaidi, kwa sababu Yehova alikuwa amembariki Abramu alipokuwa Harani. Simulizi hilo linataja “mali zote ambazo walikuwa wamekusanya na nafsi ambazo walikuwa wamejipatia katika Harani.” (Mwa. 12:5) Ili awe taifa, Abramu angehitaji mali nyingi na watumishi, yaani, familia kubwa. Yehova hafanyi watumishi wake wawe matajiri kila mara, lakini huwapa vitu wanavyohitaji ili kutimiza kusudi lake. Akiwa ametiwa moyo, Abramu aliongoza msafara ule kwenda kusikojulikana.

Haikuwa rahisi kwa Abramu na Sarai kuacha maisha ya starehe huko Uru

18. (a) Ni wakati gani ambapo Abramu alifikia hatua muhimu katika historia ya utendaji kati ya Mungu na watu Wake? (b) Baadaye ni matukio gani mengine muhimu ambayo yalikumbukwa Nisani 14? (Ona sanduku “ Tarehe Muhimu Katika Historia ya Biblia.”)

18 Mwendo wa siku kadhaa kutoka Harani kulikuwa na mji wa Karkemishi, ambapo kwa kawaida wasafiri walivuka Mto Efrati. Labda, hapo ndipo Abramu alipofikia hatua muhimu katika historia ya utendaji kati ya Mungu na wanadamu. Inaelekea Abramu aliongoza msafara wake kuvuka mtu huo mwaka wa 1943 K.W.K., siku ya 14 ya mwezi ambao baadaye uliitwa Nisani. (Kut. 12:40-43) Upande wa kusini kulikuwa na eneo kubwa ambalo Yehova alikuwa ameahidi kumwonyesha Abramu. Siku hiyo, agano kati ya Mungu na Abramu lilianza kufanya kazi.

19. Mungu alitaja nini katika ahadi yake kwa Abramu, na huenda Abramu alikumbuka nini?

19 Abramu alipoelekea kusini katika nchi hiyo, msafara wake ulisimama karibu na miti mikubwa ya More, karibu na Shekemu. Akiwa huko, Abramu alipokea tena ujumbe kutoka kwa Yehova. Wakati huu, ahadi ya Mungu ilitia ndani uzao, au wazao, ambao wangeimiliki nchi hiyo. Je, Abramu alikumbuka unabii ambao Yehova alitoa katika Edeni, uliotaja “uzao,” au mzao, ambaye siku moja angewakomboa wanadamu? (Mwa. 3:15; 12:7) Labda aliukumbuka. Huenda alianza kuelewa kwamba angehusika katika kutimizwa kwa kusudi hilo kuu la Yehova.

20. Abramu alionyeshaje kwamba alithamini pendeleo alilopewa na Mungu?

20 Abramu alithamini sana pendeleo alilopewa na Yehova. Alipoendelea na safari, bila shaka akiwa mwenye tahadhari, kwa kuwa bado nchi hiyo ilimilikiwa na Wakanaani, Abramu alisimama na kumjengea Yehova madhabahu, kwanza karibu na mti mkubwa wa More, kisha karibu na Betheli. Aliliitia jina la Yehova, na inaelekea alimshukuru Mungu kutoka moyoni alipofikiria wakati ujao wa wazao wake. Huenda pia aliwahubiria Wakanaani waliokuwa jirani zake. (Soma Mwanzo 12:7, 8.) Bila shaka, baadaye Abramu angekabili majaribu makubwa ya imani. Kwa hekima, Abramu hakufikiria nyumba na starehe alizokuwa ameacha huko Uru. Alikazia fikira wakati ujao. Andiko la Waebrania 11:10 linasema hivi kumhusu Abramu: “Alikuwa akingojea jiji lililo na misingi ya kweli, ambalo mjenzi na mtengenezaji wa jiji hilo ni Mungu.”

21. Tofauti na Abramu tunajua mambo gani kuhusu Ufalme wa Mungu, na umeazimia kufanya nini?

21 Leo, sisi tunaomtumikia Yehova tunajua mengi zaidi kuliko Abramu kuhusu jiji hilo la mfano, yaani, Ufalme wa Mungu. Tunajua kwamba Ufalme huo unatawala mbinguni na hivi karibuni utaondoa mfumo wa mambo wa ulimwengu huu, na tunajua kwamba sasa Yesu Kristo, Uzao wa Abramu ulioahidiwa, ndiye mfalme wa Ufalme huo. Litakuwa pendeleo kama nini kuishi wakati ambapo Abramu atafufuliwa na mwishowe aelewe jinsi kusudi la Mungu lilivyotimizwa! Je, ungependa kuona Yehova akitimiza ahadi zake zote? Ikiwa ndivyo, jitahidi kabisa kumwiga Abramu. Uwe na mtazamo wa kujidhabihu, uwe mtiifu, na uendelee kumshukuru Yehova kwa sababu ya mapendeleo ambayo anakupatia. Ukiiga imani ya Abramu, “baba ya wale wote walio na imani,” atakuwa pia baba yako!

^ fu. 1 Miaka mingi baadaye, Mungu alibadili jina la Abramu na kuwa Abrahamu, linalomaanisha “Baba ya Umati.”—Mwa. 17:5.

^ fu. 4 Vivyo hivyo, Abramu anatajwa kwanza kati ya wana wa Tera, ingawa hakuwa mzaliwa wa kwanza.

^ fu. 6 Baadaye, Mungu alibadili jina la Sarai kuwa Sara, linalomaanisha “Binti mfalme.”—Mwa. 17:15.

^ fu. 12 Wasomi fulani wanatilia shaka kama ngamia walifugwa siku za Abramu. Hata hivyo, maoni yao hayana msingi. Biblia inataja mara kadhaa kwamba Abramu alikuwa na ngamia.—Mwa. 12:16; 24:35.