Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA NNE

Alijifunza Kuwa Mwenye Rehema

Alijifunza Kuwa Mwenye Rehema

1. Yona alihitaji kufunga safari ya aina gani, na alihisije kuhusu jiji la Ninawi?

YONA alitumia muda mwingi sana kufikiri. Alihitaji kusafiri zaidi ya kilomita 800, mwendo ambao ungechukua mwezi mmoja au zaidi kwa miguu. Kwanza alihitaji kuamua ikiwa angepitia njia ndefu zilizokuwa salama au njia fupi zilizokuwa hatari, kisha avuke mabonde na milima mingi sana. Ilimbidi kupita kandokando ya Jangwa kuu la Siria, kuvuka mito kama vile mto mkubwa Efrati, na kuomba mahali pa kulala kwa watu asiowajua katika miji na vijiji vya Siria, Mesopotamia, na Ashuru. Aliposafiri alifikiria jiji aliloogopa sana la Ninawi, na kila alipopiga hatua alilikaribia jiji hilo.

2. Yona alijifunzaje kwamba hangeweza kuukimbia mgawo wake?

2 Yona alijua jambo moja hakika: Hangeweza kugeuka na kukimbia mgawo huu. Alikuwa amejaribu kutoroka bila mafanikio. Kama tulivyoona katika sura iliyotangulia, kwa subira Yehova alimfundisha Yona akitumia dhoruba baharini na kumwokoa kimuujiza akitumia samaki mkubwa. Siku tatu baadaye Yona alitapikwa ufuoni, akiwa amestaajabu na kunyenyekezwa.​—Yona, sura ya 1, 2.

3. Yehova alimtendeaje Yona, na ni maswali gani yanayozuka?

3 Yehova alipomwamuru Yona mara ya pili aende Ninawi, nabii huyo alitii na akafunga safari hiyo ndefu kuelekea upande wa mashariki. (Soma Yona 3:1-3.) Hata hivyo, je, alikuwa amebadili mtazamo wake baada ya kutiwa nidhamu na Yehova? Ona kwamba Yehova alikuwa amemwonyesha rehema kwa kumwokoa asife maji, kutomwadhibu alipoasi, na kumpa nafasi nyingine ya kutimiza mgawo wake. Baada ya hayo yote, je, Yona alijifunza kuwaonyesha wengine rehema? Mara nyingi ni vigumu kwa wanadamu wasio wakamilifu kujifunza jinsi ya kuonyesha rehema. Acheni tuone mambo tunayoweza kujifunza kutoka kwa Yona.

Ujumbe wa Hukumu na Itikio Lisilotarajiwa

4, 5. Kwa nini Yehova aliliita Ninawi “jiji kubwa,” na hilo linatufunza nini kumhusu?

4 Yona hakuwa na maoni kama ya Yehova kuhusu Ninawi. Tunasoma hivi: “Ninawi lilikuwa jiji kubwa kwa Mungu.” (Yona 3:3) Mara tatu, simulizi la Yona linasema kwamba Yehova aliliita “Ninawi lile jiji kubwa.” (Yona 1:2; 3:2; 4:11) Kwa nini jiji hilo lilikuwa kubwa, au muhimu, kwa Yehova?

5 Ninawi lilikuwa jiji la kale, mojawapo ya majiji ya kwanza ambayo Nimrodi alijenga baada ya Gharika. Eneo la Ninawi lilikuwa kubwa na lenye majiji kadhaa, na ilimbidi mtu atembee siku tatu ili kuvuka kutoka upande mmoja hadi mwingine. (Mwa. 10:11; Yona 3:3) Inaonekana Ninawi lilikuwa jiji lenye kupendeza, lenye mahekalu ya kifahari, kuta imara, na majengo mengineyo. Lakini mambo hayo hayakufanya jiji hilo liwe muhimu kwa Yehova Mungu. Alipendezwa hasa na watu. Ninawi lilikuwa na watu wengi wakati huo. Licha ya uovu wa watu hao, Yehova aliwajali. Anathamini uhai wa wanadamu na anaona kwamba kila mtu anaweza kutubu na kujifunza kufanya mema.

Yona alitambua kwamba Ninawi lilikuwa jiji kubwa lililojaa uovu

6. (a) Kwa nini huenda Yona aliogopeshwa na jiji la Ninawi? (Ona pia maelezo ya chini.) (b) Tunajifunza nini kumhusu Yona kutokana na kazi aliyofanya ya kuhubiri?

6 Mwishowe Yona alipofika Ninawi, huenda aliogopa sana kwa sababu ya wakaaji zaidi ya 120,000 wa jiji hilo. * Alitembea kwa siku moja, na kuingia ndani zaidi ya jiji hilo kubwa, labda akitafuta mahali panapofaa ili kuanza kutangaza ujumbe wake. Angewasilianaje na watu hao? Je, alikuwa amejifunza kuzungumza lugha ya Waashuru? Au, je, Yehova alimpa uwezo huo kimuujiza? Hatujui. Huenda Yona alitangaza ujumbe wake katika Kiebrania na akatumia mtafsiri ili awaeleze Waninawi. Vyovyote vile, ujumbe wake ulikuwa rahisi na ungefanya achukiwe na watu: “Bado siku 40 tu, na Ninawi litaangamizwa.” (Yona 3:4) Alisema kwa ujasiri na akarudia tena na tena. Kwa kufanya hivyo, alionyesha imani na ujasiri mkubwa, sifa ambazo Wakristo wanahitaji leo kuliko wakati mwingine wowote.

Ujumbe wa Yona ulikuwa rahisi na ungefanya achukiwe na watu

7, 8. (a) Watu wa Ninawi waliitikiaje ujumbe wa Yona? (b) Mfalme wa Ninawi alitendaje aliposikia ujumbe wa Yona?

7 Waninawi walisikiliza ujumbe wa Yona. Huenda alifikiri kwamba watu wangekuwa wajeuri na wenye uhasama. Badala yake, jambo la kushangaza lilitukia. Watu walisikiliza na kutii! Ujumbe wake ulienea haraka. Muda si muda, jiji lote lilikuwa likizungumzia unabii wa hukumu wa Yona. (Soma Yona 3:5.) Kila mtu alitubu, awe tajiri au maskini, mwenye nguvu au dhaifu, na mdogo kwa mkubwa. Wakafunga kula. Punde si punde, mfalme alisikia kwamba watu walikuwa wakitubu.

Yona alihitaji imani na ujasiri ili kuhubiri huko Ninawi

8 Mfalme pia alitubu aliposikia ujumbe wa Yona. Aliinuka kutoka kwenye kiti chake cha ufalme, akavua mavazi yake ya kifahari, akavaa nguo za magunia ambazo watu wake walikuwa wamevaa, na hata ‘akaketi katika majivu.’ Akiwa pamoja na “wakubwa” au wakuu, mfalme alitoa agizo rasmi la kufunga, ingawa tayari watu walikuwa wameanza kufunga. Aliamuru watu wote, kutia ndani wanyama wa kufugwa wavae nguo za magunia. * Kwa unyenyekevu, alikiri watu wake walikuwa na hatia ya kutenda mabaya na jeuri. Akionyesha kwamba alitumaini Mungu wa kweli angewaonyesha rehema kwa vile walitubu, mfalme alisema: ‘Huenda Mungu wa kweli atageuka na kuacha hasira yake inayowaka, tusije tukaangamia.’​—Yona 3:6-9.

9. Wachambuzi wamesema nini kuhusu Waninawi, na tunajuaje kwamba hawasemi ukweli?

9 Wachambuzi fulani wanadai kwamba Waninawi hawangegeuka na kutubu haraka hivyo. Hata hivyo, wasomi wa Biblia wanasema kwamba nyakati za kale kwa kawaida watu kama hao waliopenda ushirikina walibadili maoni yao haraka. Zaidi ya hayo, tunajua wachambuzi hao hawasemi ukweli kwa sababu baadaye Yesu Kristo alisema Waninawi walitubu. (Soma Mathayo 12:41.) Yesu alikuwa na uhakika kwa sababu alikuwa mbinguni na alijionea mambo hayo yalipotukia. (Yoh. 8:57, 58) Kwa kweli, hatupaswi kamwe kukata kauli kwamba watu hawawezi kutubu, hata wakionekana kuwa wakatili sana. Ni Yehova tu anayeweza kusoma yaliyo moyoni mwa mwanadamu.

Tofauti Kati ya Rehema ya Mungu na Wanadamu Wasiosamehe

10, 11. (a) Yehova alitendaje Waninawi walipotubu? (b) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova hakuwa ametangaza ujumbe wa hukumu kimakosa?

10 Yehova alitendaje Waninawi walipotubu? Baadaye Yona aliandika hivi: “Mungu wa kweli akaona matendo yao, kwamba walikuwa wamegeuka kutoka katika njia yao mbaya; naye Mungu wa kweli akajuta juu ya msiba ambao alikuwa amesema ataleta juu yao; naye hakuuleta.”​—Yona 3:10.

11 Je, hilo linamaanisha kwamba Yehova alikuwa ametangaza kimakosa hukumu juu ya Ninawi? La. Biblia inasema Yehova ni mwenye haki kabisa. (Soma Kumbukumbu la Torati 32:4.) Yehova aliacha kuwakasirikia Waninawi. Aliona jinsi walivyobadilika na akaona kwamba hawakustahili kuadhibiwa kama alivyokusudia. Huu ulikuwa wakati wa Mungu kuonyesha rehema.

12, 13. (a) Yehova anaonyeshaje kwamba ni mwenye rehema, usawaziko, na yuko tayari kubadili maoni? (b) Kwa nini unabii wa Yona haukuwa wa uwongo?

12 Yehova si Mungu mshupavu, asiyejali, na mkatili kama anavyofafanuliwa na viongozi wa kidini. Badala yake, ni mwenye usawaziko, rehema, na yuko tayari kubadili maoni. Anapoamua kuwaadhibu waovu, kwanza yeye hutumia wawakilishi wake duniani kutoa onyo, kwa sababu anatamani kuona waovu wakifanya kama Waninawi, yaani, kutubu na kubadili njia zao. (Eze. 33:11) Yehova alimwambia nabii wake Yeremia hivi: “Wakati wowote nikisema juu ya taifa na juu ya ufalme ili kuung’oa na kuubomoa na kuuharibu, na kwa kweli taifa lile ligeuke kutoka katika ubaya wake ambao nilisema juu yake, mimi pia nitajuta juu ya ule msiba niliokuwa nimefikiria kuutimiza juu yake.”​—Yer. 18:7, 8.

Mungu anatamani kuona waovu wakitubu na kubadili njia zao kama Waninawi walivyofanya

13 Je, unabii wa Yona ulikuwa wa uwongo? Hapana; ulitimiza kusudi la kuwaonya watu. Onyo hilo lilitolewa kwa sababu ya uovu wa Waninawi, ambao sasa walikuwa wamegeuka. Ikiwa Waninawi wangerudia mazoea yao maovu, Mungu angewaangamiza. Na ndivyo alivyofanya baadaye.​—Sef. 2:13-15.

14. Yona alitendaje Yehova alipowaonyesha Waninawi rehema?

14 Yona alitendaje uharibifu ulipokosa kuja wakati aliotarajia? Tunasoma hivi: “Hata hivyo, jambo hilo halikumpendeza Yona hata kidogo, naye akawaka hasira.” (Yona 4:1) Yona alisali kwa njia inayosikika kana kwamba alikuwa akimkosoa Mweza-Yote! Yona alisema kwamba afadhali angekaa nyumbani, katika nchi ya kwao. Alidai kwamba alijua Yehova hangewaletea Waninawi msiba, na kwamba hiyo ndiyo sababu iliyofanya akimbilie Tarshishi mwanzoni. Kisha akaomba afe, akisema kwamba afadhali afe kuliko kuwa hai.​—Soma Yona 4:2, 3.

15. (a) Nini kilichomfanya Yona ajisikitikie? (b) Yehova alishughulikaje na nabii wake aliyekuwa akiteseka?

15 Ni nini kilichomhangaisha Yona? Hatujui alichokuwa akifikiria, lakini tunajua Yona alikuwa amewatangazia watu hao wote kwamba Ninawi lingeangamizwa. Walikuwa wamemwamini. Na sasa, hawangeangamizwa. Je, aliogopa kudhihakiwa au kuitwa nabii wa uwongo? Vyovyote vile, hakufurahi watu walipotubu au Yehova alipowaonyesha rehema. Badala yake, inaonekana alijisikitikia na kuhisi kwamba jina lake limechafuliwa. Hata hivyo, bado Mungu mwenye rehema alikazia fikira sifa nzuri za Yona aliyekuwa akitaabika. Badala ya kumwadhibu Yona kwa kukosa heshima, Yehova alimwuliza kwa upole swali moja ili kumsaidia afikiri: “Je, umewaka hasira kwa haki?” (Yona 4:4) Yona alijibuje? Biblia haisemi.

16. Huenda wengine wasikubaliane na Mungu kuhusu mambo gani, na tunajifunza nini kutokana na Yona?

16 Ni rahisi kukosoa matendo ya Yona, lakini ni vizuri kukumbuka kwamba ni kawaida kwa wanadamu wasio wakamilifu kutokubaliana na Mungu. Huenda wengine walitazamia kwamba Yehova angezuia msiba fulani au angeondoa haraka watu waovu au kwamba tayari anapaswa kuwa ameangamiza mfumo huu wa mambo. Mfano wa Yona unatukumbusha kwamba tusipokubaliana na maoni ya Yehova Mungu, sikuzote maoni yetu ndiyo yanayopaswa kurekebishwa, bali si yake.

Yehova Alimfundishaje Yona Kuonyesha Rehema?

17, 18. (a) Yona alifanya nini baada ya kuondoka Ninawi? (b) Miujiza ya Yehova iliyohusisha mtango ilimwathirije Yona?

17 Nabii huyo aliyevunjika moyo aliondoka Ninawi, na badala ya kwenda nyumbani alielekea upande wa mashariki ambako kulikuwa na milima fulani. Alijenga kibanda kidogo, akaketi ili angoje na kuona kitakachopata jiji la Ninawi. Labda bado alitumaini kuona jiji hilo likiangamizwa. Yehova angemfundishaje mtu huyu asiyesamehe jinsi ya kuonyesha rehema?

18 Usiku, Yehova akafanya mtango umee. Yona alipoamka, aliona mmea huo uliositawi vizuri na uliompa kivuli bora kuliko alichopata katika kibanda chake duni. Akafurahi sana. “Yona akaanza kushangilia sana” kwa sababu ya mmea huo, huenda aliona muujiza huo kuwa ishara ya baraka na kibali cha Mungu. Hata hivyo, Yehova hakutaka tu kumwepusha Yona na joto wala hakutaka kumfanya aache kukasirika. Alitaka kugusa moyo wa Yona. Hivyo, Mungu akafanya miujiza mingine. Alimtuma mdudu aharibu mmea huo. Kisha akaleta “upepo wenye kukausha wa mashariki” mpaka Yona akaanza ‘kuzimia’ kwa sababu ya joto. Yona akavunjika moyo tena na akatamani kufa.​—Yona 4:6-8.

19, 20. Yehova alisema nini alipozungumza na Yona kuhusu ule mtango?

19 Yehova akamwuliza tena Yona kama alikuwa na haki ya kukasirika, wakati huu kwa sababu ya kuharibiwa kwa mtango. Badala ya kutubu, Yona alijitetea na kusema: ‘Ni kwa haki mimi nimewaka hasira, kiasi cha kufa.’ Sasa wakati ulikuwa umefika wa Yehova kumfundisha Yona somo.​—Yona 4:9.

Mungu alitumia mtango ili kumfundisha Yona jinsi ya kuonyesha rehema

20 Mungu alizungumza na Yona na kumwambia nabii huyo kwamba alikuwa anasikitikia mmea tu ambao ulisitawi usiku mmoja, na ambao Yona hakuwa ameupanda wala kuukuza. Kisha Mungu akamalizia hivi: “Kwa upande wangu, je, sipaswi kusikitikia Ninawi lile jiji kubwa, ambalo lina wanadamu zaidi ya 120,000 wasiojua hata kidogo tofauti kati ya mkono wao wa kuume na wa kushoto, na tena wanyama wengi wa kufugwa?”​—Yona 4:10, 11. *

21. (a) Yehova alimfundisha Yona somo gani? (b) Simulizi la Yona linawezaje kutusaidia kujichunguza kwa unyoofu?

21 Je, unaelewa maana ya mfano ambao Yehova alitumia? Yona hakuwa amefanya chochote ili kuutunza mmea huo. Kwa upande mwingine, Yehova alikuwa amewapa Waninawi uhai na aliwategemeza kama anavyowategemeza viumbe wote duniani. Yona angewezaje kuthamini zaidi mmea mmoja kuliko maisha ya wanadamu 120,000, pamoja na wanyama wao wote wa kufugwa? Ni kwa sababu Yona alifikiri kwa njia ya kibinafsi. Alisikitikia mmea huo kwa sababu ulikuwa umemnufaisha yeye mwenyewe. Vivyo hivyo, aliwakasirikia Waninawi kwa sababu za kibinafsi. Alitamani kuheshimiwa, na kutoonekana kuwa mwongo. Simulizi la Yona linaweza kutusaidia tujichunguze kwa unyoofu. Sote tuna mwelekeo wa kutenda kwa ubinafsi. Tunathamini sana kwamba Yehova anatufundisha kwa subira kutokuwa na ubinafsi, na pia kuonyesha hata zaidi huruma na rehema!

22. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yona alijifunza kutokana na ushauri wenye hekima wa Yehova kuhusu rehema? (b) Sote tunapaswa kujifunza somo gani?

22 Swali ni, je, Yona alielewa somo hilo? Kitabu cha Yona kinamalizika bila kujibu swali la Yehova. Huenda wachambuzi fulani wakalalamika kwamba Yona hakujibu. Hata hivyo, alijibu. Aliandika kitabu cha Yona. Uthibitisho unaonyesha kwamba Yona ndiye aliyeandika kitabu hicho. Hebu mwazie nabii huyo akiandika simulizi hilo akiwa salama nchini kwao. Tunaweza kumwazia mtu aliyezeeka, mwenye hekima na mnyenyekevu zaidi akitikisa kichwa anapoandika makosa yake mwenyewe, uasi wake, na jinsi alivyokataa kwa ukaidi kuonyesha rehema. Ni wazi kwamba Yona alijifunza kutokana na maagizo ya Yehova yenye hekima. Alijifunza kuonyesha rehema. Namna gani sisi?​—Soma Mathayo 5:7.

^ fu. 6 Inakadiriwa kwamba katika siku za Yona, Samaria, mji mkuu wa ufalme wa makabila kumi ya Israeli ulikuwa na wakaaji kati ya 20,000 na 30,000, karibu robo ya wakaaji wa Ninawi. Jiji la Ninawi lilipositawi na kuwa maarufu, huenda lilikuwa jiji kubwa zaidi ulimwenguni.

^ fu. 8 Huenda hilo likashangaza, lakini lilikuwa jambo la kawaida zamani. Mwanahistoria Mgiriki Herodoto alisema kwamba Waajemi wa kale waliomboleza kifo cha jenerali maarufu kwa kuhusisha wanyama wa kufugwa katika desturi za kuomboleza.

^ fu. 20 Mungu aliposema kwamba watu hao hawakujua tofauti kati ya kuume na kushoto alimaanisha kwamba hawakujua sheria za Mungu.