Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA SITA

Alimweleza Mungu Mahangaiko Yake

Alimweleza Mungu Mahangaiko Yake

1, 2. (a) Kwa nini Hana alikuwa na huzuni alipokuwa akijitayarisha kwa safari? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na simulizi la Hana?

HANA alikuwa akijitayarisha kwa ajili ya safari, huku akijaribu kusahau matatizo yake. Hiyo ilipaswa kuwa pindi yenye furaha; Elkana, mume wake alikuwa na desturi ya kusafiri na familia yake yote kwenda kwenye maskani huko Shilo kila mwaka. Yehova alitaka pindi hizo ziwe zenye shangwe. (Soma Kumbukumbu la Torati 16:15.) Na bila shaka tangu utotoni, Hana alifurahia sherehe hizo. Lakini mambo yalikuwa yamebadilika katika miaka ya hivi karibuni.

2 Hana alipendwa sana na mume wake. Hata hivyo, Elkana alikuwa na mke mwingine. Aliitwa Penina, naye alikuwa ameazimia kufanya maisha ya Hana yawe magumu. Penina alitumia pindi hizo za kila mwaka kumfadhaisha Hana hata zaidi. Jinsi gani? Na jambo muhimu hata zaidi, imani ya Hana katika Yehova ilimsaidiaje kukabiliana na hali hiyo iliyoonekana kuwa ngumu sana? Ikiwa unakabili matatizo yanayokufanya ukose shangwe maishani, huenda simulizi la Hana likakutia moyo.

“Kwa Nini Moyo Wako Unahisi Vibaya?”

3, 4. Hana alikabili matatizo gani mawili, na kwa nini kila tatizo lilikuwa gumu?

3 Biblia inafunua matatizo mawili yaliyomkumba Hana. Angeweza kuvumilia kwa kiasi fulani tatizo la kwanza, lakini tatizo la pili lilipita uwezo wake. Kwanza, alikuwa katika ndoa ya wake wengi na mke mwenzake alimchukia. Pili, Hana alikuwa tasa. Hilo ni jambo gumu kwa mke yeyote anayetaka kuzaa watoto; na kulingana na tamaduni za siku za Hana jambo hilo lilileta huzuni kubwa. Kila familia ilitegemea watoto ili kuendeleza jina la familia. Kwa hiyo, kutozaa kulionwa kuwa suto na aibu.

4 Huenda Hana angekabiliana na hali yake kwa mafanikio ikiwa Penina hangemtaabisha. Ndoa ya wake wengi ilisababisha hali ngumu. Mara nyingi ndoa hizo zilikuwa na mashindano, chuki, na uchungu. Zoea hilo halikupatana na mpango wa Mungu wa ndoa ya mke mmoja ambao alianzisha katika bustani ya Edeni. (Mwa. 2:24) Hivyo, Biblia inapozungumzia familia ya Elkana inaonyesha wazi kwamba ndoa ya wake wengi ni chanzo cha matatizo.

5. Kwa nini Penina alitaka Hana ateseke, na alitumia njia gani kumwumiza Hana?

5 Elkana alimpenda sana Hana. Hadithi za Kiyahudi zinasema kwamba alimwoa Hana kwanza, kisha akamwoa Penina baada ya miaka kadhaa. Vyovyote vile, Penina alimwonea wivu sana Hana, na alitafuta njia za kumtaabisha mke mwenzake. Penina alijiona kuwa bora kwa sababu alikuwa na uwezo wa kuzaa. Alizaa mtoto mmoja baada ya mwingine, na kadiri watoto wake walivyoongezeka ndivyo alivyozidi kuwa na kiburi. Badala ya kumhurumia Hana na kumfariji, Penina alimfadhaisha kwa sababu alikuwa tasa. Biblia inasema kwamba Penina alimsumbua mno Hana kiasi cha “kumfadhaisha.” (1 Sam. 1:6) Penina alifanya hivyo kimakusudi. Alitaka kumwumiza Hana, na alifaulu.

Hana alihuzunika sana kwa sababu alikuwa tasa, na Penina alifanya kila awezalo ili kumuudhi

6, 7. (a) Ingawa Elkana alijaribu kumfariji Hana, kwa nini huenda Hana hakumweleza habari zote? (b) Kwa vile Hana alikuwa tasa, je, ilimaanisha kwamba Yehova hakupendezwa naye? Eleza. (Ona maelezo ya chini.)

6 Inaonekana Penina alipata nafasi ya kumdhihaki Hana walipofunga safari za kwenda Shilo kila mwaka. Elkana alimpa kila mtoto wa Penina—“wanawe na binti zake wote”—fungu la dhabihu zilizotolewa kwa Yehova. Lakini Hana ambaye hakuwa na mtoto alipewa fungu la pekee. Kisha Penina mwenye wivu alijitutumua sana kwa Hana na kumkumbusha kuhusu hali yake ya kuwa tasa hivi kwamba mwanamke huyo akaanza kulia sana na kukosa hamu ya kula. Elkana alitambua kwamba Hana mke wake mpendwa alikuwa amefadhaika na hakuwa akila, hivyo akajaribu kumfariji. Alimwuliza: “Hana, kwa nini unalia, na kwa nini huli chakula, na kwa nini moyo wako unahisi vibaya? Je, mimi si bora kwako kuliko wana kumi?”​—1 Sam. 1:4-8.

7 Elkana alitambua kwamba Hana alifadhaika kwa sababu alikuwa tasa. Na Hana alithamini sana jinsi Elkana alivyompenda kwa wororo. * Elkana hakuzungumzia chuki ya Penina; wala Biblia haisemi kwamba Hana alimwambia jambo hilo. Labda alihisi kwamba kumshitaki Penina kungefanya hali yake iwe mbaya hata zaidi. Je, Elkana angeingilia kati? Hilo lingemfanya Penina amchukie zaidi Hana na kuwafanya watoto na watumishi wa Penina wafanye hivyo pia. Na hivyo, Hana angehisi kuwa ametengwa kabisa katika nyumba yake mwenyewe.

Alipotendewa vibaya nyumbani, Hana alimgeukia Yehova ili kupata faraja

8. Unapochukiwa au kutendewa isivyo haki, kwa nini inafariji kukumbuka Yehova ni Mungu wa haki?

8 Iwe Elkana alijua kuhusu chuki ya Penina au la, Yehova aliona yote yaliyokuwa yakitendeka. Neno lake linafunua kwamba aliona mambo yote, na hilo linatoa onyo kwa wale walio na tabia ya kuwaonea wengine wivu na kuwachukia. Kwa upande mwingine, watu wasio na hatia na wenye kufanya amani kama Hana wanaweza kufarijika kujua kwamba Mungu wa haki husuluhisha mambo kwa njia yake na kwa wakati wake. (Soma Kumbukumbu la Torati 32:4.) Labda Hana alijua jambo hilo kwa kuwa alimwomba Yehova msaada.

“Hakuonyesha Tena Kuhangaika”

9. Tunajifunza nini kutokana na utayari wa Hana wa kusafiri kwenda Shilo ingawa alijua jinsi ambavyo Penina angemtendea?

9 Asubuhi na mapema, familia nzima ilikuwa na pilikapilika nyingi. Kila mtu alikuwa akijitayarisha kwa safari, kutia ndani watoto. Safari hiyo ya kwenda Shilo ilikuwa ya kilomita zaidi ya 30 kuvuka nchi ya Efraimu yenye milima-milima. * Safari hiyo ingechukua siku moja au mbili kwa miguu. Hana alijua jinsi ambavyo Penina angemtendea. Hata hivyo, hakubaki nyumbani. Kwa hiyo, akawawekea mfano mzuri waabudu wa Mungu mpaka leo. Si jambo la hekima kuruhusu mwenendo mbaya wa wengine utuzuie kumwabudu Mungu. Tukiruhusu watuzuie, tutakosa baraka zinazotusaidia kuvumilia.

10, 11. (a) Kwa nini Hana alienda kwenye maskani bila kukawia? (b) Hana alimwelezaje Baba yake wa mbinguni mahangaiko yake katika sala?

10 Baada ya kusafiri siku nzima kwenye barabara za milimani zilizopinda-pinda, familia hiyo kubwa ilikaribia Shilo. Waliliona jiji hilo lililokuwa limezungukwa na vilima virefu. Walipokuwa wakikaribia, huenda Hana alitafakari mambo ambayo angemwambia Yehova katika sala. Mara tu familia hiyo ilipofika, walikula pamoja. Hana alipopata nafasi, mara moja aliondoka na kwenda kwenye maskani ya Yehova. Kuhani Mkuu Eli alikuwa ameketi karibu na mlango. Lakini Hana alikazia fikira Mungu wake. Alikuwa na uhakika kwamba angesikiwa akiwa katika maskani. Ingawa hakuna mwanadamu ambaye angeelewa hali yake yenye kufadhaisha, Baba yake aliye mbinguni angemwelewa. Uchungu ulimjaa moyoni na akaanza kulia.

11 Huku akitetemeka kwa sababu ya kulia, Hana alizungumza na Yehova kimoyomoyo. Midomo yake ilitetemeka alipokuwa akitafakari maneno ya kueleza uchungu wake. Alisali kwa muda mrefu, akimweleza Baba yake yaliyokuwa moyoni mwake. Hata hivyo, alifanya mengi zaidi ya kumwomba Mungu atimize tamaa yake ya kupata mtoto. Hana hakutamani tu kupata baraka za Mungu bali pia alitaka kumpa Mungu chochote ambacho angeweza. Kwa hiyo, aliweka nadhiri akisema kwamba ikiwa angepata mtoto wa kiume angemtoa ili amtumikie Yehova.​—1 Sam. 1:9-11.

12. Kama mfano wa Hana unavyoonyesha, tunapaswa kukumbuka nini kuhusu sala?

12 Hivyo, Hana anawawekea watumishi wote wa Yehova mfano mzuri kuhusu sala. Yehova anawaalika watu wake wawasiliane naye kwa uhuru, bila kuogopa, wakimmiminia mahangaiko yao kama vile tu mtoto anayemwamini mzazi mwenye upendo anavyofanya. (Soma Zaburi 62:8; 1 Wathesalonike 5:17.) Mtume Petro aliongozwa na roho ya Mungu kuandika maneno haya yenye kufariji kuhusu sala kwa Yehova: ‘Tupeni mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.’​—1 Pet. 5:7.

13, 14. (a) Eli alikataje kauli yenye makosa haraka-haraka kumhusu Hana? (b) Jibu la Hana kwa Eli linatuwekea mfano gani bora wa imani?

13 Hata hivyo, wanadamu hawawezi kuelewa na kuonyesha huruma kikamili kama Yehova. Hana alipokuwa akilia na kusali alishtuka kusikia sauti ya mtu fulani. Ilikuwa sauti ya Eli, kuhani mkuu, ambaye alikuwa akimtazama. Eli akamwambia: “Utaendelea kujiendesha kama mlevi mpaka wakati gani? Iondolee mbali divai yako.” Eli alikuwa ameona midomo ya Hana ikitetemeka, machozi yake, na huzuni yake nyingi. Badala ya kumwuliza tatizo lake, Eli alikata kauli haraka kwamba Hana alikuwa mlevi.—1 Sam.1:12-14.

14 Kushutumiwa bila msingi wowote na mwanamume aliye na cheo chenye kuheshimika kulimwumiza sana Hana, hasa wakati huu alipokuwa amefadhaika. Hata hivyo, aliweka tena mfano bora wa imani. Hakuruhusu kutokamilika kwa mwanadamu kumzuie kumwabudu Yehova. Alimjibu Eli kwa heshima na akamweleza hali yake. Eli alipotambua kuwa amekosea, alijibu labda kwa sauti ya upole akisema: “Nenda kwa amani, naye Mungu wa Israeli akupe ombi lako ambalo umemwomba.”​—1 Sam. 1:15-17.

15, 16. (a) Hana alihisije baada ya kumwabudu na kumweleza Yehova mahangaiko yake kwenye maskani? (b) Tunawezaje kuiga mfano wa Hana tunapokabiliana na hisia zisizofaa?

15 Hana alipomweleza Yehova mahangaiko yake na kumwabudu katika maskani, alihisije? Simulizi hilo linasema: “Mwanamke huyo akaenda zake, akala chakula, na uso wake haukuonyesha tena kuhangaika.” (1 Sam. 1:18) Biblia Habari Njema inasema: “Hakuwa na huzuni tena.” Hana alihisi utulivu. Ni kana kwamba alikuwa amechukua mzigo wake wa kihisia na kumtupia Yehova, Baba yake wa mbinguni mwenye nguvu. (Soma Zaburi 55:22.) Je, Yehova anaweza kushindwa na tatizo lolote? La—hajawahi kushindwa na kamwe hatashindwa!

16 Tunapohisi tumelemewa na hisia au kuhuzunika kupita kiasi, tunaweza kumwiga Hana na kuzungumza waziwazi na Mungu ambaye Biblia inamwita “Msikiaji wa sala.” (Zab. 65:2) Tukisali kwa imani, huenda tukaacha kuhuzunika na badala yake tukawa na “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.”​—Flp. 4:6, 7.

“Hakuna Mwamba Ulio Kama Mungu Wetu”

17, 18. (a) Elkana alionyeshaje kwamba aliunga mkono nadhiri ya Hana? (b) Penina hangeweza tena kumfanya nini Hana?

17 Asubuhi iliyofuata, Hana alirudi kwenye maskani akiwa na Elkana. Huenda alimweleza kuhusu ombi lake na nadhiri aliyoweka, kwa kuwa Sheria ya Musa ilisema kwamba mume alikuwa na haki ya kufutilia mbali nadhiri iliyowekwa na mke wake bila ruhusa yake. (Hes. 30:10-15) Lakini mwanamume huyo mwaminifu hakufanya hivyo. Badala yake, yeye na Hana walimwabudu Yehova kwenye maskani kisha wakarudi nyumbani.

18 Ni wakati gani ambapo Penina alitambua hangeweza tena kumhuzunisha Hana? Simulizi hilo halitaji, lakini maneno uso wa Hana “haukuonyesha tena kuhangaika” yanaonyesha kuanzia wakati huo Hana alikuwa mwenye furaha. Vyovyote vile, baada ya muda mfupi Penina aligundua hangeweza tena kumhuzunisha Hana. Baada ya hapo, Biblia haimtaji Penina tena.

19. Hana alipata baraka gani, na alifanya nini ili kumwonyesha uthamini yule aliyembariki?

19 Kadiri miezi ilivyopita, Hana alizidi kuwa na amani ya akili na furaha tele. Akashika mimba! Shangwe yake haikumfanya asahau ni nani aliyekuwa amembariki. Mvulana wake alipozaliwa, alimpa jina Samweli, linalomaanisha “Jina la Mungu,” na ni wazi linarejelea kuliitia jina la Mungu, kama Hana alivyokuwa amefanya. Mwaka huo hakufuatana na Elkana na familia yake kwenda Shilo. Alikaa nyumbani na mtoto huyo kwa miaka mitatu, hadi alipomwachisha kunyonya. Kisha akajitayarisha kwa ajili ya siku ambayo mwanawe mpendwa angeondoka nyumbani.

20. Hana na Elkana walitimizaje ahadi yao kwa Yehova?

20 Ni wazi kwamba haingekuwa rahisi kutengana na mwanawe. Bila shaka, Hana alijua kwamba Samweli angetunzwa huko Shilo, labda na wanawake fulani waliotumikia kwenye maskani. Lakini, bado alikuwa mchanga, na ni mama gani ambaye hangetamani kukaa pamoja na mtoto wake? Hata hivyo, Hana na Elkana walimpeleka mvulana huyo, si kwa kulazimishwa bali kwa kupenda. Walitoa dhabihu katika nyumba ya Mungu, wakamkabidhi Samweli kwa Eli, na wakamkumbusha kuhusu nadhiri ambayo Hana alikuwa ameweka miaka kadhaa iliyopita

Hana alithibitika kuwa baraka kwelikweli kwa mwana wake Samweli

21. Sala ya Hana kwa Yehova ilionyeshaje kwamba alikuwa na imani yenye nguvu? (Ona pia sanduku “ Sala Mbili za Pekee.”)

21 Kisha, Hana akatoa sala ambayo Mungu aliona ilistahili kutiwa ndani ya Neno lake lililoongozwa na roho. Unaposoma maneno yake yaliyoandikwa katika 1 Samweli 2:1-10, utaona kila mstari unaonyesha alikuwa na imani yenye nguvu. Alimsifu Yehova kwa kutumia nguvu zake kwa njia ya ajabu—uwezo wake usio na kifani wa kuwashusha wenye majivuno, kuwabariki walioonewa, na kuua au kuhifadhi uhai. Alimsifu Baba yake kwa utakatifu wake wa pekee, haki yake, na uaminifu wake. Hana alisema hivi kwa uhakika: “Hakuna mwamba ulio kama Mungu wetu.” Yehova anategemeka kabisa, na habadiliki, ni kimbilio kwa wote walioonewa na kukandamizwa na ambao wanamwomba msaada.

22, 23. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Samweli aliendelea kukua akijua kwamba alipendwa na wazazi wake? (b) Yehova alimbariki Hana kwa njia gani nyingine?

22 Kijana Samweli alikuwa na pendeleo kubwa la kuwa na mama aliyekuwa na imani yenye nguvu katika Yehova. Ingawa alimkosa sana mama yake alipokuwa akikua, hakuhisi amesahaulika. Kila mwaka, Hana angerudi Shilo, akiwa na koti lisilo na mikono ambalo Samweli angevaa alipokuwa akitumikia kwenye maskani. Kwa kumshonea koti hilo alionyesha wazi kwamba alimpenda na kumjali mwanawe. (Soma 1 Samweli 2:19.) Tunaweza kuwazia akimvisha mvulana wake koti hilo jipya, akilinyoosha, na kumtazama kwa upendo huku akizungumza naye kwa fadhili na kumtia moyo. Samweli alibarikiwa sana kuwa na mama kama huyo, naye akaja kuwa baraka kubwa kwa wazazi wake na taifa lote la Israeli.

23 Hana naye hakusahauliwa. Yehova alimbariki kwa kumrudishia uwezo wa kuzaa, naye akamzalia Elkana watoto wengine watano. (1 Sam. 2:21) Hata hivyo, huenda baraka kubwa zaidi ambayo Hana alipata ni uhusiano wa karibu pamoja na Baba yake, Yehova, ambao uliendelea kuimarika kadiri miaka ilivyopita. Na iwe hivyo pia kwako unapojitahidi kuiga imani ya Hana.

^ fu. 7 Ingawa Biblia inasema kwamba Yehova alikuwa ‘amefunga tumbo la uzazi la Hana,’ hilo halithibitishi kuwa Mungu hakupendezwa na mwanamke huyo mwaminifu na mnyenyekevu. (1 Sam. 1:5) Nyakati nyingine Biblia husema Mungu alifanya mambo fulani kwa kuwa tu aliyaruhusu yatendeke kwa muda.

^ fu. 9 Umbali huo unategemea uwezekano wa kwamba mji wa nyumbani wa Elkana ulikuwa Rama, eneo ambalo baadaye katika siku za Yesu liliitwa Arimathea.