Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Umalizio

Umalizio

“Muwe waigaji wa wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.”—WAEBRANIA 6:12.

1, 2. Kwa nini ni muhimu kwetu leo kuimarisha imani? Toa mfano.

IMANI. Hilo ni neno lenye kupendeza, ambalo linamaanisha sifa muhimu. Hata hivyo, tunaposoma neno hilo, tunapaswa kukumbuka neno lingine: “Uharaka!” Kwa kweli, ikiwa hatuna imani tunapaswa kutafuta sifa hiyo haraka. Na kama tuna imani, tunapaswa kuilinda na kuiimarisha haraka. Kwa nini?

2 Wazia kwamba unavuka jangwa kubwa. Unahitaji sana kuwa na maji. Ukipata maji, unapaswa kuyalinda kutokana na jua. Pia, unahitaji kuchota maji zaidi ili uwe na ya kutosha mpaka utakapofika. Leo, tunaishi katika jangwa la kiroho, ulimwengu ambamo imani ya kweli—kama maji hayo—haipatikani na inapotea haraka isipolindwa na kuimarishwa. Tunahitaji imani sikuzote; kama vile tusivyoweza kuishi bila maji, hatuwezi kuwa na uhusiano mzuri na Yehova bila imani.—Rom. 1:17.

3. Yehova ametupatia nini ili kutusaidia kusitawisha imani, na ni mambo gani mawili tunayohitaji kufanya?

3 Yehova anatambua jinsi tunavyohitaji sana kuwa na imani, na anajua jinsi ilivyo vigumu kusitawisha na kuimarisha imani leo. Bila shaka, hiyo ndiyo sababu ametupatia mifano ya kuiga. Yehova alimwongoza mtume Paulo kuandika hivi: “Muwe waigaji wa wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.” (Ebr. 6:12) Na ndiyo sababu tengenezo la Yehova linatuhimiza tujitahidi kuiga mifano ya wanaume na wanawake waaminifu, kama wale ambao tumechunguza katika kitabu hiki. Hata hivyo, tunapaswa kufanya nini? Acheni tukumbuke mambo haya mawili: (1) Tunahitaji kuendelea kuimarisha imani yetu; (2) tunahitaji kuendelea kukumbuka tumaini letu.

4. Shetani amethibitikaje kuwa adui wa imani, na kwa nini hatupaswi kuogopa?

4 Endelea kuimarisha imani yako. Imani ina adui mkubwa—Shetani. Mtawala huyo wa ulimwengu amefanya mfumo huu uwe jangwa linaloangamiza imani. Ana nguvu nyingi kuliko sisi. Je, tunapaswa kuogopa kusitawisha na kuimarisha imani? Hapana! Yehova ni Rafiki mkuu wa wale wanaositawisha imani ya kweli. Anatuhakikishia kwamba Akiwa upande wetu, tutafaulu kumpinga Ibilisi na kumfanya atukimbie! (Yak. 4:7) Tunampinga kwa kutenga wakati kila siku ili kuimarisha na kujenga imani yetu. Jinsi gani?

5. Wanaume na wanawake waaminifu wanaotajwa katika Biblia walipataje imani? Fafanua.

5 Kama tulivyoona, wanaume na wanawake wanaotajwa katika Biblia hawakuzaliwa wakiwa na imani. Maisha yao yalionyesha kwamba roho takatifu ndiyo chanzo cha imani. (Gal. 5:22, 23) Walisali ili wapate msaada, naye Yehova akaendelea kuimarisha imani yao. Acheni tuwaige, bila kusahau kwamba Yehova huwapa roho takatifu kwa ukarimu wale wanaomwomba na kutenda kulingana na sala zao. (Luka 11:13) Je, kuna jambo lingine tunaloweza kufanya?

6. Tunawezaje kufaidika zaidi tunaposoma masimulizi ya Biblia?

6 Katika kitabu hiki, tumechunguza mifano michache tu ya watu waliokuwa na imani thabiti. Kuna wengine chungu nzima! (Soma Waebrania 11:32.) Kila mfano una habari nyingi tunazoweza kuchunguza kwa makini na kuzitafakari. Tukisoma haraka-haraka masimulizi ya Biblia kuhusu watu wenye imani, hatutafaidika sana. Ili tufaidike kikamili, tunahitaji kutumia muda ili kuchunguza kwa undani muktadha na hali zilizokuwepo katika masimulizi ya Biblia. Ikiwa sikuzote tutakumbuka kwamba wanaume na wanawake hao wasio wakamilifu walikuwa na “hisia kama zetu,” mifano yao itakuwa halisi zaidi kwetu. (Yak. 5:17) Tukihisi kama walivyohisi, tutaelewa hisia zao walipokabili majaribu na matatizo kama yale tunayokabili.

7-9. (a) Huenda wanaume na wanawake wenye imani wanaotajwa katika Biblia wangehisije ikiwa wangemwabudu Yehova jinsi tunavyofanya leo? (b) Kwa nini tunapaswa kuimarisha imani yetu kupitia matendo?

7 Pia, tunaimarisha imani yetu kupitia matendo. Kwa kweli, “imani bila matendo imekufa.” (Yak. 2:26) Hebu wazia jinsi ambavyo wanaume na wanawake ambao tumechunguza wangefurahi ikiwa wangepewa kazi ambayo Yehova ametupatia leo!

8 Kwa mfano, ingekuwaje kama Abrahamu angeambiwa amwabudu Yehova, si kwenye madhabahu yaliyojengwa nyikani kwa mawe ambayo hayajachongwa, bali pamoja na waabudu wenzake katika Majumba ya Ufalme na makusanyiko makubwa, ambako ahadi alizoona “kwa mbali” zinazungumziwa na kufafanuliwa kwa njia ya kustaajabisha? (Soma Waebrania 11:13.) Namna gani ikiwa Eliya angeambiwa kazi yake haingehusisha kuwaangamiza manabii wa Baali huku akijaribu kumtumikia Yehova chini ya utawala wa mfalme mwovu aliyeasi imani, na badala yake awatembelee watu kwa amani ili kuwatangazia ujumbe wa faraja na tumaini? Bila shaka, wanaume na wanawake wenye imani wanaotajwa katika Biblia wangefurahi sana kama wangemwabudu Yehova kama tunavyofanya leo?

9 Basi, acheni tuimarishe imani yetu kwa matendo. Tukifanya hivyo, tutaiga kihalisi mifano ya wanaume na wanawake wenye imani wanaotajwa katika Neno la Mungu. Kama ilivyotajwa katika Utangulizi, tutakuwa na urafiki wa karibu zaidi nao. Hata hivyo, hivi karibuni uhusiano huo utakuwa halisi zaidi.

10. Tutapata shangwe gani katika Paradiso?

10 Endelea kukumbuka tumaini lako. Sikuzote, wanaume na wanawake waaminifu wametiwa nguvu na tumaini walilopewa na Mungu. Namna gani wewe? Kwa mfano, wazia shangwe ya kukutana na waabudu waaminifu wa Mungu baada ya “ufufuo wa waadilifu.” (Soma Matendo 24:15.) Ungependa kuwauliza maswali gani?

11, 12. Katika ulimwengu mpya, huenda ukauliza watu wafuatao maswali gani? (a) Abeli. (b) Noa. (c) Abrahamu. (d) Ruthu. (e) Abigaili. (f) Esta.

11 Utakapokutana na Abeli, je, ungependa kumuuliza kuhusu utu na sura ya wazazi wake? Au huenda ukamuuliza: “Je, uliwahi kuzungumza na makerubi waliokuwa wakilinda mwingilio wa Edeni? Je, walikujibu?” Namna gani Noa? Huenda ukamuuliza: “Je, uliwaogopa Wanefili? Uliwatunzaje wanyama wengi hivyo ulipokuwa ndani ya safina?” Ukikutana na Abrahamu, huenda ukauliza: “Je, uliwahi kukutana na Shemu? Ni nani aliyekufundisha kuhusu Yehova? Je, ilikuwa vigumu kuondoka Uru?”

12 Vivyo hivyo, fikiria maswali ambayo huenda ukawauliza wanawake waaminifu watakaofufuliwa. “Ruthu, ni nini kilichokuchochea uwe mwabudu wa Yehova?” “Abigaili, je, uliogopa kumweleza Nabali kuhusu jinsi ulivyomsaidia Daudi?” “Esta, ilikuwaje kwako na kwa Mordekai baada ya simulizi lililo katika Biblia kwisha?”

13. (a) Huenda wale watakaofufuliwa watakuuliza maswali gani? (b) Unahisije kuhusu tumaini la kuwaona wanaume na wanawake waaminifu walioishi zamani?

13 Bila shaka, huenda pia wanaume na wanawake hao waaminifu watakuuliza maswali mengi. Itasisimua kama nini kuwaambia kuhusu siku za mwisho na jinsi Yehova alivyobariki watu wake walipokabili matatizo! Kwa kweli, watafurahi kujifunza jinsi Yehova alivyotimiza ahadi zake zote. Wakati huo ujao, haitakuwa vigumu kuelewa hali walizokabili watumishi washikamanifu wa Mungu wanaotajwa katika Biblia. Watakuwa pamoja nasi, katika Paradiso! Basi, endelea kujitahidi kabisa sasa kuwaelewa vizuri watu hao. Endelea kuiga imani yao. Na ufurahie kumtumikia Yehova pamoja nao wakiwa rafiki zako milele!