Hamia kwenye habari

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kufunga?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kufunga?

Jibu la Biblia

 Katika nyakati za Biblia, kufunga kulikubalika machoni pa Mungu maadamu kulifanywa kwa nia inayofaa. Lakini mtu alipofunga kwa sababu zisizofaa, Mungu alikasirika. Hata hivyo, Biblia haiamuru watu wafunge wala kuwakataza wasifunge.

Watu fulani katika Biblia walifunga chini ya hali zipi?

  •   Walipotafuta msaada na mwongozo wa Mungu. Watu waliokuwa wakisafiri kwenda Yerusalemu walifunga ili kumwonyesha Mungu kwamba wanamwomba msaada kwa unyoofu. (Ezra 8:​21-​23) Nyakati fulani Paulo na Barnaba walichagua kufunga walipokuwa wakiwaweka rasmi wazee wa kutaniko.​—Matendo 14:23.

  •   Walipokazia fikira kusudi la Mungu. Baada ya ubatizo, Yesu alifunga siku 40 ili kujitayarisha kufanya mapenzi ya Mungu wakati wa huduma aliyokuwa karibu kuanza.​—Luka 4:​1, 2.

  •   Walipokuwa wakionyesha toba kutokana na dhambi za wakati uliopita. Kupitia nabii Yoeli, Mungu aliwaambia Waisraeli waliokosa kuwa waaminifu: “Rudini kwangu kwa mioyo yenu yote, kwa kufunga na kulia na kuomboleza.”​—Yoeli 2:12-15.

  •   Walipokuwa wakisherehekea Siku ya Kufunika Dhambi. Sheria ambayo ya Mungu aliwapa Waisraeli ilitia ndani amri ya kufunga wakati wa Siku ya Kufunika Dhambi ya kila mwaka. a (Mambo ya Walawi 16:29-​31) Ilikuwa muhimu sana kufunga wakati wa sherehe hiyo kwa sababu iliwakumbusha Waisraeli kwamba hawakuwa wakamilifu na walihitaji msamaha wa Mungu.

Ni sababu zipi zisizofaa za kufunga?

  •   Kujionyesha mbele ya watu. Yesu alifundisha kwamba kufunga kwa kidini kunapaswa kuwa jambo la kibinafsi kati mtu mwenyewe na Mungu.​—Mathayo 6:​16-​18.

  •   Kujionyesha kuwa mwadilifu. Kufunga hakumfanyi mtu kuwa bora kuliko wengine kimaadili au kiroho.​—Luka 18:​9-​14.

  •   Kujaribu kulipia mazoea ya kufanya dhambi kimakusudi. (Isaya 58:​3, 4) Mungu alikubali tu kufunga kulikofanywa na watu ambao walimtii na waliotubu kutoka moyoni dhambi zozote walizokuwa wamefanya.

  •   Kufuata desturi ya kidini. (Isaya 58:​5-7) Kuhusiana na hili, Mungu ni kama mzazi ambaye anachukizwa watoto wake wanapomwonyesha kuwa wanampenda kwa sababu tu ya wajibu, bali si kutoka moyoni..

Je, kufunga ni takwa kwa Wakristo?

 Hapana. Mungu aliwawekea Waisraeli takwa la kufunga wakati wa Siku ya Kufunika Dhambi, lakini alikomesha mwadhimisho huo baada ya Yesu kufunika kikamili dhambi za watu wanaotubu. (Waebrania 9:​24-​26; 1 Petro 3:​18) Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa, ambayo ilikuwa na Siku ya Kufunika Dhambi. (Waroma 10:4; Wakolosai 2:​13, 14) Hivyo, kila Mkristo anaweza kujiamulia ikiwa atafunga au la.​—Waroma 14:​1-4.

 Wakristo wanatambua kwamba jambo kuu katika ibada yao si kufunga. Biblia haihusianishi kamwe kufunga na furaha. Tofauti na hilo, Ukristo wa kweli unatambulishwa na shangwe, na pia hilo linapatana na utu wa Yehova, yule “Mungu mwenye furaha.”​—1 Timotheo 1:​11; Mhubiri 3:12, 13; Wagalatia 5:22.

Maoni yasiyo sahihi kuhusu Biblia inachosema kuhusiana na kufunga

 Maoni yasiyo sahihi: Mtume Paulo alipendekeza kwamba Wakristo waliofunga ndoa wanapaswa kufunga.​—1 Wakorintho 7:5, King James Version.

 Ukweli: Hati za kale zaidi za Biblia hazitaji kufunga kwenye 1 Wakorintho 7:5. b Ni wazi kwamba wanakili wa Biblia waliongeza maneno hayo kuhusu kufunga, na si katika mstari huo tu bali pia kwenye Mathayo 17:21; Marko 9:​29; na Matendo 10:30. Tafsiri nyingi za karibuni za Biblia hazitaji kufunga katika mistari hiyo.

 Maoni yasiyo sahihi: Wakristo wanapaswa kufunga ili kukumbuka siku 40 ambazo Yesu alifunga alipokuwa nyikani baada ya ubatizo wake.

 Ukweli: Yesu hakuamuru kamwe kwamba watu wafunge kwa njia hiyo, wala hakuna chochote katika Maandiko kinachoonyesha kwamba Wakristo wa mapema walifunga kwa njia hiyo. c

 Maoni yasiyo sahihi: Wakristo wanapaswa kufunga wanapoadhimisha kifo cha Yesu.

 Ukweli: Yesu hakuwaamuru wanafunzi wake wafunge wanapoadhimisha kifo chake. (Luka 22:14-​18) Ingawa Yesu alisema kwamba wanafunzi wake wangefunga baada ya yeye kufa, hakuwa akitoa amri bali alikuwa tu akisema kitakachotokea. (Mathayo 9:​15) Biblia iliwaagiza Wakristo waliokuwa na njaa wale nyumbani kabla ya kuadhimisha Ukumbusho wa Kifo cha Yesu.​—1 Wakorintho 11:33, 34.

a Mungu aliwaambia Waisraeli hivi: “Mnapaswa kujitesa,” au “mtajitaabisha roho zenu,” wakati wa Siku ya Kufunika Dhambi. (Mambo ya Walawi 16:29, 31) Maneno hayo yanamaanisha kufunga. (Isaya 58:3) Hivyo, Biblia Habari Njema inasema hivi: “Ni lazima mfunge siku hiyo.”

b Ona kitabu A Textual Commentary on the Greek New Testament, cha Bruce M. Metzger, Toleo la Tatu, ukurasa wa 554.

c Kuhusu historia ya kufunga kwa siku 40 inayoitwa Kwaresima, kitabu New Catholic Encyclopedia kinasema hivi: “Katika karne tatu za kwanza, kipindi cha matayarisho ya sherehe ya paschal [Ista] hakikuzidi juma moja; urefu ulikuwa siku moja au mbili. . . . Kipindi cha siku 40 kinatajwa kwa mara ya kwanza katika kitabu cha tano cha Baraza la Nicaea (325), ingawa baadhi ya wasomi wanapinga ikiwa kinachomaanishwa na Kwaresima.”​—Toleo la Pili, Buku la 8, ukurasa wa 468.