Hamia kwenye habari

Ninaweza Kupata Wapi Tumaini?

Ninaweza Kupata Wapi Tumaini?

Jibu la Biblia 

 Biblia inasema Mungu anataka kutupatia “wakati ujao na tumaini.” a (Yeremia 29:11) Kwa kweli, sababu moja ambayo Mungu ametupatia Biblia ni ili “kupitia faraja kutoka kwa Maandiko tuwe na tumaini.” (Waroma 15:4) Kama tutakavyoona, mwongozo wa Biblia unaofaa unaweza kutusaidia kuwa na mtazamo mzuri wa kushughulikia matatizo kila siku, huku ahadi zake zikitupa tumaini zuri kwa ajili ya wakati ujao. 

Kwenye ukurasa huu 

 Biblia inatusaidiaje kuwa na mtazamo wenye tumaini? 

 Kwa kutuonyesha hatua zinazofaa za kuchukua ili kuboresha  maisha yetu, Biblia inaweza kutusaidia kuwa na mtazamo wenye tumaini. Fikiria mifano kadhaa. 

  •    Tafuta mwongozo unaofaa katika Biblia. Zaburi 119:105 inasema: “Neno lako ni taa ya mguu wangu, na nuru ya njia yangu.” Taa yenye nguvu inaweza kusaidia katika njia mbili. Inaweza kumulika kilicho karibu na miguu yetu, na inaweza kuangaza mbali zaidi kutuonyesha kilicho mbele yetu. Vivyo hivyo, kanuni za Biblia zinaweza kutusaidia kukabiliana kwa njia inayofaa na matatizo yanayotukumba sasa hivi na hivyo kutusaidia kuwa na tumaini kila siku. Mafundisho ya Biblia yanaweza kuturudishia nguvu na kufanya “moyo ushangilie.” (Zaburi 19:7, 8) Wakati huohuo, Biblia inatuangazia nuru kuhusu kusudi la Mungu lenye kupendeza kwa ajili ya wakati ujao wa wanadamu na dunia. Tumaini hilo linaweza kutupa shangwe ya kudumu na uradhi. 

  •    Waruhusu wengine wakusaidie. Kunapoonekana kuwa hakuna tumaini, ni rahisi kujitenga na watu wa familia na marafiki. Biblia inatuambia kwamba si jambo la hekima kufanya hivyo, kwa sababu tunaweza kutenda na kufanya maamuzi ya kipumbavu. (Methali 18:1) Wapendwa wetu wanaweza kutuimarisha. Wanaweza pia kutoa mapendekezo yanayofaa kuhusu jinsi ya kukabiliana na hali ngumu. (Methali 11:14) Wanaweza kutufariji na kutuchangamsha, na hivyo kutupa nguvu za kuvumilia hadi hali zitakapokuwa sawa.—Methali 12:25

  •    Sali kwa Mungu. Biblia inasema hivi: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye atakutegemeza. Hataruhusu kamwe mwadilifu aanguke.” b (Zaburi 55:22) Kwa kufaa, Yehova anaitwa “Mungu anayetoa tumaini.” (Waroma 15:13) Tunaweza kusali kwake kuhusu ‘wasiwasi wetu wote’ tukiwa na uhakika kwamba anatujali. (1 Petro 5:7, maelezo ya chini) Biblia inasema hivi: “Atawafanya muwe imara, atawatia nguvu, atawapa msingi imara.”—1 Petro 5:10

  •    Tumia majaribu kuimarisha tumaini lako. Biblia inaahidi hivi: “Yule [anayemsikiliza Mungu] ataishi kwa usalama naye hatahangaishwa na woga wa msiba.” (Methali 1:33) Margaret, anayeishi nchini Australia, alipoteza mali nyingi kimbunga kilipopiga nyumba yake. Lakini badala ya kukata tamaa, alijifunza somo muhimu kwamba mali za kimwili ni za muda tu. Baada ya hapo aliazimia hata zaidi kukazia fikira vitu vya maana zaidi, yaani, familia na marafiki wake, uhusiano wake na Mungu, na tumaini lililo katika Biblia.—Zaburi 37:34; Yakobo 4:8

 Biblia inawapa wanadamu wote tumaini gani? 

 Biblia inaahidi kwamba kutakuwa na tumaini zuri kwa wanadamu na dunia. Na wakati huo ujao hauko mbali sana. Bila shaka, matatizo yanayowapata wanadamu leo yanaonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za ulimwengu wa leo. (2 Timotheo 3:1-5) Hivi karibuni, Mungu atadhibiti kabisa mambo yote yanayotendeka duniani na kuondoa ukosefu wa haki na kuteseka. Atafanya hivyo kupitia serikali ya ulimwengu inayoitwa Ufalme wa Mungu. (Danieli 2:44; Ufunuo 11:15) Yesu alikuwa akifikiria kuhusu serikali hiyo ya mbinguni aliposema hivi katika sala ya kielelezo: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani.”—Mathayo 6:9, 10

 Mapenzi ya Mungu kwa wanadamu yanatajwa waziwazi katika Biblia. Ona baadhi ya matatizo ambayo Ufalme wa Mungu utaondoa: 

  •    Hakutakuwa tena na njaa. “Dunia itatoa mazao yake.”—Zaburi 67:6

  •    Hakutakuwa tena na magonjwa. “Hakuna mwenyeji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—Isaya 33:24, maelezo ya chini. 

  •    Hakutakuwa tena na kifo. Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho [ya wanadamu], na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:3, 4

a Tunatumaini kupata kitu tunapokitamani na kuamini kwamba tunaweza kukipata. Pia, tumaini linaweza kuwa kitu tunachotarajia kupata au kusudi la tumaini letu. 

b Yehova ni jina la Mungu kama linavyoonyeshwa katika Biblia.—Zaburi 83:18