Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Biblia Inaweza Kunisaidiaje?​—Sehemu ya 2: Fanya Usomaji wa Biblia Uwe Wenye Kufurahisha

Biblia Inaweza Kunisaidiaje?​—Sehemu ya 2: Fanya Usomaji wa Biblia Uwe Wenye Kufurahisha

 Kijana anayeitwa Will anasema hivi: “Usomaji wa Biblia unaweza kuchosha ikiwa hujui jinsi ya kuisoma.”

 Ungependa kupata siri ya kufanya usomaji wako wa Biblia uwe wenye kufurahisha? Makala hii itakusaidia.

 Fanya usomaji wa Maandiko uwe halisi

 Jihusishe katika usomaji wako. Unaweza kutumia mbinu hii:

  1.   Chagua simulizi la Biblia ambalo ungependa kujifunza. Unaweza kuchagua tukio fulani la Biblia au simulizi katika Injili au simulizi kutoka katika mkusanyo wa drama za usomaji wa Biblia zinazopatikana kwenye jw.org.

  2.   Soma simulizi. Unaweza kusoma kibinafsi au unaweza kusoma simulizi hilo kwa sauti pamoja na marafiki au washiriki wa familia. Mtu mmoja anaweza kusimulia na wengine wakafanya sehemu za wahusika mbalimbali.

  3.   Jaribu mojawapo ya mapendekezo yafuatayo:

    •   Chora picha za kufafanua simulizi hilo. Au chora mfululizo wa picha zinazoonyesha jinsi matukio yalivyotokea. Andika maelezo mafupi yanayofafanua kila picha.

    •   Chora michoro. Kwa mfano, unaposoma kuhusu mhusika mwaminifu, chora mchoro unaounganisha sifa na matendo ya mhusika na baraka alizopata.

    •   Badili simulizi liwe taarifa ya habari. Ripoti tukio kwa njia mbalimbali, na utie ndani “mahojiano” pamoja na wahusika wakuu na watu walioshuhudia.

    •   Ikiwa mhusika mmoja katika simulizi alifanya uamuzi usio wa hekima, lifanye simulizi hilo liishe kwa njia tofauti. Kwa mfano, fikiria simulizi la Petro akimkana Yesu. (Marko 14:66-​72) Petro angewezaje kukabiliana kwa njia nzuri na mkazo aliokabili?

    •   Ikiwa unaweza kuwa mbunifu, jaribu kuandika drama yako ya simulizi la Biblia. Tia ndani masomo unayoweza kupata kutokana na simulizi hilo.​—Waroma 15:4.

      Unaweza kufanya usomaji wa Biblia uwe halisi!

 Chunguza!

 Ikiwa unachunguza habari, unaweza kupata hazina zilizofichika katika simulizi hilo. Kwa kweli, wakati mwingine neno moja au mawili tu ndiyo ya muhimu sana katika simulizi la Biblia.

 Kwa mfano, linganisha Mathayo 28:7 na Marko 16:7.

  •    Kwa nini Marko anatia ndani maneno ya Yesu kwamba karibuni angewatokea wanafunzi wake “na Petro”?

  •  Dokezo: Marko hakushuhudia matukio hayo; alisimuliwa habari hizo na Petro.

  •  Hazina iliyojificha: Kwa nini inawezekana hisia za mashaka za Petro ziliondolewa aliposikia kwamba Yesu alitaka kumwona tena? (Marko 14:66-​72) Yesu alijithibitishaje kuwa rafiki wa kweli wa Petro? Unaweza kumwigaje Yesu na kuwa rafiki mzuri wa watu wengine?

 Ukifanya usomaji wa Biblia uwe halisi na kuchunguza habari, usomaji huo wa Biblia utakuwa wenye kufurahisha sana!