Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Kuwachezea Wengine Kimapenzi Kuna Madhara?

Je, Kuwachezea Wengine Kimapenzi Kuna Madhara?

 Kuchezea wengine kimapenzi ni nini?

 Baadhi ya watu wanafikiri kwamba kumchezea mtu kimapenzi ni kumwonyesha mtu wa jinsia tofauti kwa maneno au matendo kwamba unavutiwa naye kimahaba. Je, ni vibaya kuonyesha kwamba unavutiwa kimapenzi na mtu fulani? Si katika kila kisa. Msichana anayeitwa Ann anasema hivi: “Ikiwa uko tayari kuanzisha uchumba na unavutiwa na mtu fulani, kuna njia nyingine ya kujua ikiwa nyote wawili mna hisia zinazofanana?”

 Hata hivyo, katika makala hii, tutazungumzia kuwachezea wengine kimapenzi kwa njia inayoonyesha kwamba unavutiwa na mtu kimahaba lakini kumbe huna kusudi la kuendeleza uhusiano na mtu huyo.

 “Kuna tofauti kati ya kumwonyesha mtu uangalifu wa pekee kwa sababu unataka kuanzisha uhusiano wa kimapenzi pamoja naye, na kumfanya mtu ahisi kwamba unavutiwa naye kisha kwa ghafla unamwacha kwa sababu hukukusudia kuanzisha uhusiano naye.”​—Deanna.

 Kwa nini watu fulani huwachezea wengine kimapenzi?

 Baadhi ya watu huwachezea wengine kimapenzi ili wajihisi vizuri. “Kutambua kwamba unaweza kumfanya mtu apendezwe nawe kunaweza kukuchochea ufanye hivyo zaidi,” anasema msichana anayeitwa Hailey.

 Hata hivyo, ikiwa kwa makusudi unajionyesha kuwa unavutiwa kimapenzi na mtu wakati kwa kweli huvutuwi naye, unaonyesha wazi kwamba hujali hisia za mtu huyo. Pia uwezo wako wa kufanya maamuzi utatiliwa shaka. Biblia inasema hivi: “Mtu ambaye amepungukiwa moyoni huonea shangwe upumbavu.”​—Methali 15:21.

 Hailey anasema hivi: “Kuchezea wengine kimapenzi huanza kama mchezo usio na madhara lakini hatimaye unakuwa hatari sana.”

 Kuna madhara yoyote?

  •   Kuchezea wengine kimapenzi huharibu sifa zako nzuri.

     “Mtu anayewachezea wengine kimapenzi huonekana kuwa hajiamini na pia hajakomaa. Unahisi kwamba yeye si mwaminifu kwako, anajaribu tu kupata kitu fulani kutoka kwako.”​—Jeremy.

     Biblia inasema hivi: “Upendo . . . hautafuti faida zake wenyewe.”​—1 Wakorintho 13:​4, 5.

     Jambo la kufikiria: Ni maneno gani au matendo gani yanayoweza kufanya uonekane kama mtu ambaye huwachezea wengine kimapenzi?

  •   Kuchezea kimapenzi humuumiza unayemchezea.

     “Kukutana na mtu anayewachezea wengine kimapenzi, hunifanya nijaribu kumwepuka. Inaonekana anaongea na mimi kwa sababu tu mimi ni msichana. Watu wanaowachezea wengine kimapenzi hawanijali; kitu pekee wanachojali ni kutosheleza hisia zao ili wajihisi vizuri.”​—Jaqueline.

     Biblia inasema hivi: “Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali ile ya yule mtu mwingine.”​—1 Wakorintho 10:24.

     Jambo la kufikiria: Umewahi kufikiri mtu fulani anavutiwa nawe kimapenzi lakini hatimaye ukagundua hakuwa akivutiwa nawe? Ikiwa ndivyo, ulihisije baada ya kugundua jambo hilo? Unaweza kuepuka jinsi gani kumuumiza mtu mwingine kwa njia hiyo?

  •   Kuchezea wengine kimapenzi kunaharibu matarajio yako ya kupata mwenzi anayependezwa nawe kikweli.

     “Hakuna mtu ambaye angependa kufunga ndoa au kuanzisha uchumba na mtu anayewachezea wengine kimapenzi. Nitawezaje kumfahamu vizuri au kumwamini mtu ikiwa ananichezea tu kumapenzi?”​—Olivia.

     Katika Biblia, mtunga-zaburi Daudi alisema hivi: “Siingii pamoja na wale wanaoficha jinsi walivyo.”​—Zaburi 26:4.

     Jambo la kufikiria: Wanaochezea wengine kimapenzi wanawavutia watu wa aina gani? Je, wewe ungependa kumvutia mtu anayewachezea wengine kimapenzi?