Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Ni Urafiki wa Kawaida au wa Kimapenzi?—Sehemu ya 1: Ananipa Ishara Gani?

Je, Ni Urafiki wa Kawaida au wa Kimapenzi?—Sehemu ya 1: Ananipa Ishara Gani?

 Unampenda sana mtu fulani wa jinsia tofauti, na unajua kwamba yeye pia anakupenda. Isitoshe, huwa mnatumiana jumbe mara kwa mara, mnakuwa pamoja kwenye mikusanyiko ya watu . . . , na baadhi ya jumbe anazokutumia ni za kimapenzi.

 Hivyo unaamua kumuuliza mtu huyo kuhusu uhusiano wenu, ili kupata uhakika ikiwa yeye pia anahisi hivyo. Anakujibu hivi: “Nakuona kama rafiki tu​—hakuna jambo lingine.”

 Jinsi unavyohisi

 “Nilikasirika sana​—nilimkasirikia yeye na kujikasirikia mimi mwenyewe! Tulikuwa tukitumiana ujumbe kila siku, na alionyesha anapendezwa na mimi. Hivyo, nilisitawisha hisia kumwelekea.”​—Jasmine.

 “Mimi na msichana mmoja tulikuwa na kawaida ya kuwasindikiza kwenye matembezi ndugu na dada fulani waliokuwa wakichumbiana. Nyakati nyingine ilionekana kama sisi pia tuna urafiki wa kimapenzi. Tulikuwa tukizungumza sana pamoja, na kisha tukaanza kutumiana jumbe fupi kwenye simu. Haikuwa rahisi kwangu kukubali msichana huyo aliponiambia kwamba ananiona kuwa rafiki tu na kwamba alikuwa na urafiki wa kimapenzi na mtu mwingine kipindi hicho chote.”​—Richard.

 “Kijana fulani alikuwa akinitumia jumbe fupi kwenye simu kila siku, na nyakati nyingine sote tulitumiana jumbe za ‘kimapenzi.’ Lakini nilipomweleza jinsi nilivyohisi kumwelekea, alicheka na kusema, ‘sitaki kuanzisha urafiki wa kimapenzi na mtu yeyote kwa sasa!’ Nililia kwa muda mrefu sana.”​—Tamara.

 Jambo kuu: Unapofikiri kwamba una uhusiano wa kipekee na mtu fulani na kisha unatambua kwamba ni wewe tu mwenye hisia za kimapenzi, ni jambo la kawaida kukasirika, kuaibika, na hata kuhisi umesalitiwa. “Nilivunjika moyo sana jambo hilo lilipotokea kwangu, na kwa kweli liliniumiza moyo sana,” anasema kijana anayeitwa Steven. “Ilichukua muda fulani kabla niweze tena kumwamini mtu mwingine.”

 Kwa nini inatokea

 Kutumiana jumbe fupi na kutumia mitandao ya kijamii inafanya iwe rahisi kwako kukuza hisia kumwelekea mtu fulani ambaye kihalisi havutiwi na wewe kimapenzi. Fikiria yale ambayo vijana wenzako wanasema.

 “Mtu anaweza tu kuanza kukutumia ujumbe kwa kuwa hana jambo lingine la kufanya wakati huo, lakini unaweza kuona jambo hilo kuwa ishara ya yeye kupendezwa nawe. Na ikiwa anakutumia ujumbe kila siku, unahisi kimakosa kwamba anakuona kuwa mtu wa pekee sana kwake.”​—Jennifer.

 “Mmoja anaweza kuwa anataka urafiki wa kimapenzi, wakati mwingine anataka tu mtu wa kuzungumza naye, atakayemtia moyo.”​—James.

 “Ujumbe rahisi kama ‘usiku mwema’ unaweza kuonwa kuwa ujumbe wa kimapenzi, lakini ujumbe huohuo ungeweza kutumwa kwa wororo na mtu anayeuza bidhaa kupitia simu.”​—Hailey.

 “Jumbe fupi yenye alama ya tabasamu inaweza kumaanisha ama ‘ninakuonyesha fadhili’ au ‘ninakuchezea kimapenzi.’ Wakati mwingine mtu anayepokea ujumbe huo anaweza kuhisi kwamba unamchezea kimapenzi.”​—Alicia.

 Jambo kuu: Tofautisha kati ya kuelekezewa fikira na kupendwa.

 Si rahisi kufanya hivyo. Biblia inasema hivi: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” (Yeremia 17:9) Moyo unaweza kukufanya usitawishe uhusiano wa kimahaba wa kuwaziwa tu akilini mwako.

 Unachoweza kufanya

  •   Ona mambo kihalisi. Chunguza uhusiano wenu kihalisi. Jiulize, ‘Nina sababu za msingi za kufikiri kwamba mtu huyu ananitendea kwa njia ya pekee tofauti na wengine?’ Usiruhusu hisia zako zitawale “nguvu zako za kufikiri.”​—Waroma 12:1.

  •   Uwe na utambuzi. Kati ya ishara zote zinazokufanya uhisi kwamba huenda wewe ni zaidi ya rafiki wa kawaida, chunguza kwa makini zile zinazokufanya utilie shaka hisia hizo. Usifikiri kwamba kwa kuwa wewe unahisi hivyo kumwelekea mtu fulani, ndivyo yeye pia anavyohisi kukuelekea.

  •   Uwe na subira. Subiri mpaka mtu atakapokwambia waziwazi kwamba anataka kukujua zaidi ili kuanzisha urafiki wa kimapenzi, ndipo uanze kuruhusu hisia za kimahaba zisitawi.

  •   Uwe mnyoofu. Biblia inasema kwamba kuna “wakati wa kusema.” (Mhubiri 3:7) Ikiwa unataka kujua kama mtu anakuona kuwa zaidi ya rafiki wa kawaida, zungumza waziwazi na mtu huyo. “Ikiwa yeye hana hisia kama zako, ni bora kujua mapema na kuumia kidogo sasa, kuliko kujua baada ya miezi kadhaa kwamba hapendezwi na wewe kimahaba.”

 Jambo kuu: Methali 4:​23 inasema, “Linda moyo wako.” Ikiwa unahisi unavutiwa na mtu fulani, chunguza ikiwa mtu huyo anavutiwa na wewe pia. Kuruhusu hisia za kimapenzi zitie mizizi kabla ya kujua ikiwa anavutiwa nawe ni sawa na kujaribu kupanda mmea kwenye mwamba.

 Ukitambua kwamba mtu fulani ana hisia za kimapenzi kukuelekea​—na ikiwa una umri wa kutosha na uko tayari kuanzisha urafiki wa kimapenzi​—utaamua ikiwa unataka kuendeleza urafiki huo. Kumbuka kwamba ndoa imara hufanywa na mume na mke ambao wana miradi sawa ya kiroho na ambao ni wanyoofu na wanaambiana ukweli. (1 Wakorintho 7:​39) Kwa kweli, hatuna shaka kwamba wao walianza mahusiano wakiwa marafiki wazuri na wataendelea kuwa marafiki wazuri.​—Methali 5:​18.