Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Ngono ya Mdomo Ni Ngono?

Je, Ngono ya Mdomo Ni Ngono?

 Kulingana na ripoti ya Marekani ya Centers for Disease Control and Prevention, karibu nusu ya waliohojiwa, wenye umri wa miaka 15 hadi 19, wamefanya ngono ya mdomo. Sharlene Azam, mwandishi wa kitabu Oral Sex Is the New Goodnight Kiss, anasema hivi: “Ukizungumza na matineja [kuhusu ngono ya mdomo] watakuambia si jambo la ajabu. Kwa kweli, hawaioni kuwa ngono.”

 Una maoni gani?

 Jibu ndiyo au la kwa maswali yafuatayo.

  1.   Je, msichana anaweza kupata mimba kwa kufanya ngono ya mdomo?

    1.   Ndiyo

    2.   La

  2.   Je, ngono ya mdomo ina madhara yoyote kiafya?

    1.   Ndiyo

    2.   La

  3.   Je, ngono ya mdomo ni ngono?

    1.   Ndiyo

    2.   La

 Ukweli wa mambo ni nini?

 Linganisha majibu yako na majibu yafuatayo.

  1.   Je, msichana anaweza kupata mimba kwa kufanya ngono ya mdomo?

     Jibu: La. Hiyo ni sababu moja inayowafanya watu wengi wakate kauli isiyofaa kwamba ngono ya mdomo haina madhara yoyote.

  2.   Je, ngono ya mdomo ina madhara yoyote kiafya?

     Jibu: Ndiyo. Mtu anayeshiriki ngono ya mdomo anaweza kupata mchochota wa ini (aina ya A au B), vipele au vidonda kwenye viungo vya uzazi, kisonono, virusi vya Ukimwi, na kaswende.

  3.   Je, ngono ya mdomo ni ngono?

     Jibu: Ndiyo. Jambo lolote linalohusu viungo vya uzazi vya mtu mwingine​—kutia ndani ngono, ngono ya mdomo, ngono ya mkundu, na kumpiga punyeto mtu mwingine​—ni ngono.

 Kwa nini ni muhimu kujua?

 Fikiria maandiko kadhaa katika Biblia yanayohusiana na habari kuhusu ngono ya mdomo.

 Biblia inasema hivi: “Haya ndiyo mapenzi ya Mungu, kwamba . . . mjiepushe na uasherati.”​—1 Wathesalonike 4:​3.

 Neno la lugha ya awali lililotafsiriwa “uasherati” linamaanisha mahusiano yote nje ya ndoa, kutia ndani ngono, ngono ya mdomo, ngono ya mkundu, na kumpiga punyeto mtu mwingine. Mtu anayefanya uasherati anaweza kupatwa na matokeo mabaya sana, na tokeo baya zaidi ya yote ni kuharibika kwa urafiki wake pamoja na Mungu.​—1 Petro 3:12.

 Biblia inasema hivi: “Yeye aliye na mazoea ya kufanya uasherati anautendea dhambi mwili wake mwenyewe.”​—1 Wakorintho 6:18.

 Ngono ya mdomo inaweza kusababisha matokeo mabaya sana ya kimwili na kiroho. Inaweza pia kukuathiri kihisia. Kitabu Talking Sex With Your Kids, kinasema hivi: “Kuhisi kuwa umetumiwa, kuwa na majuto, au kuhisi kwamba umekosa ulinzi hakutokei tu kwa wale wanaofanya tendo la ngono kupitia tu uke. Hisia zote zisizofaa zinazotokana na kufanya ngono chini ya hali zisizofaa zinaweza kumpata yeyote anayefanya aina yoyote ya ngono. Ngono ni ngono.”

 Biblia inasema hivi: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe.”​—Isaya 48:​17.

 Je, unaamini kwamba sheria za Mungu kuhusu ngono ni zenye faida kwako? Au unafikiri zina vizuizi vingi? Ili kukusaidia kujibu maswali hayo, fikiria barabara yenye magari mengi iliyo na alama nyingi za barabarani. Je, unaona alama hizo kuwa kizuizi au ulinzi? Ni nini kingetokea ikiwa wewe na madereva wengine mngezipuuza?

Sheria za barabarani zinadhibiti uhuru wako, lakini zinakulinda. Vivyo hivyo, sheria za Mungu zinakudhibiti, lakini zinakulinda

 Vivyo hivyo na viwango vya Mungu. Ukivipuuza, bila shaka utavuna unachopanda. (Wagalatia 6:7) Kitabu kinachoitwa Sex Smart kinasema hivi: “Kadiri unavyopuuza mambo unayoamini na kujihusisha na mambo ambayo unahisi si sawa, ndivyo utakavyokosa kujiheshimu. Tofauti na hilo, ukiishi kupatana na viwango vya Mungu, utaonyesha kwamba wewe ni mwenye maadili thabiti. Zaidi ya hilo, utadumisha dhamiri safi.​—1 Petro 3:16.