Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Nifanye Nini Ikiwa Ninaanguka Mitihani?

Nifanye Nini Ikiwa Ninaanguka Mitihani?

 “Mimi huwaona wanafunzi wenzangu wakiketi darasani bila kitabu huku wakiwa wamevaa vifaa vya masikioni vya kusikiliza muziki wakati ambapo mwalimu anafundisha. Halafu wanafunzi hao wanashangaa kwa nini hawafaulu! Kisha kuna watu kama mimi ambao tunasoma kupita kiasi na bado tunaanguka mtihani. Kwa kweli sielewi kwa nini hilo hutokea. Ninahisi vibaya sana ninapopata alama mbaya baada ya kukesha kwa juma moja nikisoma.”—Yolanda.

 Je, umewahi kupitia hali kama ya Yolanda? Ukweli ni kwamba unaweza kuvunjika moyo kuanguka mtihani mmoja au kwa mfululizo.

 Baadhi ya vijana ambao hawafaulu shuleni wanaweza kuacha kujaribu kupata alama nzuri zaidi. Huenda wengine wakaacha kwenda shule kabisa. Ingawa huenda mtu akataka kufanya mambo hayo, kuna njia nyingine ya kushughulikia tatizo hilo. Fikiria hatua sita unazoweza kuchukua ili kuboresha alama zako.

 Unachoweza kufanya

  •   Usikose kipindi chochote darasani. Kufanya hivyo kunaweza kuonekana kuwa jambo la kawaida tu, lakini ukikosa vipindi vingi, bila shaka utapata alama za chini.

     “Shuleni, wanafunzi ambao hawakujali watapata alama gani mara nyingi ndio waliokosa kufika shuleni, kwa hiyo, ni kama tu walijiangusha mtihani.”—Matthew.

     Kanuni ya Biblia: “Lolote analopanda mtu, ndilo atakalovuna pia.”—Wagalatia 6:7.

  •   Hakikisha kwamba unajifunza yote uwezayo katika kila kipindi. Ni jambo zuri kuwepo kwa ajili ya kila kipindi, lakini hakikisha kwamba unajifunza yote uwezayo katika kila kipindi. Andika mambo makuu. Jaribu kufuata mtiririko wa mawazo ambayo mwalimu anafundisha. Ikiwa inaruhusiwa, uliza maswali.

     “Mimi huuliza maswali mengi darasani kwa sababu nimeona kwamba mwalimu huelezea somo zaidi anapotambua kwamba mwanafunzi hajalielewa.”—Olivia.

     Kanuni ya Biblia: “Kazieni uangalifu jinsi mnavyosikiliza.”—Luka 8:18.

  •   Usiibe mtihani. Kuiba mtihani ni ukosefu wa unyoofu. Kuna njia nyingi za kuiba mtihani. Njia moja ni kuangalia karatasi ya mwenzako na kuinakili. Mbali na kwamba huo si unyoofu, hakukunufaishi kwa njia yoyote.

     “Ikiwa huelewi jambo, usiibe majibu kutoka kwa karatasi ya mwanafunzi mwenzako. Unapoiba, hujisaidii kwa njia yoyote. Badala ya kujifunza kutatua matatizo, unajifunza kuwategemea wengine.”—Jonathan.

     Kanuni ya Biblia: “Fanya kazi yako mwenyewe vizuri, kisha utakuwa na kitu cha kujivunia.”—Wagalatia 6:4, Contemporary English Version.

  •   Usikose kufanya kazi ya shuleni. Ikiwezekana, fanya kazi za shuleni kabla ya mambo mengine—hasa burudani. a Ukimaliza kazi za shule kwanza, utafurahia burudani hata zaidi!

     “Nilitanguliza kazi za shule, na hilo lilinisaidia kuboresha alama zangu. Nilipofika nyumbani, mara nyingi nilitaka kulala kidogo au kusikiliza muziki. Lakini nilijaribu kufanya kazi za shule kwanza kisha nipumzike.”—Calvin.

     Kanuni ya Biblia: “Mhakikishe mambo muhimu zaidi.”—Wafilipi 1:10.

  •   Omba msaada. Usione aibu kuomba msaada kutoka kwa wengine. Waombe wazazi wako ushauri. Mwombe mwalimu wako akusaidie kupata alama nzuri zaidi. Katika visa fulani, unaweza kupata msaada kutoka kwa mwalimu wa masomo ya ziada.

     “Mwendee mwalimu moja kwa moja. Mwombe akusaidie kuelewa somo fulani zaidi na kuboresha alama zako. Kuna uwezekano mkubwa kwamba mwalimu atavutiwa na azimio lako la kufaulu naye atakusaidia.”—David.

     Kanuni ya Biblia: “Mambo hufanikiwa kupitia washauri wengi.”—Methali 15:22.

  •   Tumia vizuri fursa zote unazopata. Katika nchi fulani, mitihani ina maswali ya ziada ambayo inaweza kuboresha alama zako. Unaweza pia kujitolea kufanya migawo fulani ambayo itakuongezea alama. Ukianguka mtihani, huenda ukaruhusiwa kuurudia unapoomba.

    Kuboresha alama zako ni kama kujifunza kucheza ala ya muziki. Ni kazi ngumu lakini faida ni kubwa

     “Ikiwa ninataka kuboresha alama zangu katika somo fulani, lazima nichukue hatua ya kwanza. Mimi humuuliza mwalimu wangu ikiwa kuna migawo ambayo itaniongezea alama au ikiwa ninaweza kurudia kazi fulani ili nipate alama za ziada.”—Mackenzie.

     Kanuni ya Biblia: “Kila aina ya kazi ngumu ina faida.”—Methali 14:23.

a Ili upate mapendekezo hususa ya jinsi ya kuboresha ustadi wako wa kujifunza, ona makala yenye kichwa “Vijana Huuliza . . . Ninaweza Kumalizaje Kazi za Shule?