Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Mateso​​—Ni Malipizi Kutoka kwa Mungu?

Mateso​​—Ni Malipizi Kutoka kwa Mungu?

LUZIA NI KILEMA KWENYE MUGUU WAKE WA KUSHOTO. Wakati alikuwa mutoto mudogo, alipata ugonjwa wa polio, ugonjwa wenye kuambukiza sana wenye unashambulia mufumo wa neva (système nerveux). Wakati alikuwa na miaka 16, mwanamuke mwenye Luzia alikuwa anatumikia alimuambia, “Mungu alikupatia malipizi ya ugonjwa wa kupooza kwa sababu haukukuwa unatii mama yako na kwa sababu ulikuwa mutoto mubaya.” Kumepita miaka, Luzia angali anakumbuka namna maneno hayo yalimuumiza sana.

WAKATI DAMARIS ALIAMBIWA KAMA ALIKUWA NA KANSERE KATIKA UBONGO, baba yake alimuuliza hivi: “Ulifanya nini ili upatwe na jambo hili? Unapaswa kuwa ulifanya jambo fulani la mubaya sana. Ndiyo sababu Mungu iko anakupatia malipizi.” Damaris aliumizwa sana na maneno ya baba yake.

Kwa miaka mingi watu wameamini kuwa magonjwa ni malipizi kutoka kwa Mungu. Kitabu Us et coutumes des pays bibliques (katika kiingereza) kinasema kama watu wengi wenye waliishi katika siku za Kristo waliamini kuwa mutu alipata “magonjwa kwa sababu ya zambi yake, ao ya watu wa familia yake, na kama magonjwa hayo yalitumwa ili kumupatia malipizi kwa sababu ya zambi hiyo.” Kitabu Medieval Medicine and the Plague kinasema kuwa mamia ya miaka kisha Kristo “watu fulani waliamini kuwa Mungu alileta pigo ili kuwapatia malipizi kwa sababu ya makosa yao.” Kwa hiyo, wakati mamilioni ya watu walikufa kwa sababu ya ugonjwa fulani wenye kuambukiza sana katika karne ya 14, je, ni Mungu ndiye alikuwa anahukumu watu wabaya? Ao ugonjwa huo uliletwa na mikrobi, kama vile uchunguzi wa wanganga ulikuwa umeonyesha? Watu fulani wanaweza kujiuliza, je, Mungu anatumiaka kabisa magonjwa ili kufanya watu wateseke kwa sababu ya zambi zao? *

FIKIRIA JAMBO HILI: Juu ya nini Yesu aliponyesha wagonjwa ikiwa magonjwa na mateso ni malipizi kutoka kwa Mungu yenye watu wanastahili? Hilo halingefanya watu waone kuwa Mungu hana haki? (Matayo 4:23, 24) Yesu hangepinga hata kidogo matendo ya Mungu. Alisema hivi: “Sikuzote ninafanya mambo yenye kumupendeza” na, “ninafanya kama vile Baba aliniamuru.”​—Yohana 8:29; 14:31.

Biblia iko wazi. Yehova Mungu “hana ukosefu wa haki hata kidogo.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Kwa mufano, Mungu hawezi hata kidogo kutokeza aksidenti ya avion, na kuua watu wenye hawana kosa kwa sababu anapenda kupatia malipizi mutu fulani mwenye iko katika avion hiyo! Kupatana na haki ya Mungu, Abrahamu, mutumishi muaminifu wa Mungu, alisema kama Mungu hawezi hata kidogo ‘kuharibu mwenye haki pamoja na muovu.’ Alisema kama hilo ni jambo “lenye haliwezi kuwaziwa.” (Mwanzo 18:23, 25) Biblia inasema pia kama Mungu hawezi ‘kutenda uovu’; hawezi ‘kufanya makosa.’​—Yobu 34:10-12.

MAMBO YENYE BIBLIA INATUFUNDISHA KUHUSU MATESO

Mateso yenye tunapata haiko malipizi yenye Mungu anatupatia kwa sababu ya zambi. Maneno ya Yesu yalikuwa wazi wakati yeye na wanafunzi wake waliona mwanaume mwenye alikuwa kipofu tangu kuzaliwa. “Wanafunzi wake wakamuuliza: ‘Rabi, ni nani alitenda zambi, ni mutu huyu ao ni wazazi wake, na hivyo akazaliwa kipofu?’ Yesu akajibu: ‘Mutu huyu hakutenda zambi wala wazazi wake, lakini ilikuwa vile kusudi kazi za Mungu zifikie kufunuliwa kupitia yeye.’”​—Yohana 9:1-3.

Kwa sababu ya mawazo ya mubaya yenye watu wengi walikuwa nayo, inawezekana wanafunzi wa Yesu walishangaa wakati aliwaambia kuwa mwanaume huyo hakupata magumu hayo kwa sababu ya zambi zake ao zambi za wazazi wake. Yesu aliponyesha mwanaume huyo kipofu, lakini zaidi ya hilo, kwa kufanya hivyo alitupilia mbali mawazo yenye makosa ya kuwa mateso ni malipizi kutoka kwa Mungu. (Yohana 9:6, 7) Wale wote wenye wanapambana na magonjwa hatari leo wanaweza kutiwa moyo kwa kujua kama haiko Mungu ndiye anawaletea mateso hayo.

Ikiwa watu waligonjwa kwa sababu Mungu aliwapatia malipizi juu ya makosa yao, juu ya nini Yesu aliwaponyesha?

Maandiko yanatuhakikishia

  • “Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu, wala yeye mwenyewe hamujaribu mutu yeyote.” (YAKOBO 1:13) Kwa kweli, “mambo maovu” yenye yamewapiga wanadamu kwa miaka mingi, kutia ndani magonjwa, maumivu, na kifo, vitaondolewa hivi karibuni.

  • Yesu Kristo ‘aliponyesha wote wenye walikuwa wagonjwa.’ (MATAYO 8:16) Kwa kuponyesha wale wote wenye walikuja kwake, Mwana wa Mungu alionyesha mambo yenye Ufalme wa Mungu utatimiza katika dunia yote.

  • “[Mungu] atapanguza kila chozi katika macho yao, na kifo hakitakuwa tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu havitakuwa tena. Mambo ya zamani yamepita kabisa.”​—UFUNUO 21:3-5.

NI NANI ANATULETEA MATESO?

Sasa, sababu gani wanadamu wanapata maumivu na mateso mengi? Wanadamu wamejiuliza ulizo hilo kwa mamia ya miaka. Ikiwa haiko Mungu ndiye anatuletea mateso, ni nani anayaleta? Habari yenye kufuata itajibia maulizo hayo.

^ fu. 4 Hata kama zamani kuko wakati Mungu alipatia watu malipizi kwa sababu ya zambi fulani, Biblia haionyeshe kama leo Yehova iko anatumia mambo kama vile magonjwa ao misiba ili kupatia watu malipizi kwa sababu ya zambi zao.